July 10, 2013





 Na Saleh Ally
Mchezo wa soka nchini unaathiriwa na mambo mengi sana, lakini bahati mbaya wengi wamekuwa wakiyafanya mambo hayo kama hadithi za kupita bila ya kuyashughulikia.

Soka ni mchezo wenye mashabiki wengi zaidi nchini na duniani kote, ni biashara kubwa na inayoweza kutoa ajira kwa wingi kwa vijana na Watanzania wengine, tena wakapata mishahara bora kabisa na kuepusha mambo mengi kama vijana kuwa vibaka au watumiaji madawa ya kulevya.

Ndani ya soka kuna wigo mpana sana, utapata ajira, fedha pamoja na afya. Ndiyo maana nataka kuzungumzia matatizo yanayoonekana kama kitu cha kawaida na kuachwa yapite hivihivi.

Kila timu inayoshiriki Ligi Kuu Bara, sasa ipo kwenye mchakato wa kujenga kikosi imara na moja ya mikakati mikubwa ni usajili.

Usajili una wigo mpana sana, lakini tatizo kubwa ambalo limekuwa likiyumbisha mambo mengi sana ni ubinafsi wa watu ambao zaidi wanaangalia nafsi zao kuliko hali halisi na kwa kifupi mambo mengi hayaendi kitaalamu.

Matumbo:
Wapo watu ndani ya klabu nyingi nchini ambao wamekuwa wakishiriki katika zoezi la usajili kama wahusika na wao zaidi wanaangalia watapata kiasi gani ili wafaidishe matumbo yao kuliko klabu itafaidika na kipi.

Mwaka 2004 nikiwa nchini Rwanda kuripoti michuano ya Kombe la Kagame, kulitokea mgogoro mkubwa katika Klabu ya Rayon Sports ambayo haikuwa ikishiriki kwa kuwa wenyeji waliwakilishwa na APR na Kiyovu.

Tatizo kubwa lilikuwa ni kocha mmoja raia wa DR Congo kulaumiwa kuwa alikuwa akichukua fedha kwenye usajili wa wachezaji na wengine walilia alikuwa akikata hadi mishahara yao.

Mambo hayakuisha kimyakimya, mwishowe kocha huyo alitupiwa virago na wengine waliokuwa wakishirikiana naye wakaonywa kwa kuwa mtandao ulikuwa mkubwa.


Hata hapa nyumbani mtandao ni mkubwa na hasa katika klabu za Yanga na Simba. Wapo watu ambao siku zote ninaeleza hutaka kuonyesha wana mapenzi makubwa na klabu hizo, kumbe wanajua wanafaidika vipi, maana yake hawazipendi bure!

Watu hawa husajili wachezaji kwa lengo la kupata ‘ten percent’, hapa kwa kuwa wanaangalia zaidi maslahi yao, basi kama mchezaji bora atagoma kuwapa ‘kitu kidogo’, halafu yule asiye bora anakubali, watamchukua.

Utaona hapa klabu ndiyo imeharibikiwa kwa kuwa itakosa mchezaji bora na kupata bora mchezaji ili watu washibishe matumbo yao. Haya mambo yanafanyika na wahusika wanajua.

Watoto wa mjomba:
Nimetumia jina la ‘mtoto wa mjomba’, lakini inawezekana akawa wa shangazi, nyumba ndogo na vinginevyo. Ufafanuzi ni kwamba kuna ambao wanahusika na usajili huangalia nafsi zao na si faida kwa timu.

Kwa kuwa mtu fulani amepewa nafasi katika kamati ya usajili au ana sauti kwa kuwa yupo karibu na mwenyekiti au katibu wa Yanga au Simba, basi anapiga debe na kutoa nafasi ya mtoto wa ndugu yake kufanyiwa majaribio.

Halafu anakwenda kwa kocha anayejua ndiye anatakiwa kupitisha ubora wa mchezaji na kumueleza anahitaji msaada wake. Siku ya mwisho mtoto wa mjomba anapita na kupata nafasi ya kuichezea Simba, Yanga au timu nyingine, hatimaye anakuwa mtu wa benchi.
Hili jambo limekuwa likionekana ni kama stori ya kawaida na mambo yanaendelea kutokea kila kukicha, hasa katika kipindi kama hiki cha usajili.
Kweli klabu ndiyo inayoumia na wanaofaidika ni hao watu wachache bila ya kujua madhara ya baadaye kwa klabu ambayo inakuwa imetoa fedha nyingi halafu inakuwa na kikosi dhaifu.

Kwa nini kikosi ni dhaifu? Kwa kuwa watu fulani wamepata fedha, wamekula au wamewafaidisha ndugu zao! 

Vitu hivi viwili ni sehemu ya sumu inayofanya soka ya Tanzania endelee kudumaa na wachache hao wakigeuza kipindi cha usajili ni mtaji kwao.
Makocha mfano Abdallah Kibadeni kwa Simba, Ernie Brandts kwa Yanga ambao ndiyo wataalamu, wapewe nafasi ya kufanya kazi yao kwa faida ya klabu na vikosi vyao. Kuna kila sababu ya kusema wao ndiyo wahusika wakuu, ingawa wanaweza kushauriwa, sawa, lakini si kuelekezwa.

Kwa wale ambao wanaangalia nafsi na matumbo yao, lazima wakumbuke kwamba mashirika mengi ya umma yalikufa kwa kuwa watu wengi walifanya kama wanavyofanya wao sasa. Hivyo vizuri wakawa waungwana na kufanya kazi kwa uaminifu na kufuata weledi.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic