May 17, 2013



 
Milovan akifanya mahojiano na Saleh Ally, mara baada ya mechi ya Ligi Kuu Bara mzunguko wa kwanza kati ya  Yanga na Simba iliyomalizika kwa sare ya bao 1-1...

Na Saleh Ally
MILOVAN Cirkovic ameingia katika rekodi kati ya makocha waliowahi kuzifundisha moja ya timu kubwa za Tanzania, lakini kikubwa zaidi ni kuiwezesha moja kushinda kwa mabao mengi katika mechi inayokutanisha watani.

Ushindi mkubwa zaidi katika mechi za watani nchini ni ule wa mwaka 1977 wakati Simba ilipoishindilia Yanga kwa mabao 6-0. 

Lakini kuanzia miaka ya 1980, 1990 na 2000, Milovan raia wa Serbia ndiye anashikilia rekodi ya kuwa kocha aliyepata ushindi mnono zaidi katika mechi ya watani.


Milovan aliiongoza Simba kuichapa Yanga mabao 5-0 katika mechi ya mwisho msimu uliopita, wakati huo Yanga ilikuwa ikitafuta heshima baada ya kuwa imeangukia katika nafasi ya tatu, nafasi ambayo ilikuwa haijawahi kuishika tokea mwaka 1988, mara zote ilikuwa bingwa au nafasi ya pili.

Kesho Simba na Yanga zinarudi uwanjani, ‘hadithi’ za mechi hiyo hazina tofauti kabisa na mechi iliyopita, kama ilivyokuwa Simba bingwa msimu uliopita, zamu hii ni Yanga na Msimbazi wanaendelea kutafuta nafasi ya tatu na wanataka waishinde Yanga.


Yanga ambao ni mabingwa, wanataka kushinda kwa ajili ya kusherekea kombea lao raha mustarehe lakini kuanzia viongozi, makocha, wachezaji na hata mashabiki wanachotaka ni kulipa kisasi cha mabao 5-0 waliyofungwa katika mechi ya kufunga msimu uliopita.


Yanga nao wanataka kufunga msimu kwa heshima na kikubwa ni kurudisha adhabu ya kipigo na ikiwezekana tano zote zirudi.  Katika mechi hiyo mabao ya Simba yalifungwa na Abdallah Kibadeni dk 10, 42, 89, Jumanne Masimenti dk 60, 73 na Selemani Saidi wa Yanga aliyejifunga katika dk 20.

Milovan ambaye sasa amerejea anaishi katika mji aliozaliwa wa Cacak nchini Serbia anasema kama ni soka pekee bila ya mipango mingine yoyote, Yanga haina uwezo wa kuifunga Simba bao 5-0.

Mahojiano kati ya Salehjembe na Milovan kutoka Serbia yalikuwa hivi:
Salehjembe: Yanga wanajiamini sana na wanaamini kuishinda Simba ni lazima?

Milovan: Wanakosea, mpira hauchezwi kwa hisia, lazima ujipange, uingie uwanjani na kuanza kutafuta matokeo.

Salehjembe: Kama ilivyokuwa Simba, timu bora msimu uliopita, safari hii ni Yanga. Hauoni wana haki ya kujiamini kwa watashinda tena kwa idadi kubwa?

Milovan: Kujiamini ni haki yao, hamuwezi kwenda uwanjani hamjiamini. Lakini kuifunga Simba itabidi wacheze kwa mipango zaidi na kuwazidi lakini si kuamini hivyo kabla ya kucheza.

Salehjembe: Inawezekana wakashinda mabao matano na kulipa kisasi?
 Milovan: (kicheko), Yanga watakosea zaidi kuanza kuwaza bao tano wakati hawajafunga hata moja. Hilo ni kosa.

Salehjembe: Kwani wanatakiwa kuwaza vipi?
Milovan: Kawaida ukifunga bao moja, unafikiria la pili, ukifunga la tatu unapanga la nne. Hivyo ndivyo mambo yanakwenda.

Salehjembe: Nakumbuka siku chache kabla ya mechi ya Yanga mlioshinda tano, ulisema mnaweza kushinda tano?
Milovan: Kweli, nilisema tunaweza. Sikwenda nasema tunakwenda kuishinda tano, badala yake niliamini inawezekana, lakini isingekuwa hivyo kusingekuwa na tatizo nilichotaka ni ushindi. Lakini Yanga wanataka tano tu, hilo ni kosa.

Salehjembe: Unakionaje kikosi cha Simba?
Milovan: Simba ni timu yenye vikosi bora Tanzania, utaona pamoja na matatizo yote iko katika nafasi ya tatu. Maana yake, Yanga hawapaswi kuidharau, wanaweza kujikuta wanashangaa.

Salehjembe: Nilifikiri ungekuja kuangalia mechi hiyo ya Jumamosi?
Milovan: Nilitamani maana wanaocheza ni vijana wangu, nawapenda na kuwakumbuka sana. Lakini sitaweza ila nitafuatilia kila kitu kupitia mitandao. Tanzania bado ni rafiki wengi na ninakupenda sana.

Salehjembe: Nashukuru kwa ushirikiano Profesa Cirko.
Milovan: Nashukuru, wewe matatizo sana...

SOURCE: CHAMPIONI




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic