March 25, 2020



JONAS Mkude kiungo mkali wa Simba wiki iliyopita aliendelea kugonga vichwa vya habari kuhusiana na nidhamu yake.

Inawezekana wengi wamesahau lakini ukweli ni kwamba kiungo huyu amekuwa na mwendelezo wa utovu wa nidhamu kwa baada ya hivi karibuni kushindwa kuungana na wenzake kwenye kambi ya timu ya Taifa, Taifa Stars.

Jina la kiungo huyo lilikuwa kati ya wachezaji 35 walioitwa Stars na kocha wa kikosi hicho, Etienne Ndayiragije lakini wenzake walijiunga na baadhi walitoa taarifa kutokana na kuzuiwa kutoka sehemu waliyopo kutokana na mlipuko wa Virusi vya Corona, hao wengi ni wale wa kimataifa.

Nakumbuka pia wakati fulani aliitwa timu ya taifa na Kocha Emmanuel Amunike, yeye pia alionekana kulalamikia nidhamu za baadhi ya wachezaji kuwa hawakwenda kambini huku wakishindwa kutoa sababu za msingi akiwemo Mkude japokuwa kocha hakumtaja hadharani.

Lakini kumbuka kiungo huyo, miezi iliyopita hakusafiri na timu yake ya Simba akiwa sambamba na wachezaji wenzake, Clatous Chama, Erasto Nyoni na Gadiel Michael kwenda kucheza mechi za Kanda ya Ziwa ambazo ilikuwa dhidi ya Kagera Sugar na Biashara United.

Lakini akiwa bado anahojiwa juu ya suala hilo, timu iliporudi Dar es Salaam kuendelea na maandalizi ya mechi kuna siku akachelewa kwenye mazoezi ambayo yalikuwa yanafanyika Viwanja vya Gymkhana, Posta jijini Dar.

Hii si mara ya kwanza kwa kiungo huyo kukumbwa na matukio ya utovu wa nidhamu, licha ya kuwa amekuwa na mchango mkubwa kikosini humo na ndiye mchezaji mkongwe Simba, nafikiri anahitaji msaada wa kuwekwa sawa.

Mkude ambaye amewahi kuwa nahodha wa Simba kabla ya kupokwa na kupewa John Bocco, ni role model wa vijana wengi mtaani ambao wanachipukia sasa kwa hiki anachokifanya sasa hivi siyo sawa kabisa, anapaswa kubadilika.

Ifikie wakati wachezaji wanapaswa kujulishwa umuhimu wa kuitumia timu ya taifa hasa kwa wale wenye ndoto za kucheza soka la kulipwa nje.

Ni ngumu kama malengo yako ni kucheza nje kupuuzia kuichezea timu yako ya taifa kwani moja kati ya vipengele wanavyoangalia ni nafasi yako kwenye timu ya taifa sasa kama wewe unaona sasa hivi huna mpango na taifa lako andika umeumia.

Hii siyo kwa Mkude tu ni kwa wachezaji wote Tanzania, hili ni somo inawezekana wengi hawajui, lakini ukweli ndiyo huu.

Sasa matukio kama haya ukiangalia yanaripotiwa kwenye vyombo vya habari hivyo inapotokea anahitajika kwenda kucheza soka la kulipwa inaweza kumpa shida kidogo kwani klabu nyingi Ulaya zimekuwa zikizingatia nidhamu ya hali ya juu.

Mkude bado ni kijana mdogo, taifa na klabu yake ya Simba bado zinahitaji huduma yake katika kuhakikisha soka letu linapiga hatua.
Hii kwa wote; Nidhamu ni muhimu sana kazini. Starehe zipo, fanya kwa wakati wako lakini linapokuja suala la kazi basi fuata misingi ili usipotee.

Kama leo ligi zimesimama kutokana na mlipuko wa Virusi vya Corona basi wachezaji mzingatie suala la mazoezi ili kudumisha viwango vyenu, uzuri mchezo wa soka unachezwa wazi hivyo ni vyema mkaendelea na mazoezi sehemu ambazo hazina hatari ya kupata maambukizi hayo.

Kila mmoja akili kichwani mwake, najua wapo ambao wanaendelea na matizi na wapo ambao wanakaa tu wakisubiri ligi zirudi, siyo sawa linda kipaji chako kwa kufanya mazoezi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic