March 3, 2014



Na Saleh Ally
YANGA imevunja mwiko dhidi ya Waarabu wa Misri, imewafunga Al Ahly katika kipindi wakiwa mabingwa wa Afrika na kikosi namba moja kwa ubora barani Afrika.

Yanga wana kila sababu ya kuamini kwamba wana kikosi bora, si kwa bao moja pekee la Nadir Haroub ‘Cannavaro’ lakini namna walivyocheza na kuwapa kazi kubwa Waarabu hao wabishi.

Katika mechi hiyo ya Ligi ya Mabingwa Afrika iliyopigwa juzi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, Yanga walionyesha uwezo wa juu lakini wakawa na kasoro kadhaa, moja kubwa ni ile ya kutotumia nafasi walizozipata.
Wakati Yanga inafungwa bao 1-0 na Al Ahly kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar mwaka 2009, kosa kama hilo pia lilitokea. Pamoja na kwamba walifungwa, lakini walipoteza nafasi nyingi sana za kufunga kupitia Davies Mwape na Kenneth Asamoah.

Walipokwenda jijini Cairo, wakakutana na kipigo cha mabao 3-0, wakawa wametolewa kwa jumla ya mabao 4-0, rekodi ya kuendelea kunyanyaswa na Waarabu ikaendelea kujazwa uzito.
Sasa Yanga wameivunja, wamewafunga Waarabu hao wenye uwezo mkubwa kisoka. Huo ni mwanzo, hakuna anayejua kuwa kazi ni ngumu na ili Yanga iweke rekodi sahihi, lazima ibaki njia kuu, ikichepuka tu, imekwisha!
Kusherehekea ushindi wa bao 1-0 Taifa juzi ni sahihi kabisa. Lakini vizuri sherehe zisizidi saa 24, badala yake maandalizi ya mechi ya mwisho inayotarajiwa kupigwa Jumapili ijayo ndiyo yapewe nafasi kubwa hasa kwa kikosi cha Yanga.
Al Ahly wameondoka, wakitua kwao moja kwa moja wataanza maandalizi na inawezekana kabisa yatakuwa ni maandalizi ya juu kuliko walivyotarajia kwa kuwa wamepoteza mchezo, kitu ambacho hawakutarajia.

Kocha Hans van Der Pluijm amesema anajua kuwa fitna zitachukua nafasi kubwa, hilo amejiandaa lakini uwezo wa soka, kila aliyekwenda uwanjani ameona, wanao, tena ni mkubwa. Kama wakijumlisha na fitna, itakuwa ni kazi kubwa zaidi kwa Yanga.
Ili Yanga ibaki njia kuu, lazima hesabu zake ziwe na muendelezo badala ya kuchepuka na kuanza upya. Hadi walipofikia ni nusu ya safari, kama ingekuwa ni ligi ndiyo mzunguko wa kwanza umemalizika na inajulikana wa pili unavyokuwa mgumu.
Muendelezo ni muhimu, hadi kufikia walipo na kuifunga Al Ahly kwa mara ya kwanza nyumbani, nini kilifanyika. Lakini sasa ni wakati mwafaka wa kuingia B kwa kutumia A ambayo ni muhimu sana kwao.
Kuingia kwenye hatua ya pili kwa kufuata njia waliyoanzia bila ya kuchepuka kutajenga muendelezo na kufanya Yanga iwe na nafasi ya kufanya vizuri Cairo.
Wanachotakiwa kuamini ni kazi imefanyika nusu, nusu iliyobaki lazima ifanyiwe kazi kikamilivu na kitu kizuri zaidi ya Yanga wamewaona Ahly wakipambana nao lakini lazima wajue huo ni mchezo wa ugenini.

Vichwa:
Wachezaji wa Ahly walizozana sana baada ya kufungwa, si kwamba pekee hawapendi kufungwa, lakini kilichowaudhi ni bao la kichwa. Kwamba wao ni warefu na wana uwezo wa kupiga zaidi mipira ya juu.
Walilia na uzembe wao na kweli ndiyo uliosababisha wao kufungwa. Utaona kwa asilimia 70 mipira ya juu ilikuwa yao na si kwa wachezaji wa Yanga.
Kwa hili, Yanga lazima wajue kuna kazi ya kufanya, Ahly walipata shida na mipira ya chini, Yanga kuinua juu mipira ni sawa na kuigawa sadaka.

Mashuti:
Kingine ambacho kilionekana ni kosa kubwa kwa Yanga, ni wachezaji wake kurudi nyuma wakati wa kukaba na kuruhusu Waarabu hao kukimbia hadi zaidi ya mita 10 na mpira, halafu wakapiga mashuti.
Hakuna ubishi wana nguvu na kama mashuti yao yakilenga lango, basi ni hatari. Iwe isiwe, lazima Yanga walifanyie kazi suala hilo. La sivyo litakuwa tatizo kubwa.

Mabeki:
Walinzi wa pembeni wa Yanga lazima wajue wao ni nusu ya uhai wa Yanga, utaona Ahly walikuwa wakipambana kupata krosi. Inaonekana mfumo wa Pluijm uliwazima kufanya walichotaka kwa asilimia kubwa.
Lakini wakiwa Cairo haitakuwa kazi rahisi sana, lazima watapiga krosi nyingi na wanategemea mipira mingi ya vichwa, wana sifa ya kuwa wazuri kwenye kufunga mabao ya vichwa, pia wana miili mikubwa, hivyo wana nafasi ya kufunga.
Kama mabeki wa pembeni watacheza kwa uwezo wa juu, mawinga au viungo watawasaidia kukaba na kuziba mifereji ya krosi, watasaidia kwa kiasi kikubwa kupunguza hatari.
Kujiamini:
Huenda wengi hawakuliona hili, ila kuna wachezaji wa Yanga walikuwa na ‘mcheche’, hata kutoa pasi ilikuwa shida. Hapo ni nyumbani, kama wakifanya hivyo ugenini litakuwa ni tatizo kubwa. Hivyo lazima wajiamini na kuonyesha uwezo kwa kufuata mipango ya kocha.

Haya ni machache, kocha na benchi la ufundi la Yanga linajua mengi zaidi. Kikubwa hapa ni kubaki njia kuu na kuendeleza kufanya mambo kwa uhakika, kikubwa wakumbuke, mechi ijayo itakuwa ngumu zaidi ya ile ya juzi Taifa.






0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic