April 19, 2013





Na Saleh Ally
SIMBA imefundishwa na makocha wawili katika msimu wa 2012-13, wote kutoka barani Ulaya, mmoja akiwa anatokea Serbia na mwingine Ufaransa.

Milovan Cirkovic raia wa Serbia ambaye aliipa ubingwa msimu uliopita, alitimuliwa mwishoni mwa mzunguko wa kwanza kwa madai alishindwa kufanya vizuri katika mechi zake 13 na kusababisha timu hiyo imalize mzunguko huo ikiwa katika nafasi ya tatu.

Akaletwa Mfaransa Patrick Liewig, ambaye aliwahi kufanya kazi ukanda wa Afrika Magharibi, lengo likiwa kuiokoa Simba kutoka katika mwenendo ambao viongozi wa Simba waliuita ni mbaya.


Tokea Liewig ametua nchini, Simba imeshacheza mechi tisa za Ligi Kuu Bara na hadi sasa iko katika nafasi ya nne, chini ya vinara Yanga, wakifuatiwa na Azam FC na Kagera Sugar.

Kwa hesabu, inaonyesha Simba hawajalimaliza tatizo ambalo walilianzisha mzunguko wa kwanza na mwisho kuamua kuchukua uamuzi wa kumuondoa Milovan huku wakisema kocha ni tatizo.

Kuna mambo makubwa mawili yanajionyesha, kwamba huenda Milovan hakuwa tatizo na badala yake ni uongozi, kama si hivyo, basi kocha wa sasa Patrick Liewig ndiye atakuwa tatizo kwa kuwa ameshindwa kuleta mabadiliko.

Milovan:
Mserbia huyo, katika mechi zake 13, Simba ilishinda 6, ikatoa sare 5 na kupoteza mbili. Kikosi chake kikafunga mabao 20, kikafungwa 11 na kumaliza katika nafasi ya tatu kikiwa na pointi 23. Tofauti kati yake na Yanga (ilikuwa sita) na Azam FC (pointi moja).


Liewig:
Katika mechi tisa, tayari kikosi chake kimeshinda 3, kimetoka sare 4 na kupoteza mbili. Wafungaji wake wamefunga mabao 11, wamefungwa 9, hivyo katika mechi zote tisa hizo Simba imeingiza pointi 13 tu.

Tofauti ya pointi ya Simba na vinara Yanga na Azam FC ni kubwa sana ukilinganisha na wakati wa Milovan. Sasa Simba inazidiwa pointi 17 na Yanga, Azam wanaizidi pointi 11.

Mjadala:
Pamoja na mabadiliko ya uongozi kwa Simba, kinachoonekana hapa hakuna chochote kilicholeta mabadiliko na badala yake mwenendo wa kikosi cha Liewig kitakwimu ndiyo unaonekana kuyumba zaidi.

Simba imebakiza mechi nne tu kumaliza ligi, ukiacha Yanga, zote ni dhidi ya timu za wanajeshi kuanzia Ruvu Shooting, Polisi Moro na Mgambo Shooting, hakuna ubishi zitakuwa ngumu sana kwao.

Ili kufikia angalau rekodi aliyofukuzwa nayo Milovan kwa madai ni mbovu, Liewig analazimika kushinda mechi zote nne zilizobaki, kwani ndiyo atakuwa amemzidi Milovan kwa kushinda saba wakati yeye alishinda sita. Je, itawezekana?

Idadi ya mabao ya kufunga, kwa maana ya kuwa na fowadi kali. Katika mechi 13, Milovan alifunga mabao 20, Liewig ana 11 katika mechi tisa. Ikiwa na maana, katika nne alizobakiza anatakiwa kufunga angalau mabao 10 ili kumvuka Mserbia na kuonyesha ilikuwa sahihi kumtimua.

Safu ya ulinzi ya Milovan, ilifungwa mabao 11 katika mechi 13, lakini ya Liewig ndani ya mechi tisa imeruhusu nyavu kitikiswa mara tisa. Bado mabao matatu tu kumfikia Mserbia ambayo uongozi wa Simba chini ya Ismail Aden Rage ulisema ni mbaya.

Swali, katika mechi nne, safu yake ya ulinzi inaweza kuzuia mabao manne yasiguse nyavu?

Sare za Milovan zilikuwa tano, tayari Simba ina sare nne. Maana yake kufikia tano inawezekana kabisa. Kitakwimu, bado inaonekana hakuna tofauti au sababu ya msingi kwa Simba kufanya mabadiliko.

Inawezekana kabisa Milovan hakuwa na matatizo na ugumu au matatizo yalianzia kwa uongozi kwa kuwa hata Liewig anaelekea kufeli na huenda akaanguka zaidi ya Milovan kama hakutakuwa na mikakati madhubuti katika mechi nne zilizobaki.
                                       MSIMAMO WA MILOVAN: 
                               P        W                D            L        F       A      GD      Pts 
    1. Yanga            13       9                 2             2       25      10      15        29
    2. Azam           13          7                3             3       17        11      6        24   
    3. Simba         13          6                 5            2       20         11      9      23
    4. Mtibwa      13          6                4             3       17       12       5         22
    5. Coastal       13      6                   4             3       16       13       3        22   

                                     MSIMAMO WA LIEWIG:
 P      W     D       L        F       A      GD    PTS 
1. Yanga    23     16     5       2       41     13     28     53    
2. Azam     23     14     5       4       41     19     22     47    
3. Kagera   23     11     7       5       24     17     7       40    
4. Simba    22     9       9       4       32     21     11     36    
5. Mtibwa  24     9       9       6       27     23     4       36

SOURCE: CHAMPIONI NEWSPAPER

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic