Makocha wawili wakongwe wa Ligi Kuu
Bara, Mrage Kabange na Mohamed Kampira, wameitabiria mazuri Kilimanjaro Stars,
wakidai itatinga fainali na kutwaa ubingwa wa Chalenji mwaka huu.
Stars iliwafurahisha mashabiki wa soka
nchini baada ya kuifunga Uganda kwa penalti 3-2 na kutinga nusu fainali ya
Chalenji ambapo kesho Jumanne itavaana na Kenya katika michuano michuano hiyo
inayoendelea nchini Kenya.
Kabange ambaye ni Kocha Msaidizi wa
Kagera Sugar, amesema baada ya Stars kuwafungashia virago waliokuwa mabingwa
watetezi, hakuna tena kipingamizi kikubwa kwao.
“Kili imeifunga timu ngumu ukilinganisha
na Kenya ambao ni wenyeji, matumaini makubwa ya kutinga fainali yapo kutokana
na timu yetu kuwa na mchanganyiko wa wachezaji wa rika tofauti ambao nina imani
watapigana kuhakikisha wanarudi na kombe.
“Kwa jinsi kikosi kilivyokomaa
kimashindano huwezi kuwa na hofu yoyote, katika safu ya ushambuliaji Mbwana
Samatta na Thomas Ulimwengu wametengeneza kombinesheni ya hatari ambayo muda wowote
unaweza kushangilia goli,” alisema Kabange.
Kwa upande wake Kampira ambaye ni Kocha
Mkuu wa Mgambo JKT, alisema kikosi cha Stars kipo katika morali ya ushindi kwa
sasa baada ya kuitoa Uganda.
“Nawaomba
Watanzania wawe na imani na timu yao kwa kuwa wachezaji wote walioko Kenya wanajua
wanachofanya na wanatambua wadau na mashabiki wa soka wako nyuma yao na
wanahitaji ushindi katika mchezo unaofuata,” alisema Kampira.







0 COMMENTS:
Post a Comment