September 25, 2013



Straika Simba, Amissi Tambwe, amesema sasa anafurahia maisha ndani ya kikosi hicho, lakini akatoa siri nzito kuwa ilisalia nukta moja atue katika Klabu ya Yanga ambayo ni wapinzani wakubwa wa Wekundu hao.


Tambwe raia wa Burundi, amesema kati ya klabu mbili za Simba na Yanga, Yanga ndiyo walikuwa wa kwanza kuanza kuzungumza naye.

Alisema walifika kwake wakiwa na lengo kubwa la kutaka kumsainisha mkataba lakini alipowaambia wasubiri mpaka amalize mechi kati ya nchi yake dhidi ya Sudan, hawakurudi tena.

Tambwe amesema mara baada ya kumalizika kwa mchezo huo, mabosi hao wa Yanga hawakuonyesha tena kuwasiliana naye kabla ya Simba kuingilia kati kupitia aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa Wekundu hao, Geoffrey Nyange ‘Kaburu’, aliyefanikisha usajili wake na timu hiyo.

“Mpaka sasa nadhani ningekuwa Yanga kwa kuwa wao ndiyo waliotangulia kunifuata na kuzungumza na mimi wakitaka kunisajili, nikawaambia wasubiri lakini baadaye hawakuja tena, niliwasubiri lakini wakawa kimya, hapo ndipo Simba walipopata nafasi,” alisema Tambwe ambaye sasa ndiye kinara katika msimamo wa ufungaji akiwa na mabao sita.

“Yanga walifikia pazuri na hata katika mazungumzo yangu ya mwisho na bosi wao, alikubali hata kwenda Vital’O kuvunja mkataba wangu, lakini ukimya wao ukawapa nafasi Simba, waliokuja kupitia Kaburu na kila kitu kilikwenda kwa haraka tofauti na Yanga,” alisema.

Tambwe amesajiliwa na Simba msimu huu akitokea Vital’O ya Burundi. Kabla ya kujiunga na Wekundu hao, alifanikiwa kuipa klabu hiyo ubingwa wa Kombe la Kagame huku yeye akiwa mfungaji bora katika michuano hiyo iliyofanyika Sudan, mwaka huu.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic