July 11, 2013





Lawama za kwamba wachezaji wamekuwa ni watovu wa nidhamu zimekuwa zikisambaa kila kukicha na kuna mambo mengi sana ya kuthibitisha kwamba kuna wachezaji Fulani wamekuwa wakihusika na vitendo hivyo.

Hakuna ubishi, wachezaji lukuki tumesikia wamekamatwa wakifanya vitendo vya utovu wa nidhamu na klabu zao zao zikaamua kuchukua hatua zinazostahili kwa ajili ya kuwadhibiti.

Ingawa mashabiki wamekuwa wakilalama, bado viongozi wana haki ya kuchukua hatua kwa kuwa kama watatoa nafasi ya vitendo vya nidhamu kuendelea kwa ajili ya kuwafurahisha mashabiki basi watakwama na siku ya mwisho lawama zitaangukia kwao.


Hivyo ni suala la msingi sana kwa viongozi kusimamia suala la nidhamu bila ya hofu ya kitu chochote kwa kuwa tunajua wazi kwamba bila ya nidhamu, basi hakuna mafanikio hata kama timu itakuwa na vipaji vya hali ya juu, bila ya nidhamu, hakuna mafanikio.

Pamoja na yote hayo, bado nataka kusisitiza pia kuhusiana na viongozi wanaokuwa katika timu ambao wanakuwa na tabia ya kujenga chuki kama inatokea wakakosa na wachezaji.


Mara kadhaa tumekuwa tukisikia na wachezaji nao wakilalama kwamba kuondoka kwao katika timu fulani kunahusiana na chuki kati yao na viongozi kadhaa wa timu wanayoondoka.

Lakini kama wadau suala hilo tumekuwa tukilichukulia la kawaida tu, hakuna ambaye anataka kuhoji na kujua kama kweli viongozi wanaweza kuwa tatizo kwa kuingiza masuala ya kibinadamu, yaani yasiyohusu umuhimu katika timu na kuyageuza maamuzi ndani ya timu.

Mimi ninaamini kwamba katika timu mbalimbali za Ligi Kuu Bara, kuna viongozi wenye tabia hizo ambao wamekuwa wakijenga chuki kati yao na wachezaji na mwisho wakafanya vitu Fulani bila ya kujadili wanachoamua kitaiathiri klabu.

Badala yake wanaangalia watafurahisha vipi nafasi zao kwa kuona mchezaji au wachezaji fulani wanaondolewa katika timu ikiwa ni sehemu ya wao kuwaonyesha wachezaji hao wana nguvu kiasi gani au jeuri yao ikoje!

Kwenye kundi la watu wengi lazima kutakuwa na hali ya kutofautiana, hii inatokea shuleni, maofisini halikadhalika katika timu. Kikubwa ambacho kinaweza kuwaendesha watu ni vumilifu, kila mmoja kuvumilia sehemu mwenzake alipopungukiwa.

Pia bado ni busara kukubali kusamehe kwa kuwa binadamu hatujakamilika na ikiwezekana lazima kuna kukoseana, viongozi na wachezaji wakubali kusameheana kwa maana ya kukubali ubindamu lakini pia kuangalia faida ya wanachokitumikia kinatakiwa kifanikiwe vipi.
Ndiyo maana nasisitiza, wale wenye tabia ya kujenga chuki na hasa viongozi kwa kuwa tu wanajua wana ‘mpini’ si sahihi, lazima watafakari mara mbili. Kwamba kama viongozi, wanachotakiwa kufanya zaidi ni kwa faida ya timu na kwa faida ya nafsi zao.

Timu lazima ziendeshwe na watu, ili mambo yaendelee watu lazima wapishane mawazo kwa maana ya kutofautiana na mwisho watakaa na kujadili hadi kupata jibu moja ambalo litafanyiwa kazi ili kusukuma maendeleo ya timu.

Kama suala la wachezaji watovu wa nidhamu litaendelea kushughulikiwa kwa faida ya timu, halafu hili la viongozi wenye chuki na gubu likaachwa, basi itakuwa na kutwanga maji katika kinu.

Lazima mkubali, kwamba kama binadamu lazima mtakosea. Hivyo vizuri kila mmoja kukubali makosa ya mwenzake, msahihishane na muombane radhi lakini mwisho, kila mmoja lazima akubali kwamba kama timu lazima maslahi ya timu yawe mbele kuliko yale binafsi, hii ndiyo maana ya professional.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic