July 7, 2014



WAKATI fulani niliwahi kuzungumzia kuhusiana na namna ambavyo Simba inaweza kufanya mambo yake yakabadilika katika kipindi kifupi, lakini zaidi nikazungumzia suala la umoja.

Lakini siku chache baadaye, aliyekuwa mgombea wa Urais wa Simba, Michael Wambura akaibuka hasa baada ya Rais wa Simba, Evans Aveva kusema watamjadili Wambura kwenye mkutano mkuu wa Simba.

Wambura anapinga kujadiliwa kwa kuwa anaamini uanachama wake sasa ni sahihi kwa kuwa kamati ya rufaa ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ilimsafisha baada ya kuwa ameondolewa na kamati ya uchaguzi.

Kamati ya uchaguzi chini ya Dokta Damas Ndumbaro ilimuondoa kwa madai unachama wake una mushkeli na kila kitu kikawekwa wazi. Kamati ya rufaa ilipokutana, ikaamua tena kwa kupiga kura za vidole kwamba Wambura alikuwa mwanachama halali.
Hapo ndiyo hoja ya Wambura kuhusiana na kutaka kujadiliwa, lakini bado kamati ya rufaa ya TFF haiwezi kuwa mwamuzi wa mwisho kuhusiana na uanachama wa Wambura. Yoyote anaweza asiiamini ndiyo maana hata baada ya kusisitiza Wambura alifanya kampeni nayo ikaungana na ile ya uchaguzi kumfuta ugombea, kuna wanachama wamekwenda mahakamani.

Wanachama wa Simba waliokwenda mahakamani ni wale waliofurahia mara ya kwanza kurudishwa kwa Wambura kupitia kamati hiyo ya rufaa ya TFF. Safari ya pili ilipobaini kweli Wambura ana makosa na kuishindilia adhabu aliyopewa, wanachama haohao hawajaiamini na wamekwenda mahakamani.
Hivyo hata Simba pia wanaweza kujiridhisha na kama suala lake litajadiliwa na wanachama, basi litakuwa zuri zaidi kwa kuwa hata wale waliokuwa wanapinga taarifa za kuwa wanachama wake una walakini watakuwa na nafasi ya kuzungumza mbele ya wenzao na mwisho hilo litapata mwafaka.

Wambura anaweza kuwa kati ya viongozi wanaohitajika kwenye soka, lakini kuna mambo kadhaa likiwemo hilo la unachama anaweza kulifanyia kazi ikiwezekana kabla ya kugombea tena.

Lakini kwa Aveva, lazima ajikumbushe kwamba ana mambo mengi sana ambayo ni dhamana aliyopewa na Wanasimba ambao wamemuamini ili awondoe katika machungu na hali ya mambo kuwa sintofahamu kama ilivyokuwa kwa uongozi uliopita.
Vizuri nguvu nyingi za anayotaka kufanya azielekeze kwenye maendeleo ya Simba ambayo imekwama kwenye tope. Uzito yaani ukubwa wa klabu hiyo unahitaji gia kubwa, hivyo lazima kuwe na umakini na juhudi za juu kufanikiwa katika hilo.

Aveva hana haja ya kushika mbili ili moja isije ikamponyoka kwa kuwa lengo kubwa sasa ni kuipeleka Simba kwenye mabadiliko na baadaye mafanikio na ndicho wanachosubiri Wanasimba.

Wapiga kelele hawatakosekana, wako ambao wamekuwa wakisema wanapambana kwa ajili ya maslahi ya Simba, lakini ukweli wao wanapigania maslahi ya matumbo yao kwa kuwa klabu kama Simba, kwao ni mitaji.
Wako wanaolazimisha vurugu ili walipwe wakati wa kipindi cha vurugu, lakini wako ambao wamekubali kuwa wapambe, ili mradi kuendesha tu maisha yao na si faida ya maisha ya klabu lakini mazungumzo yao wanasema wanaipenda Simba.

Aveva amepata kura za wanacham wengi zaidi, mashabiki wengi wanamkubali, hivyo kuendeleza malumbano na upande mwingine ni kuwapa nafasi wanaotaka afeli ili aseme, waonekane wameshinda.

Lazima kuangalia zaidi kuhusu malengo, nini cha kufanya kikosi cha Simba kiimarike na kuwa bora, lakini mipango ikiwezekana hadi ya miaka kumi ijayo kuisaidia Simba kupita kwenye reli sahihi.
Aveva anaweza kuamini ule msemo wa “kelele za chura…” halafu akaendelea na mambo ambayo yanahusu maendeleo ya Simba. Lakini kikubwa zaidi ni kujitahidi kudumisha umoja kwa wale watakaokuwa wanakubaliana nao na kutenda hadi miongoni mwa wanachama na mashabiki wa klabu hiyo.

Kwa wanachama wanaompinga, pia wanapaswa kufanya mambo kwa kuangalia kipi hasa ni sahihi kwa kuwa Simba inataka mabadiliko kwenda mafanikio. Wanaotaka kulazimisha migogoro ili wafaidike kwa kisingizio kuwa wanaipenda Simba, nao ni tatizo pia.

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic