April 26, 2013


Na Saleh Ally
UNAPOMUULIZA Kocha Mkuu wa Yanga, Ernie Brandts kama Yanga ina uhakika wa kutwaa ubingwa katika mechi yake ya Jumatano ijayo dhidi ya Coastal Union, jibu lake ni “lazima”.

Brandts raia wa Uholanzi anaamini kikosi chake ndiyo imara zaidi kuliko kingine chochote kinachoshiriki Ligi Kuu Bara msimu huu, hivyo kuwazuia kutwaa ubingwa katika mechi mbili walizobakiza itakuwa miujiza.


“Nina uhakika, tutashinda na kutwaa ubingwa. Hakuna anayetaka sare hata kama tuna nafasi. Hata baada ya kuwa mabingwa tunataka kuendelea kushinda mechi zilizobaki ikiwemo ya Simba.

“Najua, Simba na Yanga ni sawa na Madrid na Barcelona. Kila upande hutaka kushinda, hivyo tutafurahi kuchukua ubingwa na kuwafunga wapinzani wetu wakubwa,” anasema.

Vita ya kuhakikisha Yanga inafikia ilipo si rahisi, Championi Ijumaa lilishuhudia makaratasi lukuki katika moja ya meza nyumbani kwa Brandts ambayo yamejaa mahesabu na michoro ‘ya ajabu’ sawa na ile ya wahasi.

Mazingira ya eneo analoishi Mholanzi huyo yanavutia kwa mpangilio lakini usafi wake unaonyesha ni ule unaofanywa kwa kufuata utaratibu.




“Kweli haya makaratasi ni mpangilio wa mazoezi kwa mwezi mzima, lakini ni namna ninavyoweza kufanya kazi zangu za kila siku.

“Kwanza ninapanga ratiba ya mwezi mzima na nini cha kufanya, baada ya hapo kila baada ya mazoezi ya siku moja huandika kilichotokea na tathmini nifanye nini siku inayofuata. Baada ya hapo narudi kwenye ratiba ya mwezi na kubadilisha mambo kadhaa.

“Haya ni mambo ya kujifunza kila siku, ninasoma kila siku bila ya kujali uzoefu wangu. Wakati mwingine nafanya hivyo hadi saa nane usiku, halafu ninaamka saa 11 alfajiri kujiandaa kwa ajili ya kwenda mazoezini,” anasema Brandts.

Alipoulizwa kwamba, pamoja na kusoma na kubadili mambo kwa mahesabu na maandishi lakini huangalia mikanda ya video ya timu pinzani?


“Hata siku moja, kazi yangu iko kwenye haya makaratasi. Naamini nina kikosi bora zaidi katika Ligi Kuu Bara. Hivyo wao ndiyo wanaopaswa kutuangalia sisi na si sisi kuwaangalia wao, sijafanya hivyo hata kidogo labda katika michuano mingine.”

Kama anabanwa na mazoezi, usafi na mambo mengine ya timu, anaweza vipi kudhibiti mambo yote na yote yakaenda kwa mpangilio mzuri?

“Ninaweza ingawa si kazi rahisi, kazi ya ukocha ni ngumu na unalazimika kuipenda ingawa suala la kujitolea inabidi ulipe nafasi. Lazima ukubali kufanya kazi zaidi ya kiwango chako wakati mwingine.

“Kuhusu usafi wa hapa nyumbani, kuna mtu anahusika na kufanya hivyo. Lakini mimi napenda kujifanyia usafi mwenyewe, nafua nguo zangu na kuosha vyombo. Ingawa (mfanyausafi) amekuwa akisisitiza niache, lakini sioni shida kufanya hivyo.

“Kwa binadamu unapokuwa una utamaduni wa kujali kitu chako, mfano mazingira unayoishi. Basi inakuwa ni rahisi kujali kazi yako na unaofanya nao kazi. Ninaamini kocha au mchezaji kama ilivyo kwa binadamu wengine anapaswa kuishi sehemu nzuri na mazingira mazuri ambayo yanapaswa yawe chini ya usimamizi wake.”

“Nilielezwa wanaume kuosha vyombo, hasa katika umri wangu inaonekana si sahihi kwa utamaduni wa Kiafrika, lakini ninaamini wako watakaoungana nami kwamba kujituma kwenye vitu vya nyumbani vinakusaidia kujituma katika kazi pia,” anasema Brandts.

Iwapo Yanga itatwaa ubingwa katika mechi hiyo dhidi ya Coastal Union ambayo inahitaji sare, maana yake kocha huyo atakuwa ameweka rekodi ya kuchukua mataji matatu ya ligi katika nchi mbili za Afrika.

Misimu miwili iliyopita alibeba ubingwa wa Rwanda akiwa kocha mkuu wa APR, hivyo kombe la Yanga litakuwa la tatu.
Pamoja na kutwaa ubingwa wa Rwanda, kwa misimu hiyo miwili, Brandts alifanikiwa kutwaa makombe manane, yaani michuano yote APR iliyoshiriki.

Hadi sasa Yanga ina pointi 56 kileleni na zinaweza kufikiwa na Azam FC pekee iliyo katika nafasi ya pili ikiwa na pointi 47 na mechi tatu mkononi.

Pointi moja inahitajika kwa Yanga, maana yake kama itatoka sare na Coastal Union inayoendelea kuwania nafasi ya tatu, basi itatawazwa kuwa mabingwa wapya wa msimu huu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic