April 9, 2014


Na Saleh Ally
KOCHA Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ ni kati ya wadau wakubwa na sehemu ya sura ya mchezo wa soka hapa nyumbani, ataendelea kuwa gumzo kwa miaka mingi ijayo bila ya kujali yu hai au la.


Julio ni kati ya wachezaji wachache wa Tanzania ambao wamekuwa na mwendelezo mzuri tokea wakiwa wachezaji hadi walipofikia kuchukua nafasi ya ukocha.

Beki huyo wa zamani wa Simba, amekuwa na mafanikio wakati akicheza lakini ameendelea kufanya hivyo baada ya kuanza kufanya kazi katika nafasi ya ukocha.


Moja ya sifa kubwa ya Julio ni ucheshi, maneno ya vichekesho na hata yale ya shombo ili mradi inategemea ni wakati gani. Ni kivutio kwa wadau wa soka na amekuwa akizidi kuongeza chachu ya burudani ya mchezo huo.

Mimi binafsi kupitia Championi, nimekuwa nikimkosoa Julio mara kadhaa kutokana na mambo mbalimbali ambayo yalitokea akiwa kocha wa Simba kwa vipindi tofauti.

Najua nitakuwa ninamuudhi sana, lakini sijawahi kulifikiria hilo sana kwa kuwa ninapomkosoa, zaidi huwa ninalenda kurekebisha kwa manufaa ya mpira wa Tanzania na si vinginevyo.

Lakini inapofikia wakati wa kusifia, basi ni kipindi kizuri kumpa mtu sifa ya kile ambacho amekifanya kama ambavyo alivyofanya kocha huyo akiwa na timu yake ya Mwadui United ya mkoani Shinyanga.

Mwadui United iliyokuwa inaongozwa na Julio imepambana hadi kufikia kupanda daraja, yaani Ligi Kuu Bara na kuwaacha jirani zao Stand United kwa muda tu, kwani wakati Mwadui wakisherekea kupanda daraja, taarifa za Stand kushinda rufaa yao dhidi ya Kanembwa ziliwadia na kuwapa nafasi ya kupanda.

Unaweza kusema kwa mara nyingine, Julio alichungulia Ligi Kuu Bara kwa sekunde kadhaa tu na baada ya hapo akarejea tena Ligi Daraja la Kwanza, ndiyo maana amekuwa na jazba kuhusiana na suala la Stand United kupanda.

Julio ana haki kama walivyo na haki Stand ambao walikuwa wamekata rufaa. Kwa kuwa ni kocha, ukaachana na rufaa utaona Julio ni kocha aliyeipandisha timu ligi kuu na hilo halina ubishi. Jiulize, timu aliyoipandisha ni ipi?

Julio aliamua kujiunga na Mwadui ambayo iko mkoani Shinyanga, tena si mjini, mwendo wa takribani dakika 45 kutoka Shinyanga mjini. Kipindi hicho ndiyo alikuwa ametemwa Simba.

Kwa kocha ambaye haiamini kazi yake, haraka asingekubali kwenda kwenye timu ambayo haina jina na inawania kucheza Ligi Kuu Bara. Lakini Julio akafanya hivyo, tena katika kipindi kigumu na somo langu la leo linaanzia hapo.

Hii inaonyesha Julio pamoja na kusifika kwa ‘mdomo mwingi’, lakini si mtu wa maneno tu, badala yake anaiamini kazi yake, anaamini anachokifanya, ndiyo maana alijiamini kwenda Shinyanga na kuifundisha Mwadui ambayo ilikuwa na jina kubwa enzi zile akina Julio wanacheza.

Julio anatokea katika familia ya soka, lakini hicho hakiwezi kuwa kigezo cha cha ubora wake, kwani hata wadogo zake walikuwa wanasoka mahiri lakini hawajafikia alipo, hii inaonyesha ana kipaji na anajituma kufikia alipo.

Inawezekana ikawa ni rahisi kumdharau Julio kwa kuwa ana maneno mengi, au kwa vile alishafukuzwa Simba halafu akarudi kila inapotokea ameitwa tena. Ukweli ni kwamba ni kocha mzalendo anayeiweza kazi yake, tofauti zake za kibinadamu weka kando.

Kupongezana ni jambo jema. Shikamoo Julio, natoa saluti kwa kazi yako safari hii na ikiwezekana unaweza kufanya vizuri zaidi ya ulivyofanya sasa kama utaendelea kujiamini lakini ukakaa kwenye mstari sahihi ambao unaamini utakusaidia kukua na kukuza mpira wetu.

Kwenye soka sasa Julio ni baba, ingawa watoto wako Super na kaka yake tayari wanacheza soka nje ya Tanzania, lakini misingi bora inatakiwa kwenye soka hapa nyumbani na watu wanaoweza kuwa mfano ni wewe na watu wa aina yako walio tayari kujitolea.

Tabia ya ukweli ni sehemu kubwa ya maendeleo katika kitu chochote duniani hata kama utakuwa unawaumiza watu. Mara nyingi umekuwa mkweli, endelea hivyo kwa kuwa mara nyingi umekuwa ukisema ukweli.

Ushauri mdogo tu, vizuri ukapunguza jazba kwa kuwa penye wengi kuna mengi na hamuwezi kufanana mnavyofikiria iwe ni sahihi au la! Mfano, siku ukitoka nje ya reli, basi nitakuwa wa kwanza kukukosoa.

Makocha wengine wazawa, mna mengi ya kujifunza kwa Julio, siwashauri mjifunze uongeaji, hicho ni kipaji chake. Lakini uwezo wake wa kujenga kikosi, kuwashawishi vijana kujituma na hali ya kujiamini aliyoionyesha kwenda kuichukua Mwadui na kuipa mafanikio ni somo kubwa kwenu, msimuone ni mtu wa kubahatisha.

Kwanza mkubali kwamba amefanya jambo zuri na lenye mafanikio, halafu pili tulieni mtadhimini uzuri wake, baada ya hapo mjifunze na mtaona mtafaidika.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic