September 1, 2019




HARUNA Shamte, mtaalamu wa mipira iliyokufa ambaye msimu uliopita alikuwa ndani ya Lipuli sasa ujuzi wake huo utaonekana ndani ya kikosi cha Mabingwa watetezi Simba.

Ana uwezo mkubwa wa kutumia mguu wa kulia ambapo amefunga jumla ya mabao matano alipokuwa Lipuli na yote ilikuwa ni mipira ya nje ya 18 tena ya adhabu.

Katika mabao hayo mawili alifunga kwenye michezo ya Ligi Kuu Bara ambayo ilichezwa Uwanja wa Samora kwenye mechi dhidi ya Singida United pamoja na mchezo wao dhidi ya Yanga ambapo Klaus Kindoki alikuwa langoni.

Mabao mengine matatu alifunga kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho na alitimiza wajibu wake kwa kuipeleka timu ya Lipuli hatua ya fainali na ilipoteza mbele ya Azam FC.

Amewahi kuzitumikia timu mbalimbali Bongo ikiwa ni pamoja na Mbeya City, JKT Ruvu na Simba msimu wa 2014/15 sasa amerejea nyumbani ambapo anakutana na mabeki kama Pascal Wawa, Yusuph Mlipili, Gadiel Michael, Mohamed Hussen na mkongwe Erasto Nyoni, huyu hapa anafunguka:-

“Kazi kubwa ambayo nimekuwa nikifanya uwanjani wengi wameipokea vizuri na imenipa matokeo mazuri ambayo kwa sasa yanaonekana hivyo kwangu ni kitu cha kujivunia na ninafurahi kufanya hivyo.

Polisi Tanzania walikuwa wanakuhitaji dili iliishia wapi?

“Kweli ilikuwa inasemwa hivyo na ukiangalia kwamba kwa sasa pale mwalimu wao ni mwalimu wangu wa timu ya zamani (Seleman Matola) namheshimu na ninamkubali ila mwisho wa siku nimetua Simba na maisha yanaendelea.

Kwa nini umechagua kutua Simba?

“Kazi yangu mimi ni mpira kikubwa ambacho ninaangalia ni dau, niliwekewa dau kubwa nikakubali kusaini hivyo sina mashaka na chaguo langu kwa sasa ambalo nimelifanya.

Unadhani kipi unachohofia ndani ya Simba?

“Kwa sasa bado kwa kuwa ligi bado mbichi ila tuna kazi kubwa ya kufanya na mambo ni mengi kwa sasa hivyo suala la hofu kwangu hakuna kitu kama hicho kwa kuwa yote ambayo yanatokea ni mipango ya Mungu.

Ulikuwa na uhakika wa namba ndani ya Lipuli je nafasi yako ndani ya Simba unaionaje?

“Kuanza ama kutokuanza ni maandalizi tu, naona kuna wachezaji wengi wazuri ambao wamesajiliwa hilo sio jambo baya kwani hata nilikotoka Lipuli kulikuwa na mabeki wazuri wachezaji wazuri ambao tulikuwa tunafanya vizuri ila mwisho wa siku kazi ya kupanga kikosi ipo chini ya mwalimu.

Wingi wa mashabiki na ukubwa wa timu ya Simba kwako unakupa picha gani?

“Natambua ni timu kubwa ila nimewahi kuitumikia zamani hivyo sina mashaka na presha ambazo zipo ninachokifanya kwa sasa ni kujiaandaa vema na kupambana ili kuwa bora.

“Mashabiki ni watu muhimu kwenye soka kwani ni mchezaji wa 12 hivyo wingi wao na sapoti yao kwetu ni muhimu katika kila jambo.

Umesajiliwa dakika za mwisho je unaamini ulikuwa kwenye mpango wa Simba?

“Kuwa kwenye mpango ama kutokuwa ndani ya mpango hilo mimi sijui, ninachojua kwa sasa mipango imetimia na nipo ndani ya Simba kwa sasa.

“Kikubwa kwa mchezaji anachotazama ni sehemu ambayo anakwenda kucheza pamoja na thamani yake hivyo kama nimepata dili la kujiunga na Simba sikuwa na namna ya kugoma eti kwa sababu nimechelewa kusajiliwa.

Mashabiki wa Simba unawaambia nini?

“Mshikamano na umoja ni vitu vya msingi, sapoti yao ni kubwa na wanaonyesha kwa vitendo hivyo napenda kuwaomba waendelee na moyo huo kwa ajili ya kuipa sapoti timu.

Mabao yako mengi ni mipira iliyokufa kwa nini?

“Wakati ule mwalimu (Matola) alikuwa ananipa kazi ya kufanya na nikiwa mazoezini nilikuwa nafunga mengi, hivyo mbinu bado ipo na ujuzi haupotei ni jambo la kusubiri na kuona kikubwa subira na dua,” anamalizia Shamte.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic