February 14, 2014


Na Saleh Ally
HUU ni wakati wa mateso ya moyo kwa mashabiki wa Manchester United. Inawezekana wako watakaokataa kwa hisia lakini hali halisi inaonyesha hivyo. 


Wataendelea kuteseka hadi mambo kadhaa yatakapobadilika ili kuweka mambo sawa.

Mabadiliko makubwa yanatakiwa kuanzia kwa Kocha Mkuu, David Moyes, maarufu kama Daudi kwa mashabiki wa soka hapa nchini.  Lazima aonyeshe kujiamini na kuna mambo muhimu yanatakiwa kuanzia kwake kabla ya wengine.

Katika mechi ya Ligi Kuu England kati ya Arsenal dhidi ya Man United, wachezaji wa Man United walionyesha wazi kwamba hawakuwa wakicheza kwa juhudi kwa asilimia mia. Hata kama walifanya hivyo ilikuwa kwa kipindi fulani.

Mambo mengi yanapaswa kubadilishwa katika kikosi hicho, huenda kwa sasa ikaonekana kuna wachezaji ambao hawana uwezo mzuri, lakini kama hali ya kisaikolojia haitakuwa vizuri, bado hata wapya watakaosajiliwa watashindwa kufanya vema.

Moyes anaweza kuanza na suala la kiungo nyota mshambuliaji, Adnan Januzaj, ambaye ana kila sababu ya kumuamini na kumtumia kwa ajili ya kumjenga na ana uwezo wa kukisaidia kikosi chake kuleta mabadiliko.

Awali, Moyes alionyesha hilo kwa Januzaj lakini kadiri siku zinavyosonga mbele, amekuwa akimuingiza akitokea benchi, huku akiamua kumtumia mkongwe kama Ashley Young ambaye inaonekana uwezo wake umeporomoka, na jibu lingekuwa ni kinda huyo.

Kocha aliyepita wa Manchester United, Alex Chapman Ferguson, alifanya mambo kadhaa ambayo Moyes anaweza kujifunza na yatamsaidia kubadilisha mambo kadhaa, jambo zuri kwake kama mfano ni lile la Cristiano Ronaldo.

Ronaldo hakuwa mchezaji wa kikosi cha kwanza cha Sporting Lisbon, tayari makocha kadhaa kama Arsene Wenger wa Arsenal na Gerard Houllier wa Liverpool wakati huo walikuwa wameishaanza kumuona lakini Ferguson akaonyesha kuwa ni kocha mwepesi kuchukua uamuzi.

Kwani Manchester United ilipocheza na Sporting Lisbon jijini Lisbon na kufungwa mabao 3-1 katika mechi ya kirafiki, Ferguson alimchangamkia mapema kinda huyo.

Ingawa wengi wanaamini kelele za wachezaji wake kutaka amsajili wakiwa kwenye ndege wanarejea England zilichochea hilo, lakini ukweli ni hivi: Hata kabla ya mechi hiyo, Ferguson alizungumza na uongozi pamoja na Ronaldo na walikuwa wamemalizana.

Siku chache baadaye Ronaldo alifunga safari kwenda Manchester akiongozana na wakala wake na huko alisajiliwa kwa dau la pauni milioni 15 (Sh bilioni 35) na utaona haikuchukua hata siku tano kabla hajaanza kumchezesha, na kingine kikubwa alichokifanya ni kuonyesha anajiamini.

Baada ya kumaliza kila kitu, Ferguson alimuuliza Ronaldo alipendelea jezi ya aina gani. Yeye alisema anataka apewe jezi namba 28, ambayo alikuwa akiitumikia wakati akiwa Sporting Lisbon. Alihofia kuivaa jezi namba 7, ambayo mara ya mwisho ilikuwa ikivaliwa na David Beckham ambaye aliondoka na kujiunga na Real Madrid.

Beckham alikuwa nyota kuliko mchezaji mwingine England wakati huo, lakini kabla, jezi hiyo ilivaliwa na magwiji kama Eric Cantona na Bobby Charlton, hivyo Ronaldo alikuwa na haki ya kuihofia. Lakini angalia Ferguson alivyomjengea hali ya kujiamini, alisisitiza: “Utavaa jezi namba saba, achana na hiyo 28.”

Kumpa Ronaldo jezi namba saba, hakuna ubishi ulikuwa mzigo mkubwa. Lakini fomula inasema hivi: Binadamu akipewa kitu kigumu zaidi ndiyo wakati wa uwezo wake kuonekana.

Maana yake Ronaldo aliona ana deni kubwa mbele yake, akaweka juhudi zaidi kusudi asifeli au kuaminika kwa kuwa kila aliyekuwa na jezi hiyo alifanya vizuri kwa kipindi kirefu na kuwa ‘anayeibeba’ Manchester United.

Moyes anasubiri nini kwa Adnan Januzaj, kinda anayeonekana kuwa na kila kitu kasoro vitu viwili tu! Kupewa nafasi ya kucheza na kuaminiwa, basi. Uwezo na kipawa cha juu anacho, sasa vipi Moyes anashindwa kujiamini na kumpa nafasi badala ya kuwa anamuingiza kipindi cha pili?

Rekodi zinaonyesha Januzaj amecheza mechi 19, kati ya hizo 10 pekee ameanza na tisa ameingia. Amefunga mabao matatu, ametoa pasi mbili za mabao na amepiga mashuti 36. Dalili kwamba ana uwezo, tatizo ni kuaminiwa, kitu anachotakiwa kukifanya Moyes.

Moyes amekuwa akimuamini Young ambaye hata kama akifanya vizuri kwa msimu huu, hana uhakika wa ubora wa juu katika misimu mingine miwili. Vema nafasi hiyo akampa Januzaj ambaye kama atakuwa bora msimu huu, basi ni faida kwake kwa misimu mingine hata mitano kama wataweza kumbakiza.

Januzaj ana kasi, uwezo wa kupiga mashuti, krosi na msumbufu kwa mabeki. Huu ndiyo wakati mwafaka na ‘Daudi’ anapaswa kupunguza uoga, kujiamini na kufanya kile kilicho sahihi bila ya kuhofia lawama.

Wakati Ferguson ameingia Manchester United mwaka 1986, akitokea Aberdeen, miaka mitatu ilikuwa ya mateso kwake na mashabiki walikuwa wakiingia uwanjani na mabango wakitaka aondoke, lakini kipindi hicho ndicho alikuwa akitangaza kuwatema baadhi ya mastaa vipenzi vya mashabiki na akasisitiza anajenga kikosi. Moyes anaweza pia kujifunza.

TAKWIMU:
MSIMU WA 2013-14
MECHI     MABAO    PASI ZAO     MASHUTI

  19                  3                  2                        36

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic