July 12, 2013



*Aeleza Yanga walivyomfuata, azungumzia nguvu ligi kuu

Na Saleh Ally
Mshambuliaji nyota wa Vital’O ya Burundi, Hamis Tambwe ametua nchini juzi Jumatano tayari kumalizana na Simba ili aichezee katika msimu mpya wa 2013/14.

Tambwe raia wa Burundi na mshambuliaji tegemeo wa timu ya taifa ya nchini hiyo, Intamba Murugamba ametua nchini kuzungumza na Simba ikiwa ni siku chache baada ya kuisaidia Vital’O kubeba Kombe la Kagame katika michuano iliyofanyika nchini Sudan.


Katika michuano hiyo, Vital’O ilifanikiwa kufika fainali na kucheza dhidi ya APR ya Rwanda katika mechi iliyokuwa na upinzani mkubwa kwa maana ya nchi hizo zina utani wa jadi kisoka.

Pamoja na upinzani huo, Tambwe ambaye ni nahodha wa Vital’O aliiongoza timu hiyo kuibuka na ushindi wa mabao 2-0, yeye akiwa amepachika moja na Deo Ndayishimiye akapachika la pili.

Katika michuano hiyo, Tambwe ameshinda vitu vitatu muhimu na huenda ikawa ni moja ya rekodi chache za michuano hiyo ya Kombe la Kagame tokea ianzishwe.
Kwanza ameisaidia Vital’O kubeba Kombe la Kagame, pili ameibuka mfungaji bora na ametangazwa kuwa mchezaji bora wa michuano hiyo.
 
TAMBWE NA SALEH ALLY...
Mshambuliaji huyo amefanikiwa kushinda makombe matatu katika michuano hiyo, kitu ambacho kinampa jeuri ya kusisitiza kwamba hajaja Simba kujaribiwa.

Mara baada ya kutua kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa sita usiku, Championi lilifanya naye mahojiano na moja kwa moja akaeleza kuhusiana na ujio wake.

Salehjembe: Utafanya majaribio na Simba muda gani?
Tambwe: Naweza kusema sijaja hapa kufanya majaribio, Simba wameona kazi yangu. Hivyo, nataka kuzungumza nao na kujua tutafikia vipi.


Salehjembe: Kusaini ni nia na kuipenda sehemu, nia ya kusajili kwako ni vipi au zaidi unaangalia maslahi.
Tambwe: Maslahi ndiyo maisha, lakini ninavutiwa na Simba ndiyo maana nikakubali kuja. Nina ofa nyingi tu.


Salehjembe: Labda kutoka katika timu zipi?
Tambwe: Kwa sasa siwezi kusema, ngoja nimalizane na Simba kwanza ili nijue.

Salehjembe: Kuna taarifa Yanga pia walikufuata?
Tambwe: Kweli, nilizungumza nao na wakataka niwatumie CV (wasifu) wangu na nikafanya hivyo.

Salehjembe: Vipi sasa umekuja Simba, wakati umetuma CV?
Tambwe: Simba walianza kabla ya Yanga na nimekuambia ninavutiwa nao.

Salehjembe: Uliwahi kukutana nao ukiwa na Vital’O?
Tambwe: Nakumbuka ilikuwa hapa Dar es Salaam katika michuano ya Kagame na mechi iliisha kwa sare ya bila kufungana.

Salehjembe: Je, unaifuatilia ligi ya soka ya Tanzania?
Tambwe: Ninafanya hivyo, ligi ya hapa wachezaji wanatumia nguvu sana tofauti na Burundi, kule kuna ufundi mwingi sana.

Salehjembe: Hauna mwili mkubwa, utaweza kupambana na umeshasema ligi ya hapa ni nguvu zaidi?
Tambwe: Nimeamua kuja hapa, najua nitaweza hata kama itakuwa ni baada ya kipindi fulani.

Salehjembe: Ukiachana na mabao yako sita yaliyokupa ufungaji bora, taarifa zinasema umekuwa mfungaji bora Burundi kwa misimu miwili mfululizo?
Tambwe: Ni msimu huu ndiyo nimekuwa mfungaji bora, nilifunga mabao 18, lakini nilikuwa na mengine mawili katika michuano ya Rais Nkurunzinza. Jumla nimefunga mabao 20 msimu uliopita.

Salehjembe: Kabla ya hapo pia ulikuwa mfungaji bora?
Tambwe: Hapana nilishika nafasi ya pili, nilifunga mabao 16 wakati mfungaji bora akawa na 18 pia.

Salehjembe: Lini unakutana na viongozi wa Simba?
Tambwe: Kweli sijajua, mimi nawasikiliza wao ambao ni wenyeji.

Salehjembe: Karibu Dar es Salaam.
Tambwe: Nashukuru sana.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic