April 12, 2013




Na Saleh Ally
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limetangaza kumtaka mshambuliaji wa Coastal Union, Nsa Job kuwasilisha ushahidi mara moja kuhusiana na mtu aliyemtaja kwamba alimhonga ili asifunge.

Aprili 3, mwaka huu, Nsa alikaririwa na kituo kimoja cha redio akisema aliwahi kuhongwa na kiongozi mmoja wa klabu kigogo cha soka nchini ili asiifunge timu yake watakapocheza dhidi yake, akampa fungu la fedha, naye akapokea halafu bado siku ya mchezo akapachika bao.

Awali ilikuwa ikiaminika kwamba Nsa alipokea fedha hizo wakati akiwa anaichezea Coastal Union, lakini kwa takwimu kama ni msimu huu, Nsa hajaifunga timu yoyote ambayo ni kigogo.

Kigogo, maana yake kongwe au kubwa kifedha na umaarufu. Katika Ligi Kuu Bara, zinazoingia kwenye kundi hilo ni timu nne tu, Yanga, Simba, Azam FC na Mtibwa Sugar.


Nsa alicheza mzunguko wa kwanza tu, akaumia mechi ya mwisho dhidi ya Ruvu JKT na ameukosa mzunguko wote wa pili. Katika mechi za mzunguko wa kwanza dhidi ya Simba, ilikuwa sare ya bila kufungana, walipocheza na Azam, timu yao ikalala kwa mabao 4-1, bao lao la kufutia machozi likafungwa na kiungo Jerry Santo.

Dhidi ya Yanga, vijana hao wa Tanga walifungwa mabao 2-0, yaliyofungwa na Didier Kavumbagu na Hamis Kiiza. Walipowavaa Mtibwa, Coastal walishinda mabao 3-0 yakiwa yamefungwa na Juma Jabu, Gerald Lukindo na Daniel Lyanga.

Kwa takwimu hizo, maana yake msimu huu, Nsa hakuwa ameifunga timu yoyote kigogo, maana yake tunalazimika kurudi na kuangalia msimu uliopita aliokuwa akiichezea Villa Squad.

Msimu uliopita, takwimu zinaonyesha Nsa alimaliza akiwa na mabao 12 akiwa nafasi ya pili ya upachikaji mabao akiwa na Villa Squad ambayo iliteremka daraja.

Hesabu zinaonyesha katika mabao yake 12 ya msimu uliopita, timu kigogo aliyoifunga katika mizunguko yote miwili akiwa na Villa Squad ni Simba katika mechi iliyopigwa Februari 4, 2012, bao lake pekee ndiyo liliiangusha Simba siku hiyo kwa ushindi wa 1-0.

Lakini Machi 17, 2012, Mtibwa Sugar iliichapa Villa kwa mabao 2-1 na hilo la kufutia ‘machozi’ likapachikwa kimiani na Nsa.

Maana yake Nsa hajaifunga Azam FC wala Yanga msimu huu na uliopita, lakini uliopita ameifunga Mtibwa na Simba na ndiko anakoelekeza lawama zake kama ni kati ya misimu hii miwili.

Kama itakuwa hivyo, maana yake timu mbili ndiyo zinaingia katika tuhuma hizo za Nsa ambazo tayari TFF imemtaka azifafanue kwao kwa kuwaeleza ni kiongozi yupi aliyefanya hivyo la sivyo adhabu itamkuta mchezaji huyo.

Rushwa limekuwa tatizo kubwa sana katika soka nchini, ingawa ni kitu kigumu kugundulika kutokana na kufanyika kwa siri sana. Lakini Nsa ameamua kuweka hadharani, huenda ni wakati mzuri kwa TFF kutoa mfano iwe kwa kiongozi fulani au mtu mwingine.

Mechi za vigogo (Yanga, Simba, Azam, Mtibwa Sugar) msimu wa 2011-12 alizocheza Nsa akiwa na Villa:

MZUNGUKO WA KWANZA:
Septemba 7, 2011
 Simba 1-0 Villa
Gervais Kago 7

Septemba 13, 2011
 Villa 0–2 Azam              
                     Tchetche 1
                      Bocco 35

Septemba 17, 2011
Villa 0-2 Mtibwa
                       Thomas Morris 13
                        Said Rashid     47

Septemba 21, 2011
Yanga 3-2 Villa
Niyonzima 19     Kijuso         11
Asamoah   27     Kigi Luseke   72
Kiiza         63

MZUNGUKO WA PILI:

Februari 4, 2012 
Villa 1-0 Simba
Nsa Job 40

Februari 15, 2012
Azam          4-1   Villa
Salum Abubakar       Nsa Job 22
Abdi Kassim 28
Hamis Mcha 43
Kipre Tchetche 45

Februari 19, 2012
Mtibwa               2-1              Villa
Vincent Barnabas 19   Nsa Job 32
Said Bahanuzi

Machi 17, 2012
 Villa 0-1 Yanga
                 Kiiza 90

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic