December 18, 2013





Na Saleh Ally
EMMANUEL Arnold Okwi amesaini mkataba wa miaka miwili na nusu kuichezea Yanga, upande wa Simba wanapinga suala hilo, bado hakijaeleweka vizuri.
 
Wakati Simba wanapinga, tayari Uhamisho wa Kimataifa (ITC) umetua nchini na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linasubiri kidogo tu, halafu litatangaza uhalali wa Okwi kuruhusiwa kuichezea Yanga au la!

Kwa msimu wa pili mfululizo, Simba imeonekana ni ya kupoteza vizuri dhidi ya Yanga na tayari timu hiyo ya Jangwani imesajili wachezaji watatu nyota kutoka Simba ambao walikuwa mahiri na msaada mkubwa kuunda kikosi bora cha Msimbazi.
Okwi, Kelvin Yondani, Mustapha Ally ‘Barthez’ ambaye hayuko kikosi cha kwanza na Juma Kaseja, lakini Simba pia imempoteza kiungo wake bora, Haruna Moshi ‘Boban’, katika mazingira yaliyoonyesha hakukuwa na umakini mkubwa.
Inawezekana Boban alikuwa ana matatizo, lakini hakuna kiongozi wa Simba aliyethubutu kuzungumza hadharani zaidi ya kulalama chinichini, sasa safu ya kiungo inayumba na baadaye ikawa upande wa kipa na viungo wa pembeni.
Kibiashara, timu huwauza wachezaji wake bora si kuwaachia tu! Leo Arsenal haiwezi kumuachia Theo Walcott kizembe, au Man United ikamuacha Wayne Rooney aende eti ni mtovu wa nidhamu au ameshuka kiwango, lazima ipate faida. Lakini Simba inaendelea tu kutoa sadaka! Maana haijapata hata senti.
Yanga wameonyesha wanaelewa umakini wa wachezaji bora na muhimu, wakati Simba walikubali Okwi aondoke bure ikiwa katika kipindi kigumu cha michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, Yanga wamemsajili katika kipindi kama hicho kwa kuwa wanahitaji huduma yake.
Jangwani wanatambua mchango wa Okwi katika michuano ya kimataifa, alionyesha hayo Simba ilipocheza na timu za Algeria na Sudan katika Ligi ya Mabingwa Afrika. Kukosekana kwake dhidi ya Libolo ya Angola, Simba ikawa nyanya na kunyanyaswa.
Yanga wana hesabu nyingi za msingi kuliko Simba? Au Simba wanapuuzia sana mambo kutokana na kutojali? Angalia Yondani, Kaseja na sasa Okwi, hawaoni matunda yao yanakwenda bila faida kusaidia upande mwingine?
Yondani:
Wakati Yanga inaanza mipango ya kumchukua, Simba walikuwa wamelala na mchezaji alisusa kwa madai ya kutoelewana na viongozi, akakimbilia kwao Mwanza na kujificha, hakuna kiongozi aliyejali sana.
Lakini siku Yanga walipofanikiwa kumchukua, Simba wakacharuka na kuanza kudai mambo kadhaa huku wakionyesha Yanga walikuwa ni tatizo.
Mwisho wakashindwa, Yondani akatua Yanga na sasa ni tegemeo katika safu ya ulinzi ya timu hiyo. Kuthibitisha kweli Simba ilipoteza mchezaji bora, ameipa Yanga ubingwa na juzi ameteuliwa kuwa nahodha wa Kilimanjaro Stars.
Kaseja:
Hata kama kuna unazi, lakini hakuna asiyejua Kaseja ni kipa bora hapa nchini. Simba walimuacha akiwa nahodha wa kikosi chao, nahodha wa timu ya taifa, Taifa Stars, na kipa namba moja nchini.
Simba wakasema kiwango chake kimeshuka, lakini zilikuwa siasa tu za kutaka Abel Dhaira apate nafasi ya kudaka, hivyo Kaseja alilazimishwa kuondoka Simba.
Ajabu, Dhaira kadaka nusu msimu, Simba wamesema ameisha, wamemuacha na kusajili makipa wawili kwa gharama nyingine tofauti.
Lakini awali walianza juhudi za kumshawishi Kaseja kurudi, wakawa wamechelewa na Yanga wakawahi, hili pigo lingine.
Barthez:
Alikuwa kipa namba mbili wakati Simba inaichakaza Yanga kwa mabao 5-0, alikuwa kwenye benchi. Yanga ikamsajili bure, Simba haikujali muda wote iliopoteza kumkuza, kitu ambacho timu zinazojua biashara haziwezi kukubali hata kidogo, akaipa Yanga ubingwa wa Kagame.
Okwi:
Blaah, blaah nyingi kuhusu suala hilo, zilikuwa zinatafuta ukingo, sasa wakati umewadia, Okwi amejiunga na Yanga kwa bei chee na siku mbili hizi, Simba wamekuwa wakihaha kuzuia.
Bado hakuna uhakika, inawezekana wakashinda au kushindwa katika hili, lakini mwisho Yanga wameonyesha nia na wepesi wa kutambua ubora.
Kitu kizuri kwa wakati mwafaka, tofauti na Simba ambayo vitu vikiwa vizuri inavihofia. Kila anayekuwa maarufu anakuwa matatizo kwa kuwa viongozi wake wanataka wachezaji waoga au wasiojitambua watakaoelekezwa kila wanachotaka.
Wakati Etoile du Sahel ilionyesha haitalipa fedha hizo ni pale ilipowaambia Simba inataka kumrudisha Okwi, wao wakakataa, tayari jibu lilipatikana.
Lakini leo mchezaji huyo ambaye alilipwa dola 40,000 kuongeza mkataba Simba siku chache kabla ya kujiunga na Etoile, akapokea dola 45,000 za Etoile akisubiri ziada, sasa amelipwa dola 50,000 kujiunga Yanga.
Zaidi ya Sh milioni 200 mkononi mwa Okwi katika kipindi cha msimu mmoja, Simba imepata hasara ya zaidi ya dola 60,000 (fedha za kumuongeza Okwi mkataba, zile zilizotumika kama tiketi na matumizi ya kushughulikia malipo ya Okwi. Kama haitoshi, dola 300,000 (Sh milioni 480) zinaendelea kuwa hadithi!
Wachezaji hao watatu ni wale waliokuwa katika kikosi kilichoifunga Yanga mabao 5-0, maana yake Yanga wameangalia ubora na kuwachukua wote.
Kitu kingine, kati ya hao watatu, wawili walifunga mabao matatu katika ile mechi. Okwi alifunga mawili na Kaseja moja kwa penalti.
Lakini Yondani, Kaseja na Okwi wote ni wachezaji wa timu za taifa pia wa kiwango cha juu, ondoka yao Simba inaonyesha kuwa hakuna mipango wala hesabu sahihi za kulinda vilivyo bora.
Lakini kama Okwi ataichezea Yanga, maana yake Simba haikuwa kibiashara, hakuna mipango sahihi na viongozi wake wamelala!
FIN.




0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic