June 17, 2013





Na Saleh Ally
GUMZO katika soka la Ivory Coast kwa kipindi hiki ni kocha mpya wa timu ya taifa ya nchi hiyo, Sabri Lamouchi, ambaye amechukua uamuzi mgumu ambao umewashangaza wengi.

Lamouchi raia wa Ufaransa akiwa na asili ya Tunisia ameamua kumuacha nahodha wa timu hiyo, Didier Drogba, tena katika kipindi kigumu wakati timu yake ikiwa katika mbio za kupata nafasi ya kubeba ubingwa.


Pamoja na hivyo, Lamouchi amemuacha beki mkongwe wa kati, Kolo Toure, na kuamua kutumia vijana zaidi katika mapambano ya kuwania kucheza Kombe la Dunia mwakani nchini Brazil.

Championi Jumatatu, lilifanya mahojiano maalum na Lamouchi saa chache kabla ya mechi ya jana dhidi ya Taifa Stars na akazungumzia mambo kadhaa.


Lamouchi ni kiungo mahiri wa zamani wa timu ya taifa ya Ufaransa, lakini alikipiga katika klabu kubwa kama Ales, Auxerre, Monaco za Ufaransa, Parma na Inter Milan za Italia. 

Pamoja na kusisitiza kwamba wamekuwa na maandalizi makubwa kabla ya mechi dhidi ya Tanzania kuliko kawaida, lakini amelenga zaidi kujenga nidhamu upya kwa kuwa timu nyingi za Afrika Magharibi zilikumbana na suala la ukosefu wa nidhamu.


Pamoja na hivyo, Lamouchi akasisitiza Drogba bado anaendelea kuwa nahodha wa timu hiyo na ana nafasi kubwa ya kurejea katika kikosi hicho huku akiona nafasi kama hiyo kwa Kolo ingawa anaiona ni ndogo sana.
Salehjembe: Vipi maandalizi dhidi ya Tanzania yawe makubwa kiasi hicho wakati ni timu ndogo?

Lamouchi: Tanzania si timu ndogo tena, angalia mechi dhidi yao kule Abidjan, haikuwa kazi rahisi kuwafunga. Lakini mechi hii ni kama fainali kwetu.
 
Lamouchi wakati akikipiga Marseille..
Salehjembe: Fainali huenda ikawa dhidi ya Morocco na si Tanzania.
Lamouchi: Tukishinda dhidi ya Tanzania, maana yake tumebakiza asilimia kumi tu ambayo tutaweka nguvu zote.


Salehjembe: Umemuacha Drogba, Kolo. Huoni ni presha kubwa ukipoteza nafasi ya kucheza Kombe la Dunia?
 Lamouchi: Inawezekana kupoteza ingawa hatutaki itokee. Lakini ikitokea pia si presha, hii ni Ivory Coast na kila mchezaji mwenye uwezo ana haki ya kuisaidia nchi yake hasa kama nimeona anafaa kufanya hivyo.

Salehjembe: Drogba na Kolo wana nafasi ya kurejea kikosini, au uzee tayari ni tatizo?

Lamouchi: Drogba ana nafasi kubwa, ninaamini atarejea. Kiasi alipoteza kidogo kasi alipokuwa China, inawezekana kutokana na ligi yenyewe. 
 Lakini sasa yuko Uturuki , ligi ngumu na yenye ushindani, pia amecheza Ligi ya Mabingwa Ulaya. Hivyo ni suala la wakati tu.

Kuhusu uzee, Drogba hajafikia huko ingawa umri umekwenda. Bado anaweza kuwa na msaada mkubwa kutegemeana na mechi. Ndiyo maana timu kubwa kama Galatasaray inaweza kumuamini.

Salehjembe: Vipi kuhusu Kolo?
Lamouchi: Sidhani kama naweza kusema ana nafasi kubwa, kuna vijana wengi wanaocheza kwenye nafasi yake kwa ubora zaidi. Lakini inaweza kutokea nikamuita. Ingawa ni vizuri kusema hana nafasi.

Salehjembe: Unafikiri Yaya, Gervinho na Kalou ndiyo tegemeo pekee la Ivory Coast?
Lamouchi: Hilo ni kosa kubwa, pia nimekuwa nikiwakumbusha wachezaji wote kwa kuwa nina uzoefu wakati nikiwa mchezaji. Kila mchezaji anayekuwa katika kikosi, pia kwenye benchi ni tegemeo la timu. Kocha haangalii majina, anaangalia nani ana msaada katika wakati husika.

Salehjembe: Baada ya Ivory Coast, unafikiri utaendelea kufundisha timu nyingine za Afrika au utarejea kufanya kazi katika klabu za Ulaya?
Lamouchi: Nilikuwa mchezaji, sasa ni kocha. Chochote kitakachokuwa bora, kama ni klabu kubwa ya Ulaya au timu ya taifa ya Afrika. Litakuwa ni suala la maslahi, lakini si pekee kwa kuwa nina ndoto nataka kuzitimiza.
Salehjembe: Ndoto zipi?
Lamouchi: Zitabaki kuwa siri yangu, siku moja zikitimia nitasema.

Salehjembe: Nashukuru.
Lamouchi: Sawa.

Baadaye jana jioni Ivory Coast iliifunga Stars kwa mabao 4-2 na kuitoa kwenye reli kabisa ya kuendelea kuwania kutaka kucheza Kombe la Dunia mwakani.

Mechi ilikuwa nzuri na yenye mvuto, lakini tatizo kubwa likawa ni umakini katika uchezaji wa kikosi cha Stars hasa wakati kikosi kinashambuliwa.
Stars haikuwa na safu ngumu ya ulinzi kwa maana ya kikosi kizima kuimarisha safu yake.

Lakini kwa makosa ya mchezaji mmoja mmoja, beki Erasto Nyoni pia alishinda kumthibiti Gervinho ambaye alimgeuza njia.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic