October 9, 2013


Rhys Torrington

 
Na Saleh Ally
Gumzo Azam TV limekuwa likipanda kila siku, taarifa za kuanza kwake na mgogoro wake na Yanga kuhusiana na kuonyesha Ligi Kuu Bara pia ni mambo yanayochukua nafasi kubwa miongoni mwa mashabiki wa michezo, hasa soka.


Championi Jumatano liliamua kupiga hodi hadi kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Azam Media, Rhys Torrington ambaye anaelezea mambo kadhaa kuhusiana na mgogoro huo, pia mipango kamili ya Azam TV.

Torrington, raia wa Uingereza, anasema mgogoro wa Yanga anauona unakwenda kisiasa zaidi, kitu ambacho anaona si sahihi, akitolea mfano suala la watu waliojiita mashabiki wa Yanga kutaka kuwashambulia wapigapicha wa Azam TV wakiwazuia kuonyesha ‘live’ wakati Yanga ikicheza na Mtibwa, Jumapili.


Mgogoro na Yanga:
Kweli si kitu kikubwa sana, lakini limekuwa jambo ambalo linakuzwa sana na kuna wakati nafikiri ule upinzani mkubwa kati ya Yanga na Azam FC katika soka ndiyo unaosababisha mambo haya.

Lakini kitu kizuri sisi tumefuata utaratibu unaotakiwa na tumeingia mikataba sahihi na tuna haki ya kufanya kazi zetu. Ila kwa usalama wa watu wetu, tuliamua kusitisha kuonyesha mpira.

Angalia, katika mechi ya kwanza ilikuwa Simba na Ruvu Shooting, tulionyesha kipindi cha pili tu. Hii ilitokana na makosa ya kibinadamu, kuna mtu alisahau kuchomeka waya, hivyo hatukuwa hewani.

Mechi ya Yanga na Mtibwa Sugar, tulijipanga kuanzia kipindi cha kwanza, ikashindikana kutokana na hizo vurugu hadi askari walipoingia.

Kiungwana kabisa nahisi hao ni watu wanaojidai mashabiki wa Yanga. Siamini mashabiki wa kweli wanaweza kufanya hivyo na ingekuwa vizuri kama uongozi wa Yanga ungekemea ili kuepuka kuchafuliwa.



Lini mtaanza?
Kwa sasa tumeingia mkataba wa kirafiki na TBC1, itakuwa kila Jumamosi na Jumapili na wao wataendelea kuonyesha hadi mwisho wa mzunguko wa kwanza, baada ya hapo kila kitu kitarudi kwetu.

Ila sisi tutaanza rasmi Novemba Mosi, itakuwa kabla ya mzunguko wa kwanza kuisha. Maana yake sisi na TBC1 wote tutaonyesha. Halafu watatuachia wenyewe baada ya kuanza mzunguko wa pili kama nilivyosema.

Tayari kuna watu wameshaanza mazoezi ya mambo lukuki hapa, tuna wataalamu kutoka Ujerumani na Afrika Kusini wanaotoa mafunzo kwa watu wetu. Mfano tuna magari mawili ya OB Van, dogo litatumika kwa viwanja vidogo na kubwa Uwanja wa Taifa.

Yote hayo yanahitaji utaalamu na si kitu kidogo, hivyo wataalamu hao wanaendelea kufanya kazi kuhakikisha mambo yako sawa.

Visimbuzi:
Kweli tutatumia visimbuzi ambavyo vinatarajiwa kuwa na chaneli takribani 50, mfano Azam1 itaonekana na lugha ni Kiswahili, chaneli hii ndiyo itakayoonyesha soka na zaidi ni Ligi Kuu Tanzania Bara.

Lakini Azam2 itakuwa ni Kiingereza, kawaida tutatumia maandishi kama yale ya Zuku au Dstv, ukilipa kwa mara ya kwanza kunakuwa na chaji kidogo ya fundi.

Kutakuwa na filamu za sehemu mbalimbali duniani pamoja na zile za Kitanzania. Lakini kuna chaneli mbalimbali za hapa nyumbani kama Mlimani TV, Clouds TV na TBC1.

ITV vipi?
Hawa ITV wamekataa katakata kuingia katika kisimbuzi chetu na kutupa haki ili waonekane kama wengine. Hivyo hatutakuwa nao lakini tunaamini mambo yataendelea vizuri tu.

Bei ya Visimbuzi:
Kweli sasa itakuwa ni siri, ila nakuhakikishia itakuwa ni ile anayoweza kuihimili mwananchi yeyote. Visimbuzi vyetu havina madaraja ya matajiri na masikini, bei itakuwa ni moja ili kila mmoja aweze kununua.

Kuna mawakala 200 kwa nchi nzima ambao watafanya kazi ya kuuza visimbuzi vyetu na hii ni kutaka kuhakikisha kila mtu anapata.

 Visimbuzi vyetu ni kati ya vilivyo bora kabisa, vinatumia mfumo wa HD na unaweza kurekodi kwa kutumia USB Flash.
Mwisho si Tanzania:

Tunataka kuanza na nyumbani kwanza na baada ya hapo tutaendelea kunajitanua hatua kwa hatua, tutaanzia na Uganda na baadaye Kenya na ikiwezekana hadi mwisho wa mwaka huu tutakuwa tumeingia sehemu hizi mbili.

Baada ya hapo, ninaamini itakuwa ni mwakani tutavuka taratibu hadi Rwanda, Burundi na ikiwezekana Malawi na tunaweza kutulia na kujiimarisha zaidi kabla ya kwenda Afrika Magharibi, hii ni mipango ya hapo baadaye.
Fin.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic