February 21, 2013





Wakongwe wa Italia, usiku wa kuamkia leo wameonyesha ukubwa ni dawa baada ya kuitandika Barcelona ya Hispania kwa mabao 2-0 katika mechi ya kwanza ya hatua ya 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Katika mechi hiyo iliyokuwa ya kuvutia, pamoja na kasi ya Barcelona lakini wenyeji AC Milan walionekana kucheza kwa kujiamini zaidi na kupanga mashambulizi taratibu na kwa uhakika.


Hadi timu hizo zinakwenda mapumziko, hakuna timu iliyokuwa imepata bao ingawa kulikuwa na kosakosa kutoka kila upande.
Ingawa Barcelona inaongoza La Liga kwa tofauti ya pointi 12 na AC Milan iko nafasi ya tatu katika Serie A, mambo yalionekana kuwa tofauti hata walivyochambua wapembuzi wa mambo ya soka kuhusiana na mchezo huo.

Mabao yote mawili ya AC Milan yalifungwa na Waafrika raia wa Ghana, Prince Boateng na Sulley Muntari, tena wote wakitikisa nyavu katika kipindi cha pili.
Kabla ya mabao hayo katika dakika za 57 na 81, Muntari nusura aipatie bao Milan baada ya shuti lake kali kugonga mwamba. 
Philippe Mexes naye alifanya kazi ya ziada kuokoa krosi ya Alba isimfikie Pedro ambaye alikuwa katika nafasi nzuri ya kufunga.
Kinda Stephane El Shaarawy nusura aipatie bao Milan lakini kushindwa kuupiga mpira vizuri akapoteza nafasi na kipa wa Milan, Christian Abbiati akachupa kiufundi kuokoa shuti kali la Xavi kutoka umbali wa mita 30.
Pamoja na kuonyesha juhudi kubwa, lakini juhudi za mchezaji bora duniani, Lionel Messi hazikufua dafu mbele ya ngome kongwe ya AC Milan.

Ushindi huo unaifanya AC Milan iende katika mechi ya marudiano Camp Nou ikiwa mbele kwa mabao mawili huku wenyeji wake Barca wakiwa na kazi ya kushinda mabao matatu au zaidi huku wakilinda zaidi nyavu zao zisiguswe.
Kivutio kingine uwanjani hapo ni mshambuliaji mpya wa AC Milan, Mario Balloteli alipojitokeza uwanjani hapo na mpenzi wake mpya, Fanny Robert Neguesha ambaye ni mwanamitindo.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic