October 9, 2013





HII ni kali na ya aina yake, kila pasi ya mwisho na bao atakalofunga kiungo mshambuliaji wa Yanga, Mrisho Khalfan Ngassa, litanunuliwa.

Milionea Davis Mosha aliyewahi kuwa makamu mwenyekiti wa Yanga, ameamua kutangaza ofa hiyo kwa Ngassa kila atakapofunga akiichezea timu hiyo.


Taarifa za uhakika zinaeleza kuwa, Mosha tayari amemueleza Ngassa kuhusiana na ofa yake hiyo.

“Unajua katika mechi mbili dhidi ya Ruvu Shooting na Mtibwa Sugar, Ngassa amefunga bao moja na kutoa pasi mbili. Davis ameshalipia zote,” kilieleza chanzo na kufafanua zaidi:

“Bao moja amemlipa shilingi milioni moja na pasi pia amelipa, sijui ni kiasi gani lakini nimeambiwa ni shilingi laki tano.”

Taarifa zaidi zimeeleza kuwa, pamoja na Mosha kununua mabao hayo, pia amemtaka Ngassa kuhakikisha anasaidia kupatikana kwa mabao mengine katika timu hiyo, akisisitiza ataendelea kununua pasi zilizozaa mabao.

“Unajua Mosha alichangia kwa kiasi kikubwa kumrudisha Ngassa Yanga, wakati akiwa Azam na hata Simba kwa kumtaka akipata nafasi ya kutakiwa kurudi Yanga asifanye makosa,” alisema mmoja wa watu wa karibu na Mosha.

 Ngassa, ambaye alikiri kuwepo kwa taarifa hizo huku akiongeza zaidi kuwa, hata bao alilolifunga juzi dhidi ya Mtibwa, alimpa zawadi Mosha ikiwa ni ishara ya kutambua mchango wake.

“Ni kweli hizo taarifa ni sahihi, natambua sana mchango wa Mosha kwangu, tunazungumza mengi lakini naweza kusema anachangia kwa kiasi kikubwa mafanikio ninayoyapata katika klabu yangu ya Yanga.

“Kila ninapofunga au kutoa pasi ananipa fedha, hiyo ndiyo sababu inayonifanya nijitume kwa kufanya mazoezi mara mbili mpaka tatu kwa siku ili niwe fiti,” alisema Ngassa.

Kama vile haitoshi, Ngassa juzi alivaa kiatu cha kisasa aina ya Nike Hypervenom Phantom (FG), kinachotumiwa na kutangazwa na wachezaji nyota duniani kama Mario Balotelli wa AC Milan, Wayne Rooney (Man United), Gonzalo Higuain (Napoli) na Neymar wa FC Barcelona.

Kiatu hicho ambacho ni toleo jipya la Nike mwaka 2013, Ngassa alikipata kutoka Uingereza ikiwa ni zawadi kutoka kwa rafiki yake.
“Kweli ndicho nilivaa katika mechi dhidi ya Mtibwa Sugar, rafiki yangu alisafiri kwenda Uingereza nikamuomba aniletee,” alisema Ngassa.

SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic