October 7, 2013


Na Saleh Ally
 Uongozi wa Simba umeanza juhudi za kusaka mshambuliaji mwingine raia wa Burundi ambaye umepewa taarifa zake kwamba ni hatari katika upachikaji wa mabao.


Kama Simba itampata Mrundi huyo ambaye bado hajawekwa wazi, basi mara moja itaachana na Mganda, Moses Oloya, ili kuongeza nguvu ya upachikaji mabao katika safu ya ushambuliaji ya kikosi cha Abdallah Kibadeni.


Mrundi Amissi Tambwe anaongoza kwa kupachika mabao kwenye Ligi Kuu Bara na sasa anayo nane baada ya kucheza mechi saba.

Mfungaji bora wa msimu uliopita alikuwa ni Kipre Tchetche wa Azam, raia wa Ivory Coast, sasa dalili zinaonyesha huenda mfungaji bora atakuwa ni Mrundi au Mtanzania.

Kabla ya raia huyo wa Ivory Coast, Wakenya na Waganda wamekuwa wakiwasumbua Wabongo kwa ufungaji. Huenda mabadiliko yakatokea lakini sasa ushindani ni dhidi ya Warundi.

Wakati Tambwe anaongoza akiwa na mabao nane, anayemfuatia ni Themi Felix wa Kagera Sugar mwenye mabao manne.

Baada ya hapo, anafuatia Mrundi mwingine, Didier Kavumbagu wa Yanga mwenye mabao matatu, sawa na Watanzania wengine Jerry Tegete (Yanga), Haruna Chanongo (Simba), Paul Nonga (Mbeya City), Peter Michael (Prisons) na Bakari Kondo (Ruvu Shooting).

Katika soka chochote kinaweza kubadilika na mwenye mabao nane anaweza akafikiwa au vinginevyo, lakini mwendo wa Tambwe kama atakuwa na afya njema, basi kuna kazi kwa kuwa ana mambo kadhaa ambayo mshambuliaji anapaswa kuwa nayo.

Pamoja na kasi, lakini hesabu za kuwahi pasi, yaani sehemu sahihi katika wakati mwafaka ni kubwa sana. Angalia mshambuliaji mwingine wa Simba anapopiga shuti kwenye lango pinzani. Mara nyingi Tambwe hufuatilia.

‘Urafiki wake na kipa’ ni mara kwa mara na anatumia mfumo wa “binadamu na makosa”.   Mara nyingi hachezi mbali na kipa hasa kunapokuwa na purukushani langoni, anajua linaweza kufanyika kosa naye akaukwamisha mpira wavuni.

Tatizo kubwa alilonalo ni nguvu, mwenyewe amekubali kwamba anahitaji muda kuzoea uchezaji wa nguvu wa Ligi Kuu Bara.

Lakini wako wenye nguvu kama Felix, ambapo uwezo wake wa kupambana na mabeki ni mkubwa. Pia anapiga mashuti ingawa anapungukiwa kasi kama ile ya Tambwe.

Kavumbagu ni kati ya washambuliaji wasumbufu sana kwa mabeki na huwa  hachoki.  Kweli ni ‘roho ya paka’ lakini anakosa kasi ya kutosha. Katika mashuti si mzuri sana lakini pia ana uwezo mkubwa wa kutoa pasi za mwisho kwa wenzake.

Nonga pia ni kati ya washambuliaji wenye nguvu na mashuti, mzuri wa mipira ya juu kama ilivyo kwa Kavumbagu. Anaweza kuwa mmoja wa washambuliaji bora zaidi kama atapata uzoefu. Lakini ni tatizo kubwa la mabeki na mara nyingi anajitahidi kuwa katika sehemu husika.

Chanongo yeye ni kiungo, anapiga mashuti makali, ana kasi lakini bado hana uwezo mzuri wa kulenga goli. Mabao aliyofunga yanaonyesha atakuwa tishio baadaye, tayari Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen, ameliona hilo, amekuwa akimchezesha namba kumi katika kikosi chake badala ya pembeni.
Ukiangalia namna washambuliaji hao wanavyoongoza msimamo wa wapachika mabao, inaonyesha wazi ushindani utakuwa mkubwa na wapo watakaoondoka na kuachwa nyuma huku wapya wakipanda nafasi za juu, ambao sasa wana bao moja au mawili tu.

Tambwe
KASI     89%
PASI   82%
TAIMINGI 95%
MASHUTI 75%
NGUVU 60%

Felix
KASI  78%
PASI  79%
TAIMINGI 80%
MASHUTI 90%
NGUVU 85%

Kavumbagu
KASI 78%
PASI 75%
TAIMINGI 80%
MASHUTI 85%
NGUVU 80%

Chanongo
KASI 91%
PASI 76%
TAIMINGI 68%
MASHUTI 80%
NGUVU 82%

Tegete
KASI 80%
PASI 70%
TAIMINGI 93%
MASHUTI 75%
NGUVU 75%
Fin.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic