Baada ya kutwaa ubingwa ikiwa imepumzika, Yanga imeamua kuwapumzisha
wachezaji wake kadhaa watakaokuwa na kadi mbili za njano.
Bado haijaelezwa ni wachezajiu gani, lakini Kocha Mkuu wa Yanga, Ernie
Brandts amethibitisha kwamba kuna baadhi ya wachezaji watapumzishwa.
Taarifa za awali zilizoifikia Salehjembe zilisema uamuzi huo umetokana
na kuhofia wachezaji hao kupata kadi nyingine ya njano na kuikosa mechi ya
Simba.
Akizungumzia suala hilo, Brandts alisema watafanya hivyo ili kuhakikisha
katika mechi na Simba wanacheza na kikosi wanachokitaka.
“Kweli tumeliangalia hilo, mchezaji mwenye kadi mbili za njano hatacheza
mechi dhidi ya Coastal ili kuhakikisha tuna kikosi tunachotaka katika mechi na
Simba.
“Lakini itakuwa nafasi nzuri kwa wachezaji ambao hawakupata nafasi, mara
nyingi mechi ya Simba inakuwa na wasiwasi, hivyo watacheza mechi ya Coastal.
“Pia itakuwa ni nafasi nzuri kwao kuonyesha kama watabaki katika msimu
ujao au vipi,” alisema Brandts.
Baada ya sare ya bao 1-1 kati ya Coastal Union na Azam mjini Tanga,
maana yake Yanga tayari ni mabingwa wa Tanzania Bara.
Watakutana na Simba waliokuwa wanaushikilia ubingwa huo Mei 18 kwenye
Uwanja wa Taifa, Dar.
Pamoja na kutwaa ubingwa, Yanga inataka kuishinda Simba ili isherekee
ubingwa kwa raha zake. Lakini Simba inataka kushinda mechi hiyo kuwapoza
mashabiki wake lakini kuepuka aibu ya kushika nafasi ya nne kwa kubeba pointi
zote tatu siku hiyo.







0 COMMENTS:
Post a Comment