July 18, 2013



*Aeleza matatizo mambo yalivyokuwa, siku alipozinduka, namna P Funk alivyompa dili feki la Sh milioni 200
*Sasa aandaa albamu, inamhusu Mangwea, apanga kujichora tatu ya marehemu

Na Saleh Ally
Msanii wa muziki wa kizazi kipya, Mgaza Pembe maarufu kama M To The P, alizushiwa kifo siku moja baada ya rafiki yake kipenzi Albert Mangweha ‘Mangwea’ au ‘Ngwea’ kufariki dunia jijini Johannesburg nchini Afrika Kusini.

Ngwea alikutwa chumbani akiwa na M To The P, wote wakiwa hawajitambui na walipokimbizwa hospitali, Ngwea aliaga dunia na yeye akalazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi (ICU). Baada ya hapo mengi yalitokea.

M To The P amepita katika mengi hadi alivyorejea nyumbani salama na sasa yuko katika hatua za mwisho za maandalizi ya albamu yake mpya. Lakini hapa katika mahojiano exclusive na Championi Ijumaa, anaelezea mengi yaliyotokea kuanzia siku ya tukio hadi alivyorejea jijini Dar es Salaam na baadaye kwenda Morogoro kushiriki mazishi ya rafiki yake kipenzi.

Siku ya tukio:
Siku hiyo nakumbuka tulikuwa na washkaji, tuliungana pamoja na kwenda kusherekea. Unajua kabla ya hapo tulichelewa ndege baada ya kupitiwa na usingizi. Hivyo safari hiyo hatukutaka kurudia kosa tena, kwa kuwa ndege ilikuwa ni Saa 12:30 asubuhi, tulikubaliana tusilale.

Tulilazimika kutolala kuepuka kuchelewa ndege, maana baada ya kuchelewa ndege ya kwanza, ili tiketi yetu iendelee kuwa hai na kuitumia wakati mwingine tulilazimika kulipa rand 1200 (Sh milioni 1.7), hatukutaka kuingia tena gharama kwa uzembe.

Hivyo tukaondoka kwenda kujiachia (kusherekea) na washkaji na lengo likiwa ni kuhakikisha hatulali, baadaye tulienda klabu na baada ya kuona muda unakaribia, nakumbuka ilikuwa Saa 10 usiku, tukaamua kurudi nyumbani kuchukua mizigo yetu kwa ajili ya safari.

Hakika huko ndiyo matatizo yalianzia, kweli nikikumbuka roho inaniuma sana na kuna mambo mengi hadi leo yananiumiza sana. Ila nakuhakikishia hivi vitu kuanzia hapo siwezi kuvizungumzia kwenye vyombo vya habari hasa kwa wakati huu. Subiri muda ukifika, lazima tujue mchini (Ngwea) ana mzazi wake, pia familia. Hivyo tuwaonee huruma pia kuwa watajisikiaje.

Nilipozinduka:
Kuhusu kuzinduka kwangu naweza kuelezea, baada tu ya kupata fahamu nilianza kumuulizia mchini wangu, nikaambiwa alikuwa ametangulia Dar. Kidogo nikashangaa, vipi aliniacha wakati tulitakiwa kuondoka wote!

Yule daktari mzungu alinisisitizakuwa natakiwa kupumzika, sikujua nilikaa hapo siku ngapi, lakini baadaye nilielezwa kuwa nilikaa siku mbili, nikauliza vitu vyangu ikiwemo mizigo ilikuwa imepotea pia.

Baada ya siku mbili nilitolewa wodi ya watu mahututi (ICU), nikapelekwa ya kawaida ambako pia nilitoka baada ya siku kadhaa nakumbuka Jumatatu kamaa saa moja usiku ndiyo niliruhusiwa na kibali cha kuruhusu mwili wa Ngwea kikatoka siku hiyo saa 4:30 usiku.


Nafikiri walisubiri kuniona niko fresh ndiyo watoe kibali, lakini muda wote huo mimi sikujua kitu chochote kwa kweli kuhusiana na msiba.

Kuchungwa:
Nilichukuliwa na kupelekwa kwa mshkaji mmoja, nilikaa huko na nilianza kushangazwa kila nilipokuwa napigiwa aliiwahi simu yangu na kuichukua halafu yeye ndiyo alizungumza na huyo mtu. Nilishangaa kwa kuwa haikuwa kawaida, nikadhani huenda kwa kuwa ni mgonjwa hakutaka nizungumze sana, sikujali sana.

Dili la Sh 200m:
Siku hiyo hiyo, P Funky alinipigia simu, akanieleza kuwa kuna dili la kurekodi muvi, limefikia hadi Sh milioni 200 na nilikuwa natakiwa mimi kwa kuwa nilianza kuifanyia mazoezi halafu baadaye wenyewe wakaahirisha. Nakumbuka hiyo muvi ilikuwa imepewa jina la Sarkana.

Nilishangazwa na wingi wa fedha, lakini niliona inawezekana maana muvi ni nzuri. Wakanikatia tiketi ya Jumanne, lakini baadaye ikabadilishwa, hata sikujua sababu. Kumbe siku hiyo ndiyo mwili wa Ngwea ulikuwa unasafirishwa tena na ndege ambayo nikapanda.

Wakanikatia ndege ya South African ambayo walijua wanapanda wazungu wengi, huenda ingekuwa vigumu kukutana na mtu ambaye angenipa pole na kufanya nijue tatizo. Nilipofika Dar es Salaam, gari nne zilikuja kunipokea, nilikuwa kama mheshimiwa au mtu fulani tajiri, waliniingiza katika moja ya gari na tukaondoka haraka kwa kasi.

Kidogo ilinishangaza, P Funk aliendelea kusisitiza kwamba sikutakiwa kuonekana kutokana na ile ishu ya muvi. Siku hiyo Dar kulikuwa na foleni sana, ingawa nilitua moja na nusu hivi, tulifika Mikocheni Saa tano usiku na huko ndiyo nilifichwa.

Baada ya kufika walifanya kama tunafanya mkutano fulani hivi kuhusiana na ile muvi na mimi nikaamini dili lilikuwa limeiva. Lakini ilipofika saa nane usiku ndiyo wakaniambia ukweli kwamba kulikuwa na tatizo kubwa na mchini wangu (Ngwea) alifariki dunia. Kwangu ilikuwa ni vigumu kuamini tu kwa maneno.

Mwili kwenye Ipad:
Kwa mara ya kwanza kuhakikisha kuwa ni kweli niliona kwenye picha kweli mchizi (Ngwea) alikuwa amefariki, picha za video kwenye Ipad, zilifanya nithibitishe. Pale ndiyo walinionyesha watu walivyokuwa wanaanga siku hiyo, sikuamini, nikachanganyikiwa na kuanza kulia sana.

Walinitaka kujikaza kwa kuwa kesho yake alfajiri nilitakiwa kuanza safari ya kwenda Morogoro kwenye mazishi. Nilijitahidi lakini ilikuwa vigumu sana kwangu, sikuacha kulia hadi siku iliyofuata. Kweli siku hiyo alfajiri tukasafiri kwenda Morogoro kwa ajili ya kuuaga mwili wa Ngwea pamoja na mazishi.

Kweli nisingependa kuelezea zaidi kuhusiana na Mangwea, natakiwa kukutana na familia, hasa Bi Mkubwa wake (mama), ili nimuelezee kila kitu. Sasa siwezi kuendelea zaidi hadi hapo nitakapomueleza. Hivyo vizuri tukaishia hapa.

Jina M To The P:
Maana ya jina hili ni Mgaza wa Pembe, ndiyo maana M, yaani Mgaza to the, nikimaanisha wa P, Pembe. Najua kunakuwa na ugumu kidogo lakini ndiyo nililiweka hivyo kisanii.

Muziki:
Nilikuwa karibu sana na Mangwea, lakini mimi pia ni msanii wa siku nyingi. Sasa ninachofanya nimeamua kurudi kwa nguvu kubwa na niko ‘siriaz’ sana. Tayari singo ya kwanza imekamilika inaitwa Masambe Wena, yaani twende zetu kwa lugha ya Kizulu ambayo asili yake Afrika Kusini.

Ndani yake nimewashirikisha Chegge na Country Boy. Maana yake kuna kwaito na hip hop. Singo hiyo itaanza kusikika kwa mara ya kwanza Jumatano (juzi). Humu pia nimetua baadhi ya sauti za Ngwea.

Songi linalofuata:
Singo inayofuata itakuwa ni Mungu Ndiyo Anapanga, humu ndani nimemshirikisha Diamond na Jay Mo, tena hautachelewa kuingia katika redio mbalimbali baada ya Masambe Wena. Ninafanya hivyo kwa kuwa nataka mambo yaende haraka pia katika mpangilio mzuri.

Ndani ya singo hii, kuna baadhi ya mambo yaliyotukuta na Mangwea nayaelezea na wenye hamu ya kusikia huenda angalau wakakata kiu chao.

Albamu:
Tayari nyimbo nne zimeishakamilika katika albamu yangu zikiwemo hizo za Masambe Wena na Mungu Ndiyo Anapanga. Lakini lengo ni kufanya albamu yenye nguvu ambayo itakidhi kiu ya mashabiki kutokana na ushindani sokoni.

Albamu itatoka haraka iwezekanavyo na kwa kushirikiana na P Funk na watalaamu wengine, tumekuwa tukifanya kazi usiku na mchana kuhakikisha mambo yanakwenda.

Taasisi:
Hii Mangwea foundation itakuwa inafanya mambo kadhaa ya kuendeleza muziki. Lakini zaidi inalenda suala la kuangalia alichokuwa amekianzisha Mangwea wakati akiwa hai.

Mfano kuna nyimbo zake nyingi sana zilizo katika studio mbalimbali, tutazikusanya na kutengeneza albamu kali ambayo mapato yataingia katika foundation. Lakini bado watu watapewa nafasi ya kutumia baadhi ya sauti zake katika nyimbo zao. Kwa kweli kuna mambo mengi sana ambayo yatafanyika kwa ajili ya kusaidia jamii.

Denja Vu:
Hawa ni vijana waliokuwa chini ya Mangwea, wana vipaji na nisingependa vipaji vyao vife. Hivyo nitashirikiana na wadau wengine akiwemo P Funky kuhakikisha tunawaendeleza. Mmoja tayari nimempa nafasi katika singo ya Masambe Wane na amefanya vizuri.

Lengo hapa ni kusaidia vipaji vingine lakini pia kuonyesha tunakubali kile kilichoanzishwa na Ngwea kuwa aliona ni kitu cha msingi na tunakiunga mkono:

Tatoo ya Mangwea:
Najiandaa kuchora tatuu kubwa mgongoni ambayo itakuwa na picha ya Mangwea, nitafanya hivi kuonyesha upendo wangu kwake na hii si mara ya kwanza.

Nilianza kuchora tatuu ya machozi baada ya kufiwa na mama yangu mzazi, hii ilikuwa ni kuonyesha mapenzi yangu kwake. Lakini nina tatuu nyingine ya gitaa, hii ni kuonyesha mapenzi yangu katika muziki ambao uko katika damu yangu.


Maana yake tatuu ya Ngwea itakuwa ni ya tatu kwangu na mambo yote utaona ni mapenzi ya dhati na ninaamini hii itatuu ya Mangwea itakuwa ni gharama kubwa.

1 COMMENTS:

  1. Asizingue, anajua kilichotokea ndo mana anataka kwanza aongee na Mama Ngwea halafu kila mara anasema kuna mengi yametokea, halafu wale Madaktari si Waganga wa kienyeji kumponya bila kujua tatizo...kwani walipiga ramli??

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic