Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen, ameweka bayana kuwa, iwapo
mlinda mlango Juma Kaseja ataendelea kusotea benchi katika klabu yake ya Yanga,
kamwe asitarajie kupata namba tena Stars.
Kocha huyo Mdenishi amekwenda mbali na kusema kuwa, Ivo Mapunda wa
Simba na Mwadini Ally wa Azam ambao wanacheza mara kwa mara, ndiyo wana nafasi
katika kikosi atakachokiita kwa ajili ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Namibia
mwezi ujao.
Alisema ‘tiketi’ pekee kwa mchezaji kucheza Stars ni kucheza mara kwa
mara kwenye klabu yake na wala hamjumuishi mchezaji kwa kuangalia jina.
Kaseja amekuwa chaguo namba moja kwa Kim kwa muda mrefu tangu akiwa
Simba, hata hivyo Kocha Mkuu wa Yanga, Hans van Der Pluijm, amekuwa akimuweka benchi
tangu alipochukua mikoba ya Ernie Brandts hivi karibuni.
Akizungumza na Championi Jumatatu, Kim alisema anaamini Kaseja bado ni
kipa mzuri lakini kwa jinsi anavyoishi kwa sasa ni chanzo cha kupoteza nafasi.
“Siwezi kuingilia kuhoji kwa nini
Yanga wanamuweka benchi, lakini siku zote, uteuzi wangu huzingatia mchezaji kucheza
mara kwa mara katika klabu yake na wala siangalii sura wala jina.
“Naamini bado Kaseja ni kipa
mzuri na anaweza kucheza vema, lakini iwapo ataendelea hivi (kukaa benchi) mhh.
Wapo makipa ambao wamekuwa wakifanya vema tangu kuanza kwa ligi kuu kama
Mwadini na Ivo, kwa kweli nimekuwa nikivutiwa nao,” alisema Kim.








0 COMMENTS:
Post a Comment