August 11, 2014



KIPIGO cha mabao 3-0 walichokipata Simba katika mechi ya kirafiki ya kimataifa dhidi ya Zesco ya Zambia, kimekuwa gumzo!


Simba waliojitokeza kwa wingi kuangalia utambulisho wa wachezaji wao wapya na wale wa zamani kwa mara nyingine, waliondoka uwanjani wakiwa vichwa chini huku watani wao wa jadi Yanga, wakiwa na furaha ya kufa mtu.

Utani ni jambo la kawaida, Simba ikifungwa ni furaha kwa Yanga, hivyo mashabiki wachache ‘walioutuliza’ Uwanja wa Taifa kwa kuwazomea Simba waliojitokeza kwa wingi, ilikuwa haki yao.

Wakati Yanga wanawazomea Simba, hapo unazungumzia ushabiki, lakini Simba imepoteza mechi hiyo, sasa tunaangalia masuala ya ufundi. Kwanza tuanze na Kocha Mkuu wa Yanga, Marcio maximo.

Hivi karibuni, Maximo ameingia kwenye lawama na mashabiki wa soka wamekuwa wakiamini ni muoga sana kwa kuwa hataki mechi za kirafiki, kisa anaona ni aibu kwake kufungwa.

Hata Katibu Mkuu wa Baraza la Vyama vya Soka Afrika Mashariki na Kati (Cecafa), Nicholas Musonye, amemuita Maximo ni muoga lakini kocha huyo Mbrazili akasisitiza anatengeneza timu na huu si wakati mwafaka.

Kipigo cha Simba kutoka kwa Zesco, tena huku Wazambia hao wakionyesha uwezo mkubwa wa pasi, mipango ulionyesha kuwa Simba bado ‘hawajakwiva’ na wanahitaji mazoezi zaidi ili kujiweka kwenye kiwango sahihi.

Kweli bado hawajawa tayari, ndiyo maana wanakwenda kambini Zanzibar kwa wiki tatu, maana yake wamecheza na Zesco wakiwa hata hawajafikia katikati ya maandalizi sahihi, lakini mashabiki hawalijui hilo na walichotaka ni ushindi.

Wakati tunatoka uwanjani, mashabiki wengi walikuwa wakilaumu kwamba Simba haina lolote, hata wachezaji waliosajiliwa ni bure na kusisitiza kwamba ‘wamepigwa changa la macho’ kwa kuwa Simba itaendelea kuwa inayoyumba kama misimu miwili iliyopita.

Asilimia 80 ya mashabiki wa Simba waliokuwa uwanjani hapo wameshindwa hata kung’amua kwamba pamoja na Zesco kutoka katika nchi iliyopiga hatua zaidi kisoka, lakini walikuwa tayari na wanashiriki ligi, tofauti na Simba iliyojaza wageni na sasa ndiyo imeanza kujipanga.

Aliyewashauri Simba wailete Zesco wamshukuru. Kwani hata kama wamepata kipigo, lakini watakuwa wameona matundu na namna ya kuanza kuyaziba na hii itawasaidia kuwa bora zaidi.

Kuona mapema makosa au ulipoteleza inakuwa ni bora zaidi kwa kuwa utapata muda wa kujirekebisha kwa nafasi na ikiwezekana kwa sasa, Simba wanahitaji mechi nyingine ya kirafiki ndani ya wiki mbili.

Katika mechi inayofuata, Loga anaweza kutumia kipimo kuangalia wingi wa makosa katika mechi ya kwanza na hiyo atakayocheza, kwamba yanapungua au kuongezeka.

Wakati matamasha zaidi yanalenga kuingiza fedha, inawezekana badala ya mipango ya kuuza jezi kwa wingi au kuingiza fedha nyingi kupitia haki za runinga, viongozi wetu wanabuni matamasha kama hayo, kujiingizia kipato ili kupunguza makali ya uendeshaji wa timu.

Kocha kama mtaalamu si wa kulaumiwa katika kipindi hiki, badala yake apewe nafasi ya kumaliza maandalizi ya kikosi chake na kukifanya imara kama anavyotarajiwa na Zesco imekuwa msaada kusaidia kurekebisha upungufu uliojitokeza.

Mashabiki waliolalamika, huenda kweli hawaelewi, lakini wanapaswa kujifunza na kukubaliana nami kwamba, ukiangalia rekodi ya matamasha ya Simba Day, Simba imepoteza mechi zake za siku hiyo kwa asilimia 90.

Hivyo ni timu inayocheza ikiwa haijakamilika. Ndiyo maana nikawa najiuliza, kama Simba ‘wamemaindi’ hivyo, unafikiri Maximo angekubali kuingiza timu mapema? Yanga wangevumilia mikwaju hiyo mitatu ya Zesco halafu wakae kimya!

0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic