February 10, 2014


WAKATI fulani nilikuwa nchini Ujerumani, niliishi kwa takribani wiki tatu kwenye mji mdogo tu wa Freiburg ambao ndiyo mji mkubwa zaidi kusini mwa nchi hiyo.


Mji huo una raha moja, pamoja na kwamba si mkubwa kama ilivyo Berlin, Munich, Frankfurt na mingine ambayo nimewahi kutembelea,  una bahati ya kuwa karibu na nchi mbili, Ufaransa na Uswisi. Hivyo inakuwa ni rahisi sana kuzifikia nchi hizo mbili.

Mmoja wa rafiki zangu aliyekuwa anaishi Freiburg, alikuwa na mapenzi makubwa na timu yao ya Freiburg FC ambayo tokea imepanda Bundesliga, hata mara moja haikuwahi kuwa na ndoto hata ya kutwaa ubingwa wa Bundesliga na kucheza Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Ndoto ya timu hiyo na mashabiki wake ni kuhakikisha inabaki kwenye Bundesliga, hivyo mashabiki na wadau kwa ujumla wamekuwa wakifanya kila linalowezekana ili ndoto yao itimie.
Ukimuuliza kwa nini msianze kuwaza kuchukua ubingwa wa Bundesliga, jibu lake: “Mashabiki wa Freiburg FC ni waelewa, wanajua kulazimisha kubeba ubingwa ni sawa na binadamu kung’ang’ania kupaa hewani, haiwezekani kwa kuwa hatuna mabawa. Siku ikifika, basi timu ifanye hivyo na sisi tutaiunga mkono.”
Wanaiunga mkono vipi kwa sasa: “Kwa kuwa tunaona ina uwezo wa kubaki Bundesliga, basi juhudi zetu ni kuiunga mkono kwa kutoa fedha pamoja na kuishangilia uwanjani.”
Unajua wanavyotoa fedha? Ngoja nikuelezee, kwanza ni kuhakikisha wananunua vitu, mfano jezi, vibeba ufunguo na bidhaa nyingine za timu hiyo. Halafu wananunua tiketi za mechi zao kwa wingi ili kuhakikisha haipati hasara.
Lakini ajabu wao pia wanawaunga mkono hata wadhamini wanaoipa sapoti Freiburg FC ili wasijute na kujua walikosea kuidhamini timu hiyo kutoka Kusini mwa Ujerumani.
Kazi yangu si kuhamasisha watu wanunue bidhaa za wadhamini wa timu za ligi kuu, hilo ni chaguo lenu, pia najua hamwezi kununua jezi na vifaa orijino vya Yanga na Simba kwa kuwa hata klabu zenyewe hazina mpango wa kuviuza na wajanja wanaendelea kujifaidisha.
Lakini ninaamini mnaweza kuziunga mkono klabu zenu, kwanza kwa kulipa ada za uanachama kwa ufasaha, lakini pia kuna suala moja, nendeni viwanjani zinapokuwa zinacheza, lipeni viingilio ili timu ziweze kupata faida na kujiendeleza.
Viingilio vyenu kama kutakuwa na udhibiti, vitaweza kusaidia klabu zenu kuwa na uwezo wa kifedha, zinawalipa makocha, wachezaji, wafanyakazi wake, pia zitaweza kujiendesha. Kwani hata klabu za Ligi kuu England, mapato ya milangoni ni kati ya vyanzo vikuu vya mapato.
Mnataka mkae nyumbani, timu zenu zinacheza viwanja vikiwa tupu, halafu mnadai mnazipenda au kuziunga mkono?  Huo ni uongo na kama mapenzi huenda yakawa ni ya rangi na si yale ya dhati.
Angalia namna mechi za Ligi Kuu Bara zilivyo na watu wachache na kadiri siku zinavyosonga mbele, watu wamekuwa wakizidi kupungua viwanjani, hali inayoashiria watu wengi kutojua maana ya kuziunga mkono timu zao.
Si Yanga na Simba tu, hata wale wa Ashanti na timu nyingine zinazotegemea mapato ili kuishi, lazima wajue msaada wao ni muhimu na kukaa kwenye vijiwe na kuzizungumzia huku wengi wakilalama kuhusu kuwa na maendeleo duni bila ya kuzichangia lolote, si sahihi.
Wanaozichangia timu zao angalau wanaweza kuwa na uwezo wa kulaumu, na utaona mashabiki wengi wa timu za mchangani wamekuwa na mapenzi makubwa na timu zao kuliko hata wale wa Simba na Yanga.

Wanakaa barabarani kuchangisha, fedha zikipungua wanafanya kila liwezekanalo kuchangisha hata kuwalipa wachezaji mahiri wanaokodishwa kuzisaidia timu zao. Lakini mashabiki wa timu kongwe wanasubiri kulaumu tu. Hiyo si sahihi, mjipime, halafu badilikeni.










0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic