June 27, 2014



Na Saleh Ally
SUALA la uchaguzi wa Simba uliopangwa kufanyika keshokutwa Jumapili limekuwa na vipingamizi vingi hapa katika, likiwemo lile suala la baadhi ya wanachama wake wachache kuamua kwenda mahakamani kuusimamisha.
Hiyo ni sehemu ya mapito tu na mara nyingi hutokea kwenye kila jambo la wengi, lakini hali halisi ni hivi, uchaguzi wa Simba lazima utafanyika, hakuna mwenye uwezo wa kuuzuia milele.

Kama kuna wanachama wa Simba watakuwa wanakubaliana nami kuwa uchaguzi huo lazima ufanyike, iwe keshokutwa Jumapili au siku nyingine, basi wao wanapaswa kujipanga kwa hesabu za kuchagua viongozi sahihi kwa klabu yao.

Nimeamua kuandika Hoja Yangu leo nikilenga suala la nani achaguliwe ikiwa ni sehemu ya niliyoyaona kwenye uchaguzi uliopita na mingine baadhi ya klabu hiyo au nyingine ambayo uchaguzi wake wa viongozi umekuwa ukisababisha matatizo kadhaa, nitafafanua.

Wakati wanachama wanakwenda kwenye uchaguzi, utaona wengi wamekuwa wakiangalia nafasi za juu nani hasa atakuwa kiongozi. Mfano mwenyekiti na makamu wake na sasa kwa Simba itakuwa ni rais na makamu wake.

Nafasi ya rais kwa sasa inagombewa na Evans Aveva na Andrew Tupa, makamu wa rais ni Jamhuri Kiwhelo ‘Julio’, Geofrey Nyange ‘Kaburu’ na Sued Nkwabi.

Nafasi hizo mbili za juu ndiyo zimekuwa jicho, kila mtu anataka kujua nani atachukua nafasi hiyo na itakuwaje lakini si lahisi kusikia nafasi za wajumbe zinazungumziwa kwamba nani atachukua.

Kuzidharau nafasi za wajumbe ni kosa kubwa, huenda wengine wamewahi kulifanya huko nyuma na hawakujua lilikuwa ni tatizo kubwa kiasi kutokana na wao kutokuwa makini wakati wa kuchagua wajumbe.
Wajumbe hao wataingia kwenye kamati ya utendaji, maana yake ndiyo watakaokuwa wakipitisha mambo yote makubwa yanayohusiana na klabu pamoja na kikosi cha SImba. Hivyo lazima wawe watu imara, wenye fikira pevu, ‘fikira jenzi’ na wanaotaka maendeleo ya dhati kwenye klabu hiyo.

Hakuna anayeweza kunikatalia kwenye uchaguzi wa klabu hizi kubwa, wako wanaotaka kuingia kwa ajili ya kujinufaisha wao, wanaotaka kuonekana tu, wanaofuata mkumbo na wengine wanajua hawana uwezo wa kuongoza, lakini watataka tu wagombee.
Wanachama wa Simba watakuwa wanawachagua watu wanaowajua, wanaishi nao, majirani zao, wanajua habari zao, hivyo wanapaswa kuwa makini kwenye kuamua badala ya kufanya kwa kufuata mkumbo au kubahatisha.
Uchaguzi wa kishabiki pia umekuwa ni tatizo kubwa katika matokeo ya uchaguzi mwinhi katika klabu au mashirikisho ya michezo mbalimbali nchini. Mwisho wake ni kuchagua watu kwa kubahatisha na iingie kwenye kipindi kigumu kwa miaka minne.

Kama rais na makamu wake watakuwa watu imara, halafu Simba ikawa na wajumbe ilimradi na watu waliwachagua kishabiki au kwa kufuata mkumbo, mwisho wake wawili hao imara wanakuwa kwenye mzigo mkubwa.
Kulahisisha mambo, lazima kutokuwa na wajumbe mizigo kwenye klabu hiyo. Hivyo wanachama ndiyo watakuwa na kazi kubwa kwenye uchaguzi huo kuhakikisha Simba haiangukii kwenye wajumbe mizigo.

Wanachama ndiyo wenye uamuzi wa mwisho kuhusiana na nani au yupi awe kiongozi wa klabu yao. Hakuna atakayekuwa anataka kupiga kura kumchagua kiongozi ambaye ataiangusha iingie kwenye matatizo.
Hivyo kitu cha kwanza ni kuepusha viongozi au wajumbe mizigo ambao watakuwepo, hawana mchango wowote, kazi yao kupiga majungu na kawaida, watu wengi wenye uwezo mdogo kwenye kuamua mambo makini au kutatua mambo magumu, wana tabia za majungu na kuanzisha migogoro.

Wengi wenye uwezo mdogo wa kujibu hoja, hukimbilia maneno mengi, wana tabia za kulaumu sana, wanaamini wameonewa na ndiyo wamekuwa matatizo makubwa hata kwa Simba yenyewe. Hivyo mkichagua kwa umakini viongozi wenu wa juu, basi msipuuze umuhimu wa kuchagua wajumbe imara pia ili kuunda uongozi imara.
Kila la kheri Jumapili.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic