May 24, 2013



 
Dewji, Zitto na Dau
Na Saleh Ally
KUTOKANA na mwendo mzuri wa timu ya taifa ya soka, Taifa Stars, Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo imeunda kamati ya Saidia Taifa Stars ishinde.

Kamati hiyo itaongozwa na Mwenyekiti, Mohammed Dewji ambaye ni Mbunge wa CCM (singida Mjini). Hakuna asiyejua uzoefu wa Mo katika masuala ya mchezo wa soka.

Kamati hiyo ina watu wengi tu ambao wanaweza kupambana kwa ajili ya Taifa Stars kama Mkurugenzi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Ramadhani Dau. Mbunge wa Kigoma Mjini (Chadema) Zitto Kabwe, mdau Teddy Mapunda na Dioniz Malinzi.
 
Teddy Mapunda
Niseme ninaiamini kamati hiyo kwamba inaweza ikafanya vizuri na kupambana kusaidia joto la ushindi katika mechi ngumu za Stars kama hiyo dhidi ya Morocco, ugenini na pia Ivory Coast hapa nyumbani.

Naiamini kamati kwa maana naona ina watu wapambani, sitaki kuingia kwenye kuhoji kwamba wako ‘wanajeshi’ wengine wameachwa nje. Najua huu si wakati wake, lakini kuna mambo nataka nikumbushe kuigusa kamati hiyo ya Mo Dewji.
 
Dk Dau
Kama nilivyoeleza awali kwamba kamati ninaiamini, lakini kuna mambo kadhaa ya kufanya ambayo yataisaidia kamati hiyo kufikia malengo yake, la sivyo itakuwa sehemu ya kuporomosha mambo kabisa na kuivuruga morali ya Taifa Stars.

Lakini tukubali kuwa Stars hadi inafikia hapo kulikuwa hakuna kamati, kwamba iliweza kufanya vizuri ikiwa chini ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), ndilo lilikuwa linapigana jino kwa jino kuhakikisha timu hiyo inafanya vizuri. Pia msiwasahau wadhamini wao Bia ya Kilimanjaro.

Katika kamati hiyo hakuna mtu wa TFF, inawezekana ikawa si lazima. Lakini kuna tatizo nimeliona mapema, kwamba sijasikia mtu wa kamati katika mahojiano akizungumzia kuhusiana na kazi nzuri iliyofanywa na shirikisho hilo.


Kamati isingeundwa kama Stars ingekuwa katika nafasi ya ‘mashaka’, hivyo lazima TFF ipewe shukurani, lakini lazima ihusishwe kwa ukaribu zaidi kwa kuwa inajua msingi na njia ilizopita Stars hadi kufikia hapo ilipo.

Watu wa kamati wameonyesha mapema kama vile ni wanajeshi wapya, wameingia kupambana. Lakini si wale wanaotaka kujua wanajeshi waliofikisha timu hapo walifanya vipi. Hilo ni kosa, TFF ipewe heshima yake, pia ipewe nafasi ya ushiriki wa karibu kwa kuwa ndiyo mhimili.

Kocha:
Bado nasisitiza, inapofikia wakati watu wa kamati wanataka kwenda kuzungumza na wachezaji kwenye kambo ya Taifa Stars, basi lazima TFF ihusishwe na kujua nini kinaendela.

Lakini muhimu zaidi ni kuheshimu ratiba ya kocha Kim Poulsen inasemaje. Msithubutu kufanya mambo kisiasa au kuangalia hamasa zaidi kuliko hali halisi inayohusu maandalizi.

Kama mwalimu atataka timu ipumzike, basi iwe hivyo na kusiwe na mjadala. Kwa kuwa haitakuwa na maana kama mtaingilia maandalizi kwa maana ya kuhamasisha, itakuwa kichekesho.

Mikakati:
Juzi, kamati hiyo imetoa Sh milioni 30 kwa Taifa Stars kama zawadi na kujenga morali. Jambo zuri sana, lakini lazima tukubaliane kutoa fedha pekee hakuwezi kuwa kila kusaidia kufanikiwa na kuibuka na ushindi dhidi ya Morocco.

Soka ina mipango, soka ina mapambano ya nje na ndani ya uwanja. Hivyo kamati inapaswa ijipange vilivyo na kuhakikisha ushindi na kufanya kazi ya ziada kwa kuwa jukumu walilokabidhiwa si lelemama na haliwezi kufanikiwa kwa kutoa motisha tu, badala yake wanatakiwa kuingia ‘msituni’ na kupambana.

Umakini:
Watu wote wa kamati ni “watu wa mpira”, hilo hali ubishi. Hofu yangu ni moja na ni vema nikaanza na mfano. Wakati fulani kuna mdau mmoja aliwahi kwenda katika kambi ya timu ya taifa, alikuwa anajulikana kama sehemu ya wahusika wa Stars kama ilivyo leo kwa watu wa kamati.

Alipofika pale akatoa jozi mbili za viatu na kumkabidhi mchezaji mmoja, hali ambayo baadaye ilizua mzozo wa chinichini katika kambi hiyo.

Inawezekana kabisa nia yake ilikuwa nzuri na mchezaji aliyepewa huenda aliomba msaada wa viatu. Lakini kwa kuwa aliyetoa alijulikana kama mhusika, tayari ikawa tatizo. Hilo ndilo ninataka kusisitiza kwamba lazima kuwe na umakini sana katika kushiriki na wachezaji.

Umakini hasa katika utoaji vitu na suala la usawa, vizuri 
kuwasaidia wote au kuacha. Kwani akionekana mtu wa kamati anamsaidia zaidi mchezaji au wachezaji fulani, tayari itazua mgawanyiko kupitia moyoni na mwisho morali “itauwawa” badala ya kuiimarisha.

Kuua morali na kusaidia timu ni sawa na kumpigia mbuzi gitaa, ndiyo maana nasisitiza sana suala la umakini katika hilo ili kamati iweze kuwa na matunda.

Sitaki kusema mengi, nimaamini nimeaminika kwa maana ya kusisitiza usawa, heshima kwa kocha, heshima na kuwajali TFF na wadhamini wao, Bia ya Kilimanjaro kama walioanza mbali na timu hadi kufikia walipo badala ya kamati kujiiona ina uwezo wa kila kitu bila ya kujua timu imefikaje ilipo.


1 COMMENTS:

  1. Good observation man, Kamati inabidi iangalie jambo hili. Linaweza kuonekana dogo sana, lakini likawa na madhara makubwa baadaye.
    abel

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic