Na
Saleh Ally
HATA
kabla ya kutua jijini Dar es Salaam, hadi leo kocha mpya wa Simba, Zdravko Logarusic mwenye umri wa miaka 51 ni gumzo katika mitaa mbalimbali ya
Jiji la Nairobi nchini Kenya.
Logarusic
ameishi nchini Kenya akiwa kocha wa Gor Mahia moja ya timu kubwa na kongwe
nchini humo na alifanya kazi yake kwa mafanikio makubwa.
Kocha
huyo raia wa Croatia, ndiye aliinua Gor Mahia iliyokuwa imepoteza mwelekeo,
akiwa anasaidiwa na nyota wa zamani wa timu hiyo na timu ya taifa ya Kenya,
Harambee Stars, Bobby Ogola walifanikiwa kuipa Gor makombe mawili.
Gor ilishika nafasi ya pili baada ya kutoka sare ya bao 1-1 katika mechi ya mwisho dhidi Thika, kama wangeshinda, wangetwaa ubingwa.
Gumzo la Logarusic katika sehemu mbalimbali wanazozungumzia soka katika Jiji la Nairobi ni vitu viwili vikubwa, uwezo wake wa kazi na ukorofi, haohofii, hajali na ‘ukimzingua’ basi ‘anachukua zake time’.
Hakuna ambaye amethubutu kusema kocha huyo ana uwezo mdogo wa kazi, lakini hakuna aliyesahau kusema kocha huyo ni mkorofi na mbishi kupindukia.
Mfano hata kuondoka kwake Gor ilikuwa ni kama suala hilo halitokei, kwani aliamua kutorudi tu baada ya kwenda likizo huku akitoa visingizio lukuki.
Logarusic aliachishwa kazi akiwa kwao Croatia baada ya kupitisha siku alizotakiwa awe amerejea Kenya, Katibu Mkuu wa Gor, George Bwana ndiye alimuandikia barua ya kumueleza ameachishwa kazi ikiwa ni siku moja baada ya msaidizi wake, Ogolla kupewa timu na kuiongoza kushinda mabao 2-1 dhidi ya Karuturi na kupewa ukaimu kocha mkuu.
Pamoja na kutimuliwa, Logarusic alizungumza na waandishi na kuwaeleza wala hajuti hata kidogo na mashabiki wengi wa Gor walionekana kutofurahia.
MAMBO 10 YA LOGARUSIC USIYOYAJUA:
I:- Ana
Diploma tatu tofauti zinazohusiana na masuala ya soka, ana vibali vya
kufundisha kutoka katika nchi za Croatia na Australia, pia ana leseni ya Uefa
Pro ambayo ni ya juu.
II:-
Aliingia katika gogoro kubwa na Klabu ya King Faisal ya Ghana baada ya kuiacha
katikati ya msimu, juhudi za kumzuia asiondoke zilishindikana, uongozi wa klabu
ukamshitaki polisi.
III:-
Logarusic aliisaidia King Faisal kuepuka kuteremka daraja katika msimu wa
2009/2010, alipoondoka akajiunga na Ashanti Gold iliyokuwa inashiriki Ligi Kuu
ya Ghana na msimu wa 2010-11 akaisaidia kushika nafasi ya pili nyuma ya
mabingwa Berekum Chelsea.
IV:- Msimu
wa 2011-12 ulikuwa mbaya kwake zaidi, ilifikia timu yake ikashika nafasi ya 12,
nafasi chache kabla kuingia katika dimbwi la kuteremka daraja.
V:-
Baada ya vuta nikuvute, Logarusic alikubali kulipa kitita cha dola 45,000 (Sh
milioni 70), ilimradi tu aondoke King Faisal na kutua Gor Mahia.
VI:- Logarusic
amefanya kazi ya ukocha katika mabara manne ambayo ni Ulaya, Australia, Amerika
Kaskazini na Afrika.
VII:-
Amefanya kazi ya ukocha kwa miaka 20, katika mabara manne aliyofanya kazi,
Logarusic ameziongoza timu mbalimbali katika mechi za mashindano zaidi ya 1,000.
VIII:-
Ndiye kocha pekee wa Kenya ambaye mashabiki wamewahi kubusu kiatu chake
wakionyesha wanaikubali kazi yake ya uhakika.
IX:-
Mtanzania pekee ambaye amewahi kufundishwa na Logarusic ni Ivo Mapunda ambaye
alisajiliwa naye akitokea Bandari ya Kenya na kutua Gor.
X:-
Mchezaji pekee aliyewahi kuzichezea Yanga na Simba na amewahi kufundishwa na
kocha huyo ni Moses Odhiambo ambaye pia amefanya naye kazi wakiwa Gor.
0 COMMENTS:
Post a Comment