June 29, 2013



Bin Slum ofisini kwake Kariakoo jijini Dar es Salaam


*ASISITIZA YEYE NI COASTAL TOKEA MDOGO MWANZO MWISHO, AZIKANA SIMBA, YANGA
Na Saleh Ally
KUTOKANA na mambo yanavyokwenda Coastal Union inaonekana kuwa moja ya timu zitakazokuwa tishio kubwa msimu ujao.

Coastal Union ni moja ya timu kubwa katika soka ya Tanzania, lakini ilionyesha kupoteza mwelekeo hadi iliporejea tena ligi kuu misimu miwili iliyopita.
Mohammed Bin Slum ni kati ya watu waliokuwa wakitoa msaada katika Coastal Union tokea ikiwa katika hali mbaya hadi sasa imeonyesha kuwa si timu ya kubahatisha mambo.

Msimu uliopita imemaliza ikiwa katika tano bora, mafanikio yake yanaonyesha timu hiyo inaweza kurejea katika heshima yake ya enzi zile ikiwa moja ya timu tishio kabisa.

Hata usajili wake wa msimu huu, tayari unaonyesha Coastal Union ni kati ya “Big Four” za Ligi Kuu Tanzania Bara. Timu nyingine ni Yanga, Simba na Azam FC ambayo tayari imejihakikishia tatu bora tena ikiwa nafasi ya pili kwa misimu miwili mfululizo.
Lakini yote hayo na mafanikio ya Coastal Union, vigumu ukayazungumzia bila ya kuitaja ‘injini’, Bin Slum ambaye sasa pamoja na kuwa mdhamini, anashikilia nafasi ya mkurugenzi wa ufundi katika klabu hiyo.

Juhudi za Bin Slum ingawa alizianza muda mrefu tena kimyakimya lengo likiwa ni kuisaidia Coastal Union, sasa zinaanza kuonekana hadharani na mwenyewe anasisitiza “atakufa na Coastal Union” maarufu kama Wagosi wa Kaya.

Bin Slum aliyezaliwa Tanga na kupata elimu yake mkoani humo hadi kidato cha sita kabla ya kuhamia jijini Dar es Salaam ambako alianza maisha yake ya biashara, anaamini Coastal Union ina nafasi ya kurejea katika kilele na kuanza kusumbua kama ilivyotwaa ubingwa wa Tanzania Bara mwaka 1988.

Bin Slum ambaye ni mmoja wa wachezaji wa zamani wa timu ya mkoa wa Tanga, maarufu kama Tanga Stars anasema yeye amekuwa shabiki wa Coastal Union tokea azaliwe. 

Kingine ambacho anaeleza na huenda kikawashangaza wengi ni kwamba hajawahi kuingia hata mara moja uwanjani katika mechi kubwa kuliko zote za soka ya Tanzania ambayo kawaida huwakutanisha watani wa jadi, Yanga na Simba.

Salehjembe: Inashangaza kidogo kwa mfadhili wa timu kubwa kama Coastal, mdau wa soka kusema hujawahi kuingia katika mechi kubwa ya watani?
Bin Slum: Kwani kuna ulazima gani kuingia kwa kuwa mimi si Simba wala Yanga.
Salehjembe: Haushabikii timu moja kati ya hizo?
Bin Slum: Haijawahi kutokea, nimekuwa Coastal Union tokea utoto hadi leo.

Salehjembe: Kipi kinafanya usiende katika mechi inayowakutanisha watani Yanga na Simba?
Bin Slum: Kwanza bugudha ya kuingia na kutoka uwanjani kwa kuwa watu ni wengi, lakini hakuna timu ninayoishangilia. Nimewahi kuangalia mechi ya Simba dhidi ya Yanga kwenye tv ilipokuwa inaonyeshwa na Supersport. Ukiachana na hivyo sijawahi kwenda uwanjani.


Salehjembe: Maana yake hujawahi kuziona Yanga na Simba zikicheza live?
Bin Slum: Nimewahi, lakini labda iwe Simba na JKT au Yanga na timu nyingine lakini si siku zinapokutana zenyewe.

Salehjembe: Unafikiri inawezekaan mtu kuwa shabiki wa soka hapa nchini bila kupenda Yanga au Simba?
Bin Slum: Kabisa, mimi ni mmoja wapo. Mimi si Yanga au Simba kama nilivyokueleza. Watu hawaelewi na wanaona haiwezekani. 

Salehjembe: Kivipi? Fafanua tafadhari.
Bin Slum: Mimi Coastal wa kuzaliwa kabisa, tokea mdogo baba yangu alikuwa akinishika mkono na tunakwenda wote uwanjani. Hivyo sijawahi kushabikia timu nyingine hapa nyumbani, zaidi kama England ni Liverpool lakini si Simba wala Yanga.

Salehjembe: Wengi wanaamini haiwezekani, kwako imekuwa vipi lahisi?
Bin Slum: Wengine wamezichagua Simba au Yanga, lakini mimi nimeanza kuipenda Coastal Union nikiwa mtoto. Ndiyo maana hata ilipokuwa daraja la kwanza nilikuwa tayari kwenda hadi viwanja kama Mabatini kwenda kuona inacheza. Mfano mechi ya Simba na Yanga ya kufunga msimu, mimi nilikuwa Morogoro kwa kuwa Coastal ilikuwa inacheza.

Katika mechi hiyo Coastal isingechukua ubingwa wala nafasi ya pili, lakini kwangu ni bora kusafiri hadi Morogoro kuiona Coastal Union inacheza kuliko kuona Simba na Yanga Dar es Salaam.

Salehjembe: Vipi kuhusu usajili wa Coastal Union?
Bin Slum:Kwa kushirikiana, ninamini tumefanya usajili vizuri sana. Coastal union itafanya vizuri zaidi ya msimu uliopita.

ITAENDELEA SEHEMU YA PILI NA YA MWISHO…

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic