November 25, 2013





Kamwe hauwezi kusikia Manchester United wamefanya usajili kwa kuwa wamesikia Arsenal wamefanya hivyo, hali kadhalika kwa Arsenal.

Kila timu inafanya mambo yake kwa kuangalia mipango yake kamili, kwamba inahitaji wachezaji katika nafasi ipi na nini cha kufanya kwa ajili ya faida ya timu.

Benchi la ufundi lina nafasi kubwa ya kuangalia wachezaji wa aina gani wahitajika wakati msimu unapoanza na mzunguko wa kwanza unapomalizika kama sasa ilivyo kwa Ligi Kuu Bara lazima kutakuwa na mabadiliko.
Benchi la ufundi safari hii linakuwa na nafasi ya kutoa tena mapendekezo yake katika mechi zilizobaki kuwa cha kufanya ni kitu gani na kama usajili wachezaji wanaotakiwa ni wa aina na nafasi zipi.
Lakini hapa nyumbani inaonekana mambo mengi yanakwenda tofauti na inawezekana mabenchi ya ufundi hayana nguvu kubwa na badala yake usajili unaangalia zaidi mapendekezo binafsi na hasa ya wanaotoa fedha.
Wako wanaotoa fedha kwa ajili ya usajili katika klabu za Simba na YAnga, wanasikilizwa kwa kuwa wanaonekana ni msaada mkubwa sana.
Wakati mwingine wanafikia kusajili wachezaji ambao walikuwa hawahitajiki na benchi la ufundi, halafu mwisho wanajikuta wakiingia katika kundi la kulazimisha wacheze na kumpa kocha wakati mgumu.
Wanalazimisha mchezaji waliomsajili acheze kwa kuwa wanaona walitumia fedha zao kwa ajili ya kumsajili, lakini benchi la ufundi halikumhitaji, mwisho hapo unaanza ugomvi kati ya watoa fedha na kocha, anaanzishiwa ‘zengwe’, kwamba uwezo wake mdogo.
Mifano iko mingi kwa wachezaji kibao walio Yanga na Simba nah ii inatokana na ule usajili wa kumrithisha mtu mmoja ambaye ana uwezo wa kutoa fedha za usajili au mshahara kumlipa mchezaji fulani.
Pia kumekuwa na tabia hizi klabu kuangalia upande mmoja imesajili wachezaji wangapi, basi upande mwingine pia kutaka kujibu mapigo huku mambo yakionekana kwenda kisiasa zaidi.
Angalia mshambuliaji wa Mtibwa Sugar, Hussein Javu, anapoteza muda wake mwingi akiwa benchi lakini juzi hapa Simba imesajili wachezaji huku kukiwa na taarifa hayakuwa mapendekezo ya benchi la ufundi.
Dunia inakwenda kasi sana katika suala la maendeleo, mambo yako tofauti kabisa katika kipindi hiki. Viongozi wanaofanya usajili au wanaohusika na zoezi hilo wanapaswa kukubali kujifunza na mwisho wabadilike.
Siasa au ushabiki wa kutaka sifa, kama vile Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage kusajili wachezaji subuleni kwake. Hiyo ni dalili ya mambo hayo ninayoyazungumzia, ikifika wachezaji hao wamekwama basi ni tatizo.
Hivyo kuna haja ya kugawanya mambo kitaalamu, yaani kama ni suala la kiufundi, basi mafundi wapewe nafasi waifanye kazi yao badala ya watu wanaohusika na uongozi au wenye fedha zao mfukoni kuingilia tu.
Tunakubaliana na mgawanyo wa kazi kupitia vitengo, kamwe hakuna timu inayoweza kufanikiwa bila mgawanyo wa kazi kama hivi, kipa, mabeki, viungo na washambuliaji. Halafu baada ya hapo wote wanafanya kazi pamoja kupitia hiyo migawanyo.
Maana yake, hata kwenye masuala ya uongozi pia kuna mgawanyo na baada ya hapo kila upande unafanye kazi zake kwa juhudi kama timu ili kusaidia mafanikio ya pamoja kupatikana. Kama itakuwa watu wengine wanajua kila kitu na wanadharau wengine kwa kuwa hawana fedha au vyeo vya juu, basi mtakwama na kila siku mtatafuta wachawi.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic