June 28, 2013



 Na Saleh Ally
Tayari mshambuliaji Nonda Christophe Nonda ameamua kustaafu soka, sasa anaendelea na maisha mengine, mfano suala la uhamasishaji wa amani katika sehemu mbalimbali duniani.

Yanga ambayo ndiyo chachu ya Nonda kuanza kupata mafanikio, imekuwa ikiumia na majeraha makubwa ambayo dawa yake ingekuwa mshambuliaji huyo kama kila kitu kingekwenda kwa mpangilio.
 
NONDA (WA TATU KUTOKA KUSHOTO WALIOSIMAMA) WAKATI AKICHEZEA YANGA
Viongozi wa soka nchini ni watu wanaojali maslahi yao binafsi hata kuliko soka ya Tanzania ndiyo maana imedumaa, wako wanaowatetea lakini ni vigumu sana kukwepa ukweli, kwa kuwa mifano ni mingi na hili la Nonda ni sehemu tu.

Ukiangalia katika rekodi za Nonda kimataifa, zinakuonyesha mshambuliaji huyo alianzia Vaal Professional ya Afrika Kusini, wazungu hawajui lolote kwa kuwa Yanga walifanya madudu makubwa wakati wa kumuuza.
 
HOTELI ANAYOMILIKI NONDA MJINI KINSHASA...
Sheria za Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) zinataka mchezaji anapouzwa, basi lazima kuwe na faida kwa klabu inayomuuza katika misingi ya asilimia.

Nonda alikuwa na uwezo wa kuiingizia Yanga zaidi ya milioni 500 katika kipindi ambacho alikuwa anauzwa kutoka klabu moja kwenda nyingine, lakini ikawa vigumu kwa kuwa uongozi wa Jangwani kipindi hicho chini ya George Mpondela haukuwa umejali hilo.

Viongozi waliokuwa madarakani waliangalia maslahi yao kipindi hicho na taarifa zinaelezwa Nonda aliuzwa kwa dola 10,000 tu na viongozi wakachanganyikiwa. Kikubwa mkataba ulisema vipi kama Nonda angeuzwa klabu nyingine.

Inaonyesha viongozi waliangalia fedha hizo siku wanakabidhiwa, hawakuona umuhimu wa kuingia mkataba wa uhakika ambao ungeisaidia Yanga kuendelea kuigiza fedha kwa miaka mingine 15 au zaidi baada ya hapo.

Angalia hapa namna uhamisho wa Nonda ulivyokuwa na huenda Yanga ingepata kiasi gani kwa kuwa mara nyingi klabu kama Yanga ingekuwa inapata asilimia 10 kila anapojiunga na klabu nyingine.


Mwaka 1995 ndiyo alijiunga na Vaal Professional baada ya kumuona akiichezea Yanga, tena aliingia kwa kuwa namba yake ilikuwa inathibitiwa na Mohammed Hussein Daima maarufu kama Chinga One.

Vaal ilimpata kwa dola 10,000 tu, yenyewe ikamuuza kwa dola 150,000 kwa klabu ya FC Zürich ya Switzerland, hiyo ilikuwa ni mwaka 1996, hapa Yanga ingepata dola 15,000, lakini ikaambulia patupu.

Nonda aliibuka mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Switzerland, soko lake likapanda na mwaka 1998 akauzwa Rennes kwa kitita cha dola milioni 9, Yanga ilitakiwa kupata dola 900,000. Na miaka miwili baadaye Nonda akajiunga na AS Monaco kwa uhamisho uliovunja rekodi wa dola milioni 25 million, Yanga ilitakiwa kupata dola 250,000.

Bado Nonda aliendelea kuhama kwenda AS Roma, Blackburn kwa mkopo na mwisho Galatasaray ya Uturuki, nafasi anayocheza leo Didier Drogba.
Hii inaonyesha kuwa Yanga ilipoteza zaidi ya Sh milioni 500 katika kipindi hicho kutokana na uzembe wa uongozi wake kipindi hicho kwa kuwa uliona dola 10,000 ilikuwa ni kama fedha  zilizohifadhiwa na benki zote duniani.

Yanga imebaki inajisifia kitu kimoja tu, kwamba Nonda aliwahi kupita hapo, kitu ambacho hakina faida yoyote zaidi ya kuonekana hakuna lolote.

Hapa kuna masomo mawili kwa Yanga na timu nyingine ambazo zinaweza kupata nafasi ya kuwauza wachezaji wake Ulaya au kwingineko ambako soka limepiga hatua. 

Kwanza kung’amua mapema kwamba umuhimu na upana wa biashara kwa kuwa katika nchi zilizopiga hatua wanalijua hilo na wanakuwa wajanja sana kuwamaliza viongozi waliozubaa kama walivyokuwa wa Yanga kipindi hicho kwa kuwa walichanganywa na dola 10,000.

Katika hilo, bado viongozi wajifunze kuingia mikataba iwe ni ya mauzo au kazi ambayo inaweza kuwa na msaada mkubwa kwa klabu na si wao binafsi. Kama wanakuwa hawaelewi, vizuri wapateushauri kutoka kwa wataalamu na si kujiona wanajua sana, kumbe hamna kitu.

Somo la pili ni kuhusiana na Nonda mwenyewe, kabla ya kuja Yanga aliichezea Atletico ya Burundi, hakuwa tegemeo na muda mwingi aliutumia kufanya kipindi cha DJ Show katika redio moja mjini Bujumbura.

Baada ya kutua Yanga hakuwa staa pia, zaidi alicheza katika timu ya pili kabla ya wachezaji wengi nyota kama akina Edibily Lunyamila kuondoka, yeye na wenzake kama Anuar Awadhi, Maalim Saleh ‘Romario’ kutoka kikosi B wakapandishwa na kuwa timu kubwa.

Siku chache baadaye akauzwa Afrika Kusini na inaonekana hivi, kama viongozi Yanga hawakufanya ‘usamjo’ na kuchukua fedha zile kwa faida yao, basi walidharau na kuona kama Nonda kawapa faida kubwa na hakuwa na lolote.
Kama ni hivyo walitakiwa kujiuliza kwa nini timu kutoka katika ligi iliyoendelea kuliko Yanga inamhitaji? Halafu wangepata jibu na kunusa faida mbele yao na mwisho wangeingia mikataba yenye faida.

Vaal wasingekubali kufanya kosa kama la Yanga, lazima watakuwa wamefaidika vilivyo kutokana na mchezaji huyo, huku Yanga wakibaki na sifa tu, eti “alipita hapa”. Halafu?
SOURCE; CHAMPIONI

1 COMMENTS:

  1. bado naamini, ska letu linaongozwa na watu dhaifu , dhaifu , dhaifu.
    Makosa aliyoyafanya Mpondela katika usajili wa Nonda hadi kuikosesha Yanga mamilioni hadi leo huwenda yanaweza kujirudia.
    na kwa wachezaji wetu, Nonda lazima awe somo kuwa Kipaji ni kichochocheo tu, lakini nidhamu na maadili ya soka ni kila kitu.
    wako wapi kina Mohamed Hussein Machinga na Edibily Lunyamila ? walimzidi kipaji tena kwa mbali, lakini Nonda aliwazidi ujanja na akili ya soka.

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic