May 20, 2020



 Na Saleh Ally
HAKIKA maisha yanabadilika kwa kasi kubwa na ukitaka kuishi kwa amani katika kipindi hiki lazima ukubaliane na hali halisi ilivyo.

Hakuna ubishi tena kwamba ni lazima uishi katika kipindi hiki ukiamini Corona ni tatizo na lazima kuwe na tofauti ya maisha na yale kabla ya kuibuka kwa Covid 19 ambayo sasa inaitikisa dunia.

Watanzania wapenda michezo, nao wanalazimika kuishi katika aina mpya ya maisha ambayo bila shaka ni kero, maumivu na manung’uniko ya kutofurahia hali.

Michezo yote ilisimamishwa, si Tanzania pekee au Afrika pekee badala yake ni dunia nzima. Kawaida ya wanamichezo wanaishi dunia nzima, ndiyo maana mara zote utasikia mtu anauliza hivi, hapa nyumbani unashabikia timu gani, nje pia timu gani?

Maisha ya wapenda michezo au soka, ni hapa nyumbani na nje. Hivyo kufungwa kwa michezo hapa nyumbani lakini hata huko nje kwao inakuwa ni kama jela hivi. Hakuna kinachoendelea kawaida kwa maana ya viwanja vya hapa nyumbani lakini hata viwanja vya nje ambako wangeweza kuangalia kupitia runinga.

Wengi wamelipa ving’amuzi mbalimbali lengo likiwa ni kuangalia mpira, wanaweza kuona hiyo ni sehemu ya hasara lakini hakuna namna kama nilivyosema kuwa lazima kuishi kulingana na mazingira ya sasa.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, John Pombe Magufuli yeye amekuwa jasiri, pamoja na kuwa na hali hii ya hofu ameendelea kuwatia moyo wananchi wake au anaowaongoza namna ambavyo inaweza kuendelea na mapambano yanavyoweza kwisha kwa ushindi.

Serikali yake imeonyesha nia ya kurejesha michezo kwa kuanza na soka na baadaye tumeona wizara husika ikieleza kwamba hilo limefanikiwa na tayari linafanyiwa kazi kuhakikisha mambo yanafanyika kwa tahadhari kubwa.

Rais Magufuli amemaliza kazi kwa kuwa amefanya kitu kikubwa kwa wanamichezo akianza na soka. Kinachotakiwa sasa ni kuhakikisha zawadi hii aliyoitoa haitumiki vibaya na wahusika kwa maana ya wadau, watende haki kuonyesha kwamba walikuwa wanastahili kupewa nafasi hii ambayo nchi nyingine nyingi bado hawajaipata.

Tumeona ligi chache kama Bundesliga ya Ujerumani ambayo imeanza sambamba na ligi ya Korea Kusini. Tayari Premier League ya England tumeelezwa itarejea Juni lakini kuna La Liga ya Hispania na Serie A ya Italia ambako nao wameamua kurejea.

Kwa Afrika, Tanzania inaonekana kuwa ya kwanza kabisa kuruhusu michezo kurejea, jambo ambalo wahusika wanapaswa kulitumia vizuri kuunga mkono uamuzi huo wa Rais Magufuli.

Kutumia vizuri hapa nawagusa wachezaji wenyewe, makocha, waamuzi na hata viongozi wa klabu na mashirikisho. Kuwa wafuate masharti ya wataalamu wanaeleza nini ili kuhakikisha wanamaliza ligi hiyo au nyingine zitakazoendeshwa wakiwa salama.

Nasisitiza usalama kwa kuwa inawezekana. Mfano mchezaji amepimwa na kuonekana yuko salama, hivyo anapitishwa kuwa sasa yuko tayari kushiriki katika mechi za ligi akiwa na wenzake dhidi ya timu nyingine, basi ni lazima awe mweledi kwa vitendo.

Mchezaji huyo kama amejua ameshapimwa na usalama wake ni usalama wa wenzake atakaokutana nao dhidi yake au wale wenzake wa timu moja anaofanya nao mazoezi, basi lazima ajilinde.

Ninaamini kwa wale watakaokuwa wamefanyiwa vipimo na kukaa sehemu sahihi, basi ni jambo jema kabisa kuwa makini badala ya kusikia au kumuona mchezaji aliye katika timu inayoshiriki ligi akiwa katika makundi ya watu wengine ambao hawajapimwa.

Ninaamini katika kipindi hicho wakati ligi zinachezwa hakutakuwa na uhuru mkubwa wa kutosha  kwa wachezaji wengi.

 Badala yake kutakuwa na masharti mengi hasa kutoka kwa wataalamu wa afya, lengo likiwa ni kumaliza ligi kukiwa na usalama au salama. Sasa kwa wachezaji, makocha, viongozi na wengine ni lazima wawe wavumilivu ili waweze kumaliza kipindi hicho cha mechi 10.

Kama watashindwa kufuata masharti, halafu wakasababisha maambukizi, maana yake watafanya ionekane Serikali ilikuwa na haraka na ilipaswa kusubiri. Au Serikali iliamua kuwapa dhamana watu wasiojielewa au wasiojua thamani ya walichopewa, hili litakuwa jambo baya sana.

Bado ninaamini watu walio ndani ya michezo watakuwa wameelewa alichokifanya Rais Magufuli kuwa si jambo dogo la kijasiri, hivyo si vizuri kumuangusha.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic