August 8, 2014




NA Saleh Ally
MOJA ya sifa za Kocha Mkuu wa Arsenal, Arsene Wenger ni ubahili! Kisa amekuwa hataki kutoa fedha ili kununua wachezaji wapya.


Kwa Tanzania, wabahili wana sifa nyingi, moja wapo ni kuficha fedha zao kwenye vibubu au vyungu. Sasa Wenger amebadilika.
 
ALEXIS
Wengi wanasema anaamini sana vijana, au anaamini sana yale magari ya kukarabati halafu unauza kwa bei kubwa!

Amefanya hivyo kwa mafanikio makubwa kwa kuchukua wachezaji walioaminika hawafai, akawanunua kwa bei chee na kuwauza ghali, Arsenal ikaingiza faida.

Utaona juzi na jana vyombo vya habari vilionyesha kushangazwa na Wenger ‘alivyolilisha’ Jiji la Manchester lenye timu za Man United na Man City, maana wachezaji kama Emmanuel Adebayor, Gael Clichy, Kolo Toure, Samir Nasri, Robin van Persie na Bacary Sagna, wote hao aliwapata kwa bei chee.
 
OZIL
Lakini kwa sasa hauwezi tena kumuita mbahili na ikitokea mtu akafanya hivyo atakuwa amejisahau au anamuonea tu.
Wenger sasa ni kati ya makocha wanaojichia vilivyo kifedha, ‘matanuzi’ kwenda mbele na hilo halina ubishi.

Msimu uliopita, alimnunua mchezaji kwa pauni milioni 42 (zaidi ya Sh bilioni 100), ukawa ndiyo usajili ghali zaidi. Huyo ni Mesut Ozil.

Msimu huu amesajili wachezaji watano kwa pauni milioni 59, kati ya hizo pauni milioni 32 pekee amemnunua Alexis Sanchez.

Hivyo kama utajumlisha fedha za Ozil msimu uliopita na Sanchez msimu huu ni pauni milioni 74. Fedha hizo kwa wachezaji wawili tu, nani atamuita Wenger mbahili, kumbuka hafundishi Real Madrid.

Msimu uliopita alipunguza ubahili, akabeba Kombe la FA. Msimu huu amezidi kupunguza ubahili zaidi. Je, Arsenal itakuwa bingwa Premiership?


Alexis Sanchez:
Usajili wake unaelezwa kufikia pauni milioni 32, si kidogo. Anatokea Barcelona kwenye La Liga, lakini uchezaji wake wa kujituma na nguvu, hakuna hofu ya kushindwa na mfumo wa Kingereza.

Hii inaonyesha kweli Wenger ameondoka kwenye kundi la wabahili kutokana na kutumia mamilioni ya pauni.

Sanchez alikuwa anaaminika ni wanne kwa ubora wa ufungaji mabao kwenye La Liga, lakini alikuwa mwiba wakati akiwa mshambuliaji wa Udinese ya Italia akicheza nyuma ya Antonio Di Natale.

Mesut Ozil:
Wenger alikubali kutoa pauni milioni 42.5 kumtwaa akitokea Real Madrid lakini ikaonekana kama vile amebugi. Msimu uliopita ndiye alikuwa mchezaji ghali zaidi.

Wachambuzi wa England wakasema hana nguvu na si imara kupambana kwenye Ligi Kuu England, sasa anawaonyesha.

Kwanza ameisaidia Arsenal kubeba ubingwa wa FA, pia ndiye mmoja wa wachezaji watatu wa juu waliotoa pasi nyingi za mabao Premiership msimu uliopita.

Kwenye Kombe la Dunia kaonyesha uwezo sahihi na sasa anarudi England akiwa tayari na amezoea, matarajio ni kung’ara.


Wapya:
Alexis Sanchez (Barcelona, pauni 32m), Mathieu Debuchy (Newcastle United, pauni 12m), David Ospina (Nice, pauni 3m), Calum Chambers (Southampton, pauni 12m).

Waliondoka:
Lukasz Fabianski (Swansea City-huru), Bacary Sagna (Manchester City-huru), Chuks Aneke (Zuite Waregem-huru), Nicklas Bendtner (huru), Chu Young Park (huru), Wellington Silva (UD Almeria-mkopo), Thomas Eisfeld (Fulham-siri), Carl Jenkinson (West Ham-mkopo).
SOURCE: CHAMPIONI


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic