August 27, 2014



Unaweza kusema kumekucha baada ya Yanga kufikia uamuzi wa kumfungulia mashitaka mshambuliaji wake Emmanuel Arnold Okwi afungiwe kucheza soka.


Yanga imefikia uamuzi huo baada ya kuonekana kutoridhishwa na mwenendo wa Okwi raia wa Uganda ambaye hata hivyo ameishatua nchini akisubiri kujiunga na kikosi cha Yanga ambacho kipo kambini mjini Zanzibar.

Barua ya Yanga ya Agosti 25 iliyosainiwa na Katibu Mkuu, Beno Njovu, imetua kwenye Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) ikifafanua mambo mengi ikiwa ni pamoja na Okwi kukiuka mkataba na Yanga kwa kufanya mazungumzo na klabu ya WadiGalde FC ya Misri.

Barua hiyo inaeleza Okwi amekiuka vipengele vya Fifa, Caf na TFF kwa kufanya mazungumzo na timu hiyo ya Misri ambayo tayari imeiandikia Yanga barua ikitaka kumnunua kwa dola 60,000 (zaidi ya Sh milioni 95).

“Okwi aliwasiliana na mmoja wa viongozi na kumuambia amefanya mazungumzo na timu ya Misri inamtaka, kiongozi akamuambia aandike barua, kweli akafanya hivyo kupitia mwanasheria wake.

“Siku chache baada ya Yanga kupokea barua, WadiGalde FC nayo ikaiandikia Yanga barua kuwa inamtaka kwa kitita cha dola 60,000 ambazo zinalingana na zile zilizoandikwa kwenye barua ya mwanasheria wake. Kulingana kwa kiwango cha fedha kunaonyesha walikuwa na mawasiliano.

“Hili ni kosa kisheria kwa kuwa Okwi bado ana mkataba na Yanga, angalau ingekuwa imebaki miezi sita angeweza kufanya hivyo. Mwanasheria wake (Edgar Agaba) pia ameshiriki na tunaomba TFF kuwafungia wote kujishughulisha na soka nchini,” ilieleza sehemu ya barua hiyo.

“Pamoja na kuwafungia, Okwi anatakiwa kutulipa fidia ya dola 200,000 kwa kuchangia kutukosesha ubingwa pamoja na kurudisha fedha zote alizolipwa za usajili ambazo ni dola 60,000 pia fedha zote za mshahara,” ilifafanya zaidi sehemu ya barua hiyo.

Yanga imemtuhumu Okwi kwa kukosa mechi saba kati ya 13 za mzunguko wa pili kitu kinachoonekana ni kama kuchukuliwa fedha zake bure kwa kuwa Okwi hakuitumikia ipasavyo.

Msisitizo umewekwa kuwa Okwi alitoroka kambini hali ambayo ilionyesha utovu wa nidhamu na baadaye akajiondoa kabisa katika kikosi kwa madai hakupewa nyumba na hakuwa amelipwa sehemu ya fedha zake zilizobaki.

Hakuna kiongozi wa Yanga au TFF aliyetaka kulizungumzia suala hilo, lakini Salehjembe ikaamua kulipaisha kwa kuwa ina uhakika wa asilimia 100 kutokana na kunasa kopi ya barua hiyo, mara tu baada ya kutua TFF.

Katika barua hiyo ambayo imetaja vifungu kadhaa vya Fifa ambavyo Okwi amekiuka, maana yake ni utuhibitisho tosha kwamba sasa haimtaki tena Okwi.

Ile nafasi moja waliyokuwa wakigombea na Hamis Kiiza, maana inakwenda kwa Mganda mwenzake na yeye anaanza ‘mgogoro’ huo na Yanga ambayo imeamua kuwa ngangari.

Okwi aliyesajiliwa Yanga kwa dau la dola 100,000 (zaidi ya Sh milioni 165), aliamua kususa kuichezea Yanga akidai kucheleweshewa fedha na alikosa mechi nne za mwisho za mzunguko wa pili, zikiwemo mbili dhidi ya Yanga na Azam FC ambao waliibuka kuwa mabingwa.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic