Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) limesema linapeleka rasmi madai
ya mchezaji wa zamani wa Yanga, Kenneth Asamoah kwenye chombo chake cha utatuzi
wa migogoro (Dispute Resolution Chamber) baada ya klabu hiyo kutojibu chochote.
Fifa ilipokea malalamiko ya Asamoah kuwa anaidai Yanga dola 5,000 za
Marekani ambapo ilikuwa ni sehemu ya malipo yake (signing fee) baada ya kujiunga
na klabu hiyo.
Desemba mwaka jana FIFA iliiandikia barua Yanga kupitia (TFF) ikitaka
maelezo yake kuhusu madai hayo ya Asamoah, lakini hadi sasa haijajibu madai
hayo.
Kwa mujibu wa FIFA, hatua ya uchunguzi wa suala hilo umekamilika, na
sasa linapelekwa rasmi katika chombo chake cha utatuzi wa migogoro (Dispute
Resolution Chamber) kwa ajili ya kufanya uamuzi.
Hii si mara ya kwanza kwa Yanga kesi zake kufikishwa Fifa, miezi
miwili iliyopita shirikisho hilo liliagiza Yanga kumlipa mchezaji na kocha wake
wa zamani.
Mchezaji aliyelipwa ni beki wake wa zamani wa kushoto, John Njoroge
raia wa Kenya wakati Kocha, Kosta Papic kutoka Serbia naye alitakiwa apate
chake kutoka Yanga.
Mara kadhaa imekuwa ni tabia za klabu za Tanzania kujisahau na
kushindwa kuwalipa wachezaji ambao imesitisha nao mkataba.
Asamoah ambaye alikuja awali na kuondoka, wakati anarejea Yanga
ilikuwa chini Lloyd Nchunga na alipokelewa kwa mbwembwe na uongozi na mashabiki
wa timu hiyo maarufu nchini, lakini kuondoka kwake kulikuwa na matatizo kibao.
0 COMMENTS:
Post a Comment