February 21, 2014


ALLY SALEH 'ALBERTO'

Na Saleh Ally
SIKU chache zilizopita nilikwenda kwenye mazoezi ya Simba kwenye Uwanja wa Kinesi eneo la Shekilango jijini Dar es Salaam. Lengo lilikuwa ni kuangalia kazi za kocha Zdravko Logarusic kwa ajili ya kujifunza.


Mimi si mwalimu wa soka, lakini napenda kujifunza kupitia kila anayejua. Mara nyingi nimekuwa nikifanya hivyo asubuhi, lakini nikaona si vibaya nikienda hata katika mazoezi ya jioni, maana nilielezwa Simba hawafanyi mazoezi asubuhi.

Dakika chache baada ya kuingia kwenye mazoezi ya Simba, kuna baadhi ya mashabiki walianza kunizomea na kutoa maneno makali, kiasi fulani ilinishangaza lakini sikuwa na hofu hata kidogo kwa kuwa nimekuwa sugu na ninapenda kuishi nikijifunza.

Ukikutana na watu wa namna hiyo ni nafasi ya kukuonyesha namna gani Mwenyezi Mungu ameumba watu wa aina tofauti. Waelewa na wasio waelewa, lakini wasiojitambua kwa hali waliyonayo.

Waliokuwa wakitukana matusi ya nguoni walisema hivi: “Nenda kwenu Zanzibar huko, si umewapa Yanga Okwi, sasa wape na Kapombe kabisa ili ufurahi. Kazi yako ya uwakala wa soka siyo hapa, kama unataka wafuate Yanga Bagamoyo ukafanye huo uwakala.”

Maneno yaliyokuwa yakisemwa huku yakiambatana na matusi makali kabisa, yalinishangaza kidogo. Saleh Ally anaweza kuwapa Yanga Okwi? Kivipi? Anaweza kuwapa Kapombe kwa njia ipi? Lakini nikaona haikuwa busara kwangu kuendelea kufikiria wanachosema, badala yake nifuate kilichonipeleka mazoezini.

Wakati nikiwa mwandishi chipukizi, nakumbuka baadhi ya viongozi walikuwa wakiwapanga mashabiki kuzomea waandishi waliowakosoa kila wanapokwenda mazoezini. Hivyo huenda mimi nina ‘zomea proof’ mwilini mwangu. Hilo haliwezi kunipa shida.

Nakumbuka mwaka 2008 wakati nikiwa mwandishi wa gazeti la Mwanaspoti, nilikwenda kwenye mazoezi ya Yanga Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) nikiwa na ‘kijana wangu’, Michael Momburi. Baada ya kufika pale, Kocha Jack Chamangwana aliniita na kutaka kunisaidia, nikaanza kumuuliza maswali, muda wote huo, mashabiki wa Yanga waliendelea kuzomea.

Wakati natoka wapo walioanza kutoa vitisho, hali hiyo ilimtisha Momburi, akazidi kuongeza mwendo. Mimi nikaona haikuwa sahihi, nikasogea hadi kwenye lile kundi na kutaka kujua sababu. Walinieleza hoja zao, nami nikawaambia niko tayari kuzijibu.

Hatua kwa hatua, wakaenda wanapungua, mwisho akabaki mmoja na baadaye wote wakakubali haikuwa sawa kuzomea na wakati naondoka nikapigiwa makofi.

Sijasahau hadi leo si kwa kuwa nilipigiwa makofi, badala yake namna watu wale wazima walivyoshindwa kujenga hoja wakaamini kuzomea na matusi ndiyo picha ya utu wao, lakini nikaamini wanaweza kubadilika kwa kuamini hoja ni nembo ya binadamu anayejitambua.

Katika mazoezi hayo ya siku chache zilizopita, niligeuka kuangalia waliokuwa wakizomea, niligundua hawakuzidi watu watatu, haraka nikaangalia sura zao, nikawa nimepata somo. Naweza kusema niliona ni watu wapenda sifa, wasio na upeo mzuri wa ufafanuzi wa mambo ambao wanaamini kelele nyingi ni sehemu ya kutambulika au kujitambulisha.

Nikaendelea kukaa kimya, lakini baada ya muda kikaibuka kichekesho. Mtu mmoja kati yao aliibuka na kuwaambia mnayemzomea ni Saleh Ally, si Ally Saleh na huyo si wakala kama mnavyofikiri. Baada ya hapo baadhi yao walianza kupunguza maneno.

Hapo ndipo niligundua kwamba waliamini mimi ni Ally Saleh ‘Alberto’ wa Zanzibar, tena kumbe chuki kwake kwa kuwa siku chache zilizopita alihojiwa na Maulid Kitenge wa Radio One na kueleza namna Yanga ilivyokuwa na uhalali wa kumtumia Okwi.

Lakini bado nikajiuliza, hata ingekuwa hivyo yaani ambaye angekuwa ameingia uwanjani pale kweli angekuwa ni Ally Saleh kweli alistahili maneno ya matusi? Huyo shabiki au mashabiki wanaotukana hawajui aliyesababisha yote hayo ni yupi?

Ally Saleh ana haki ya kuzungumzia anachokifahamu, kama mashabiki wangekuwa na busara siku wakimuona, wangeweza kumuita na kuzungumza naye kwa hoja kwa lengo la kujifunza. Kuropoka, kutukana, hakuwezi kuwa ndiyo njia sahihi ya kujua au kufanikisha jambo.

Wewe usiyejua, unatakiwa kujifunza. Kama unamtukana anayeweza kukusaidia kujifunza, basi maneno machafu ndiyo yatabaki kuwa mwonekano wa picha ya jinsi ulivyo.

Na kama unaishi kwa kupata sifa kupitia matusi, basi wewe ni mtu wa ajabu na vizuri ukajitambua. Nani amewahi kujenga au kutengeneza kitu bora kwa kutumia lugha chafu za matusi?

Kama nilivyoeleza awali, hata baada ya kugundua waliokuwa wakinitusi walidhani mimi ni Ally Saleh, sikuhitaji kuombwa radhi. Maisha yangu yote ya utoto nimeishi nikicheza soka katika timu za mchangani na matusi si tatizo kwangu.

Kiasi fulani niliona walikaa kimya baada ya kugundua waliyekuwa wakimshambulia kwa maneno machafu hakuwa waliyekuwa wamemkusudia.

Lakini bado mimi nikawa nimejifuza tena kama nilivyoeleza kuwa napenda kujifunza katika kila jambo.

Kwamba kama tumekuwa tukilalamikia utendaji wa viongozi wa soka kuwa wazembe au wabinafsi, basi kuna kila sababu ya kuwafunza hata mashabiki na wanachama wa klabu zetu kwamba bado wanahitaji kujifunza.

Huenda kujitambua ni jambo zuri, kama unafikia hadi kumshambulia mtu ambaye si sahihi, maana yake wewe ni mtu wa kukurupuka na haufanyi uchunguzi, mambo yako si ya uhakika na unakwenda kwa kupapasa. Sasa kama uko hivyo, kweli utakuwa msaada kwa klabu yako?

Kama wewe unakwenda kwa kubahatisha, unaweza kumsaidia mwingine au kuwa na mawazo ya kuisaidia klabu kujenga kitu cha msingi? Iko haja ya wanachama au mashabiki kujifunza kuwa wanaoweza kujenga hoja za msingi badala ya kukurupuka tu.

Kama tumekuwa tukilia na viongozi wanaoziangusha klabu, basi hata wanachama matatizo wasiojitambua wanaweza kuwa tatizo pia na ukiwajumlisha wao na viongozi tatizo, maana yake ni majanga kwenye klabu na hasa kongwe za Yanga na Simba.

Kwa kuwa ushabiki haunipi shida, bila ya woga ilimradi ninaamini ninachokifanya ni kwa lengo la kujenga, nitaendelea kusifia na kukosoa bila ya woga hata kidogo.
Waandishi wengine walio tayari kutaka kusaidia michezo nchini, wanapaswa kutohofia maneno kama yale ya mashabiki, badala yake wapiganie michezo ya Tanzania.

Tuko nyuma sana, tunaachwa na kila mtu na tukiwa waoga na kuwapa nafasi wanaokurupuka kama wale mashabiki, tutakwama hapa milele, kitu ambacho si sahihi hata kidogo.

Pamoja na hivyo, huu ni wakati mzuri kwa mashabiki wa soka hasa wa Yanga na Simba kutafakari, kipi mnaona sahihi. Kuendelea kuishi kwa kubahatisha na kupata sifa za umaarufu kuwa mnaweza kukurupuka na kutukana au muwe wajenga hoja, mnaochambua mambo ili inapofikia mnataka kumkosoa mtu, basi muwe na uhakika.
Salamu kwenu.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic