August 22, 2014





 WAZO la awali ilikuwa ni kwamba kikosi cha wakongwe cha Real Madrid kicheze mechi ya kirafiki dhidi ya timu ya soka ya taifa, Taifa Stars. Nilikuwa kati ya wale waliopinga hilo.


Waandaaji Kampuni ya Tanzania Sisi ni Nyumbani (TSN), chini ya mkurugenzi wao Farough Baghoza, wakaonyesha ni watu wanaoweza kusikiliza jambo ambalo lina hoja ya msingi kwa kuwa wadau wengi walichangia na kuona haikuwa sahihi.

Kweli wakalifanyia kazi na kuamua kuita kikosi cha wachezaji wakongwe kutokana na timu mbalimbali za Tanzania kama vile Simba, Yanga, Sigara, Pan African na nyingine nyingi kuunda kikosi.

Tayari chini ya Charles Boniface Mkwasa ‘Master’ akishirikiana na Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ na Fred Felix Minziro ‘Majeshi’, wameanza maandalizi kwenye Uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam.

Hili ni wazo sahihi kwamba wakongwe wa Real Madrid ambao wataongozwa na wachezaji kama Luis Figo, Christian Karembeu, Steve McManamann, Fernando Morientes, Fabio Cannavaro, Michel Salgado na wengine, watakutana na wakongwe wenzao.

Mechi hiyo itapigwa kesho Jumamosi kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar, nimeanza kuona pilika na namna ambavyo watu wamekuwa wakikimbilia tiketi kwa kuwa waandaaji waliweka hadi zile za kiwango cha chini cha Sh 5,000.

Hadi kuwa na kiingilio cha Sh 5,000, inaonyesha pamoja na gharama kubwa za maandalizi, waandaaji bado wamewafikiria Watanzania na uwezo wao na hasa wapenda soka. Wamewapa nafasi ya kwenda kuwaona nyota kama hao niliowataja.

Kumuona Figo akicheza dhidi ya Abubakari Kombo kwa Sh 5,000 tu ni zawadi na huenda itakuwa mechi ambayo kila atakayepata nafasi ya kuiona, itakuwa ni mara moja tu na si zaidi ya hapo.

Ninaweza kusema si vizuri kukosa kama una nafasi ya kufika, kwa kuwa soka ndiyo burudani yetu. Kuburudika si vibaya, lakini ninalenga watu kutokwenda kwenye mechi hiyo kwa wingi kwa lengo la kuangalia Figo na wenzake wanakimbia vipi, wanapigaje chenga ili washangilie tu, halafu wakitoka, imepita.

Ujio wa kikosi hicho, hata kama tutajikausha, ukweli ni bahati. Hakuna ubishi, wengi wao ni wachezaji waliocheza kiwango cha juu. Kucheza Real Madrid, ndiyo juu ya mlima, ni timu bora na maarufu ikiwezekana kuliko zote duniani.

Uchezaji wao lazima utakuwa na jambo au utofauti mkubwa na kwa kuwa watakuwa wakicheza dhidi ya wakongwe wetu, tunaweza kujifunza mengi kwamba wachezaji wa nyumbani wana nini na wanakosa kipi.

Kweli itakuwa ni mechi ya kujifurahisha, lakini katika soka ushindani ni kitu kisichofichika. Hivyo lazima ushindani utajitokeza na mwisho itakuwa rahisi kupima mambo.

Watakaoingia uwanjani pamoja na kuwa wadau au mashabiki wa soka, watakuwa na idara zao kama waamuzi, marefa, wachezaji wanaoendelea kucheza, makocha na kadhalika. Basi vizuri kuifanya mechi hiyo ni shule.

Ukweli si kila kitu lazima usome darasani, badala yake kuna madarasa yanayopatikana kwa siku moja na yanaweza kukuachia somo la siku kibao na faida kubwa, ila kama kweli utataka kujifunza au kujielimisha.

Kuangalia Figo anaonekana vipi, sijui umbo kubwa, mguu wenye ‘kiazi’ kikubwa, sura yake inafananaje, hiyo ni burudani. Lakini hakikisha hautoki Uwanja wa Taifa bila ya kuwa umefaidika na kisomo.

Msisitizo ni kwamba, si lazima ujifunze kupitia akina Figo, Karembeu na wenzake. Badala yake unaweza kujifunza pia kupitia wakongwe wetu ambao wanaweza kupimika wakati 
wakicheza na wale wenye kiwango na maisha ya juu.
SOURCE: CHAMPIONI

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic