September 15, 2014



WAKATi ikiwa imebaki wiki moja kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu Bara, hisia za mambo mengi kujitokeza linaweza kuwa jambo la kawaida kabisa.


Lakini maswali ya nini kitatokea ni kawaida pia kwa kuwa inapoanza ligi, mambo yanaanza kujitokeza na ndiyo burudani yenyewe.

Kizuri, hakuna ligi ambayo humalizika bila kuacha funzo au gumzo. Kunakuwa na mengi ya kujifunza kwa kuwa katika mechi 36 kwa kila timu kuna mengi yanayotokea.

Katika udhaifu ambao umekuwa ukizidi kuutafuna mpira wa Tanzania ni watu kuendelea kupenda Yanga na Simba pekee wakasahau hata timu zinazotoka kwenye mikoa ya asili yao.

England ambao tunataka kuwafuata au tunafurahia kujifunza kwao, watu hupenda timu kutoka katika maeneo yao. Hakuna ubishi mtu wa Mbeya ana haki ya kuipenda Mbeya City na wala asione haya.

Kuipenda Yanga ama Simba si dhambi, lakini si lazima. Kama wewe ni Chinga, Ndanda FC imepanda, sasa huu ndiyo wakati wako wa kuonyesha upendo na hauna sababu ya kuwa na woga.

Kweli timu hiyo inaweza isikufurahishe sana kwa kuwa haina uwezo wa kuwasajili akina Paul Kiongera au Coutinho kutokana na uwezo wake kifedha, lakini tukubaliane zinahitaji kukua.

Kukua kwake kunahitaji fedha kwa ajili ya kuziboresha na kusajili wachezaji wa kiwango cha juu. Hawawezi kupatikana bila fedha na ili fedha iingie, lazima kuwe na ushirikiano na mapenzi ya dhati.

Tumeona Mbeya City na wala msione haya kuwatolea mfano kwa msimu wao mmoja uliopita kwamba watu walikuwa tayari kuona timu yao inapata mafanikio na ndiyo maana ikafikia hapo, ndiyo maana kuna watu wamekuwa tayari kuingiza fedha zao kwa Mbeya City.

Wako wengine ni wafanyabiashara jasiri kama vile Bin Slum Tyres Ltd ambaye amekubali kuingiza fedha zake hadi Ndanda FC na Stand United ambazo ndiyo zimepanda daraja na hazina lolote.

Mfanyabishara yeyote lazima awe makini kwenye matumizi ya fedha anazoingiza. Kwa Ndanda au Stand lazima awe na hofu kwa kuwa hajaona wanachofanya kwenye ligi kuu.

Lakini Bin Slum amefumba macho na kuwapa udhamini, maana yake anawaonyesha viongozi, wanachama na mashabiki wa klabu hizo kuanzia mikoani mwao au kwingine kuwa wanapaswa kujitolea kwanza ili kuhakikisha zinakuwa na mafanikio kwenye msimu wa kwanza wa Ligi Kuu Bara.

Wasitake mafanikio ya haraka kama Mbeya City au kulazimisha mambo, badala yake angalau wabaki ligi kuu lakini uwezekano wa kufanya vizuri zaidi upo.

Toto African kwa Mwanza ilionekana ni kama timu ya upande fulani, wengine wakaipiga vita kwa juhudi kubwa na sasa hawawezi kuona mechi za Ligi Kuu Bara kwa kuwa Mwanza hakuna timu, kitu ambacho ni upuuzi mkubwa.

Yaliyotokea kwa Toto inawezekana kabisa yatatokea Shinyanga na hata kule Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara kwa timu hizo mbili kunusa ligi kuu na kuteremka kama wananchi wake hawatakuwa imara na kuonyesha mapenzi.

Kuzipenda Simba na Yanga na kuisahau timu ya mkoani kwenu hasa ukiwa unaishi hapo, si sahihi. Hiyo ndiyo inayokusaidia kuzileta timu hizo za ligi kuu ukaiona ukiwa hapo nyumbani.

Wanaoweza kuzimaliza Ndanda na Stand United watakuwa ni watu wa Mtwara na Shinyanga na si zaidi. Na tayari nilipokuwa Shinyanga niliona kuna mgawanyiko kati ya Mwadui na Stand.

Lakini kuna kila sababu ya kuamini uzalendo ni jambo namba moja na kama ni suala la mapenzi kwa Yanga na Simba, basi lifuatie na nguvu za mapenzi ziwe kwa kile kilicho nyumbani kwenu na hii itazifanya Yanga na Simba, zisikie joto la ushindani na wakati mwingine kujiimarisha zaidi kuliko kuchukulia mambo rahisi kama zinavyofanya sasa.


0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic