June 17, 2013



Aliyekuwa Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Liewig yuko jijini Dar es Salaam akisubiri kulipwa fedha zake baada ya uongozi wa timu hiyo kumfuta kazi.
Simba imemfuta kazi Liewig raia wa Ufaransa baada ya kuamua kuvunja naye mkataba na kumpa mzawa Abdallah Kibadeni na atasaidiwa na Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ aliyekuwa msaidizi wa Liewig.

Liewig alikuwa analipwa dola 6,000 (zaidi ya Sh 9.7) kwa mwezi, mkataba wake unaonyesha anatakiwa kulipwa mshahara wa miezi miwili.

Lakini kama hiyo haitoshi inaonyesha Liewig alikuwa anaidai Simba mshahara wa miezi mingine miwili na nusu, maana yake dola 15,000 (zaidi ya Sh milioni 24.5).

Ukijumlisha, Liewig anaidai Simba Sh milioni 44.1 kiasi ambacho ni kikubwa kwa klabu hiyo ukizingatiwa iko katika kipindi kigumu cha usajili na maandalizi ya msimu mpya.


Kwa kuwa fedha ni ngumu, lazima kutakuwa na ugumu kwa vile Simba ina mahitaji mengi muhimu, hilo halina ubishi. Lakini hakuna ujanja lazima walipe wanachodaiwa na kocha huyo mtu mzima.

Tokea amekuja, Championi lilikuwa la kwanza kufanya mahojiano naye na alisema hahitaji malumbano na alichotaka ni kuhusiana na fedha zake, alipwe ili aondoke kwa amani.

Hivyo ni vizuri hilo likafanyika, alipwe fedha zake kama inavyotakiwa ili aondoke, kama itashindikana kulipwa zote, basi alipwe kiasi fulani na mwisho kuwe na makubaliano ambayo yatatekelezeka.

Simba wanatakiwa kufanya hivyo hata kama wako katika hali ngumu kwa kuwa huo ndiyo uamuzi sahihi kutokana na walichokiamua.

Tukirudi miezi sita tu, tunakutana na saga la aliyekuwa kocha wa timu hiyo, Milovan Cirkovic raia wa Serbia ambaye alikuwa anadai takribani dola 33,000 baada ya mkataba wake kuvunjwa.

Staili ya kufukuzwa kwake haipishani na hii ya Liewig, naye alilazimika kurudi na kusaka fedha zake na uongozi wa Simba ukashindwa kulipa ‘kwa makusudi’ hadi mlezi wao Malkia wa Nyuki alipoamua kufuta aibu hiyo kubwa.

Sidhani kama Malkia wa Nyuki anatakiwa kurudi tena na kufuta deni la Simba, uongozi ulifikia uamuzi wa kumuondoa kocha huyo, basi lazima ulikuwa unajua cha kufanya.

Walimuondoa Milovan, mimi sikuona kama ni sawa hasa ukilinganisha na uwezo wa Liewig, Simba wakasema wanamjua zaidi, leo wamemuondoa tena kwa mtindo uleule nao wakiwa wamekubali kweli kama ulivyokuwa ufafanuzi wangu.

Vizuri wakajiondoa katika kuonekana ni timu iliyojaa watu wasiojali heshima na jina la timu hiyo na kuonekana ndiyo wanaoongoza kwa kudhulumu makocha.

Hakuna ambacho Simba wanaweza kusema kama kisingizio, kwani uamuzi wa kumuondoa kocha ulikuwa wa kwao. Unaweza kusema wanaitia hasara klabu kwa hesabu zinazolazimu kutumia mamilioni ya fedha bila sababu za msingi.

Kuna taarifa zinaeleza kwamba uongozi wa Simba umepanga kukutana na Liewig Jumapili na kulijadili suala hilo ikiwezekana mwafaka upatikane.
Lakini kwa heshima ya Simba na hali halisi, hawana ujanja ni lazima walipe, yaliyotokea kwa Milovan yasirudie kwa Liewig maana itakuwa ni zaidi ya kuharibu.

Simba ni klabu kubwa, hilo halina ubishi na inastahili heshima. Utekelezaji wa mambo kwa uhakika ni sehemu ya heshima, kuwa na viongozi wasiobahatisha mambo ni sehemu ya kuonyesha ukubwa wa Simba na ubora wa ufanisi wao, basi suala la Liewig limalizwe kitaalamu zaidi.

 


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic