March 11, 2013




Ningeweza kusema sina kabisa cha kuzungumza, lakini naamini nitaendelea kwa manufaa ya michezo ya Tanzania na hasa mchezo wa soka, nasisitiza, mwisho majibu yatapatikana tu.

Nimeanza na kusisitiza kwa kuwa kila kitu kimeanza kuonekana, kwanza nawapongeza Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Pope ambaye aliamua kubwaga manyanga baada ya kuona kweli mambo hayaendi vizuri ndani ya Simba.

Geofre Nyange ‘Kaburu’ pia aliachia nafasi yake ya makamu mwenyekiti wa Simba, kitu ambacho ni cha kumpongeza pia, kwa kuwa hata kama mwanzo alikuwa mgumu, mwisho ameona ukweli, ndiyo maana nikasisitiza wasiouona, sitachoka kuwaambia hata kama inawaudhi.

Simba imeyumba, haifanyi vizuri na matatizo yake hata si mambo yaliyojificha chini ya mwembe, kila kitu kikaonekana kwamba uongozi ni sehemu kubwa ya kusababisha Simba kufeli kuanzia katika michuano ya ndani hadi ile ya ligi.


Hii si mara ya kwanza Ismail Aden Rage kuwa kiongozi wa Simba, anajua alishawahi kuondoka baadaye akarejea. Katika masuala ya uongozi pia hilo ni jambo linaweza kutokea na yanatokea kila kukicha.

Lakini ni vizuri zaidi kuwa na viongozi wanaojitambua, wenye mapenzi ya dhati na wanachokiongoza. Mfano, kujiuzulu ni kujitambua lakini utakuwa umeonyesha unakipenda kile unachokiongoza kwa kuwa kuwepo kwako ni sehemu ya kufeli kwake, sasa kwa nini kiendelee kufeli na wewe umeng’ang’ania tu pale.

Kuendelea kung’ang’ania ni dalili tosha ya kuonyesha wewe hauna mapenzi na unachotaka ni manufaa yako binafsi, sasa huu ni wakati mwafaka wa kumkumbusha Rage bila ya woga, kwamba yeye ni Simba damu,sawa. Lakini ameshindwa kazi, afuate uzalendo wa Hans Pope na Kaburu.

Angalia matatizo yaliyotokea jana kwa Simba kuzuiliwa katika hoteli ya Sapphire kutokana na deni la Sh milioni 27, lakini pia wachezaji wake Waganda, Abel Dhaira, Mussa Mudde na Meneja, Moses Basena kutimuliwa katika hoteli ya Spice ya Kariakoo.
Aibu gani hiyo, imefikia Simba inashindwa hata kupasha viungo uwnjani wakati inacheza na Coastal Union, haikuwa sahihi. Ila mwenye hoteli pia hakuwa na ujanja zaidi ya kuanzisha shinikizo hilo ili alipwe.

Rage anastahili kuondoka Simba wakati huu, wakati ambao timu hiyo imeshindwa kila kitu. Mambo yanakwenda mlama na inaonekana hakuna pa kushika, badala yake maisha ya klabu hiyo kwa sasa ni sawa na mfamaji, inatapatapa tu.

Simba inaonekana hata uongozi umeshindwa kuongoza mambo vizuri, imefikia hadi wazee wameamua kuunda kamati mpya ya ushindi ambayo inaongozwa na Malkia wa Nyuki. Wasipoangalia inaweza ikafeli pia kwa kuwa bado kuna matatizo mengi juu.
Kuundwa kwa kamati hiyo, inaonyesha mambo si mazuri. Kama kila kitu kingekuwa kinakwenda sawa, basi wakati huu haukuwa wa kuunda kamati.

Ukiachana na hivyo, awali nilieleza kwamba uongozi ni sehemu ya matatizo, hali halisi inaonyesha hivyo kwa kuwa angalia Rage alivyokuwa tatizo kwa kuahidi mambo milioni lakini akashindwa kutekeleza hata moja.

Unajua namna ahadi inavyopandisha morali, lakini isipotekelezwa hugeuka na kuwa sumu. Rage amepandika sumu za ahadi bila ya mwenyewe kujua, lakini uongozi wake umekosea mambo mengi sana ya kiutendaji ukiwa madarakani.

Kila mmoja ameona walivyofeli, mfano kusema kocha hafai, halafu wakaleta mwingine na mambo yakazidi kuwa mabaya zaidi. Sisemi kocha ni mbaya, lakini kocha hawezi akafanya mambo mazuri bila ya kuwa katika mazingira mazuri.

Simba inatawaliwa na madeni lukuki, kila siku inakutana na fedheha kama ile ya basi lake kuzuiliwa Arusha hadi Malkia wa Nyuki alipoamua kuokoa jahazi na kulipa Sh milioni 11` kati ya Sh milioni 15 walizokuwa wanadai.

Achana na hiyo, uongozi unasisitiza wachezaji wako katika morali nzuri, lakini wengi wanadai fedha zao za usajili. Vipi watacheza mpira kwa kujituma, kibaya zaidi hata mshahara wao wanadai pia, hii hali utasema ni kosa la nani?

Achana na hivyo, wachezaji wamekuwa hawaelewani, ndani yake kuna makundi ambayo yamesababisha mpasuko mkubwa. Lakini uongozi kwa kuwa haushughuliki na masuala ya klabu kwa karibu zaidi na hasa Rage ambaye ndiye bosi mkubwa, umeshindwa kulitatua tatizo hilo hadi leo.

Mimi ninaamini Rage ni muungwana sana, itafika siku atakubali ninachomueleza kwa kuwa nia ni kusaidia kwenye tatizo, ataondoka kwa moyo safi ili kuisaidia Simba. Akiendelea kung’ang’ania, basi iko siku ataondoka kwa aibu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic