February 26, 2013




 FEDHA ZA OKWI SI KAWAIDA, KUNA KITU KINAFICHWA
KUNA shabiki mmoja wa Simba wakati anatoa maoni yake, aliwahi kuniuliza hivi: “Mara kadhaa unauliza kuhusiana na fedha za Okwi, kwani ni zako, hazikuhusu, tuachie Simba yetu.”
Wakati naanza kuisoma nilikuwa napigana na uchovu wa siku nzima, lakini baada ya hapo ilinichangamsha sana kwa kuwa nilianza kufikiria upya namna watu wanavyofikiria. Yule shabiki anaamini Simba ni yake, lakini hana uwezo hata kidogo wa kufikiria kuhusiana na klabu yake.

Kizuri kwa shabiki kama huyo na wenzake ambao wana fikra kama zake ni kuona Simba inashinda, basi. Kuhusiana na maendeleo ya klabu, kwenda kisasa na kufanya mambo kiteknolojia, hawajali. Inawezekana kabisa, watu kama shabiki huyo wanahitaji kubadilika, mimi Simba si yangu, ila nahoji kwa ajili ya faida ya Simba na jamii ya wadau wa soka na michezo kwa ujumla.

Metodo nyingine, pia bado inaendelea kuhoji kuhusiana na  fedha hizo za Okwi ambazo zilitangazwa kwamba ni dola 300,000 (zaidi ya Sh milioni 480) ambazo klabu ya Etoile du Sahel imekubali kuzitoa kumnunua kiungo huyo raia wa Uganda.

Okwi alikuwa ni tegemeo la Simba katika kuanzisha mashambulizi, ameuzwa kwa fedha nyingi ambazo unaweza kusema Simba walikuwa na kila sababu ya kushawishika na kumuachia aende na kuchukua fedha hizo.
Lakini hofu kubwa ambayo nimekuwa nayo ni mchezo wa kizamani sana ambao unachezwa, inawezekana wengine mkawa mmesahau au si wenyeji wa kitambo wa soka Bongo, nitawakumbusha kidogo.

Timu zilikuwa zikiuza wachezaji, mara nyingi wanachama walikuwa wanatangaziwa fedha zao zitalipwa kwa mafungu. Mtindo huo haukuanza leo, ingawa mifano ya hivi karibuni inajulikana, mfano Haruna Moshi alipouzwa Sweden na Henry Joseph alipouzwa Norway.
Lakini hakuna shabiki au mwanachama anayejua kama fedha hizo zilikuja zote au la, hakuna taarifa ambayo ilitolewa baada ya hapo, kwa kifupi viongozi wanajua mashabiki na wanachama ni wasahaulifu ndiyo maana wanatumia mbinu hiyo.

Kusema fedha za Okwi zitakuja kwa mafungu huku viongozi wa Simba wakionekana kujikanyaga katika hilo, kidogo kunanishtua na ninapata hisia ule mtindo wa kitambo utaendelea na mwisho hapa itatokea ishu nyingine na fedha hizo zitakuwa zimepita.

Katika ya vitu vinavyoshangaza zaidi katika biashara hiyo ya Okwi, eti Simba wamemuuza, Watunisia hao wako tayari kutoa dola 300,000 na Okwi wamempa dola 100,000 (Sh milioni 160), lakini katika malipo ya klabu hawajaanza kulipa hata senti.

Ninavyojua kama ni malipo ya mafungu (installment), basi baada ya kukubaliana, Etoile du Sahel walitakiwa kulipa fungu la kwanza. Mfano ingekuwa dola 100,000 na baada ya hapo wangeendelea kulipa hatua kwa hatua, labda dola 100,000 au 50,000 hadi watakapomaliza.
Lakini kusema Simba hawakupokea kitu kabisa baada ya biashara hiyo ni kuudanganya umma. Hakika haiwezi kuwa lahisi, hauwezi kuiita biashara ya kwenda kuuza bidhaa unaondoka bila kupata malipo ya awali.

Kama itakuwa Simba walifanya hivyo itakuwa ni makosa makubwa, lakini bado ninahisi kutakuwa na namna, huo ni wasiwasi wangu nilionao kuhusiana na hilo na kama kutakuwa na kiongozi wa Simba ambaye anapinga hilo, vizuri akajitokeza wakalizunghumzia hilo.

Fedha za Simba ni za umma, hata kama hautakuwa umma wote basi ni Wanasimba na wana haki ya kujua. Waelezwe ili kuondoa hali hii ya wasiwasi kwa kuwa fedha walizopata ni nyingi sana na zinaweza kuisukuma Simba mbele kimaendeleo badala ya kuendelea kuwa ombaomba kama ilivyo sasa.

Simba ina madeni lukuki, wachezaji hawajalipwa hata fedha zao za usajili, makocha na wachezaji bado wanadai, lakini hata kocha aliyeondoka walishindwa kumlipa hadi wakapata msaada. Sasa vipi leo kuna fedha nyingi kama hiyo hakuna ufafanuzi na wanachama wako kimya.

Najua wako wanaochukizwa na kuhoji kwangu, lakini nitaendelea kufanya hivi kwa kuwa lazima tujue kuhusiana na hilo kwa vile mauzo ya Okwi yalikuwa hadharani na kila kitu kilionekana, basi ni vizuri sana uwazi ukaendelea kuchukua nafasi.







0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic