September 20, 2014


Na Saleh Ally
MAKAO makuu ya Yanga ni pale makutano ya Jangwani na Twiga jijini Dar es Salaam, historia inaonyesha ujenzi wa jengo hilo ulianza baada ya viongozi wa Yanga kutaka kufanya ukarabati kwenye jengo lao la Mafia.

Kutokana na kutokuwa na fedha, wakafikisha ombi kwa Rais wa Zanzibar, Abeid Amani Karume na kumueleza kuhusiana na ukarabati wanaotaka kuufanya kwenye jengo lao la Mafia. Naye akawataka wafunge safari hadi Zanzibar wakati wa sikukuu ya Pasaka ambayo alikuwa akiwaalika kama kawa.
 Lakini Karume akatoa wazo kwamba Mwenyekiti wa Yanga Kondo Salum Kipwata na katibu wake waende Zanzibar wakiongozana na kiongozi wa Sunderland (sasa Simba), wakakubali.
Wakati huo Mwenyekiti wa Sunderland alikuwa ni Ramadhani Kirundi, aliongozana na Kipwata na katibu wake hadi Zanzibar na wakasherekea pasaka pamoja na baada ya hapo wakaingia katika mazungumzo ya suala la zile fedha za ukarabati wa jengo.
Karume aliwaambia kuwa amesikia walichotaka, akawaambia alikuwa na wazo la kujenga jengo moja ambalo Young African na Sunderland wangelifanya makao makuu yao. Wazo hilo lilipingwa vikali na Kirundi aliyewahi kushika nyadhifa mbalimbali za mkoa wa Dar es Salaam, ikiwemo nafasi ya Meya wa mji huo.

Kutokana na msimamo wa Kirundu, Karume aliamua kutoa kiasi cha Sh milioni 2 ambazo Young African ilianza kuzitumia kwa ujenzi wa makao makuu ya klabu hiyo pamoja na Uwanja wa Kaunda.
Hata hivyo haikuwa lahisi baada ya zengwe kuibuka na Manispaa ya Jiji kupitia wataalamu wake wa ujenzi walisema haikuwa sahihi kujenga ghorofa katika eneo hilo lingeweza kuanguka na pia eneo hilo lilitengwa maalum kwa ajili ya jalala.
Kutokana na zengwe kuwa kubwa, kwa mara nyingine, Rais Karume aliingia suala hilo kwa kufikisha taarifa yake kwa Ikulu ya Tanzania Bara na siku chache baadaye akasafiri hadi Dar es Salaam akiongozana na mainjinia wa ujenzi kutoka nchini Ujerumani.
Aprili 4, 1971, Wajerumani walikamilisha suala la kupima na kuweka msingi na Mwananchi Engineering Contracting Company ndiyo ikafanya ujenzi huo.
Hata hivyo, wakati jengo linaanza nafasi ya usimamizi ikawa chini ya MWenyekiti Mangara Tabu Mangara baada ya Kipwata aliyafanya pilika zote za uongozi kufanikisha hilo, kufariki dunia.

Magari:
Achana na jengo tu au watu wengi kuona Yanga inamiliki basi ambalo limetokana na udhamini, lakini wakati huo chini ya Mangara, Yanga ilimiliki magari kadhaa.
Yanga ilikuwa na basi dogo aina ya Ford kwa mkoa wa Arusha ilijulikana kama ‘Viford’, lilikuwa lina uwezo wa kubeba abiria 30, pia ilikuwa na basi kubwa aina ya Isuzu lililochukua watu 65, pia gari ndogo aina ya Honda.
Hii inaonyesha kiasi gani Yanga iliendelea kuwa na utajiri mkubwa chini ya uongozi wa Mangara ambaye alikuwa mmoja wa viongozi imara waliowahi kupita Yanga.
Jengo la Mafia:
Hili ndiyo jengo kongwe zaidi kwenye klabu ya Yanga, kabla ya kupatikana kwa jengo hilo, Yanga ilikuwa ikifanya kazi ya kuhama sehemu moja kwenda nyingine tokea ikijulikana kama New Youngs na hata baadaye ‘Simba’ walipojitenga, nao wakapanga pia.
Kutokana na hali hiyo, Mwenyekiti Jabir Katundu akaamua kubuni mpango wa kupata nyumba ambayo itakuwa makao makuu ya klabu. Ukafanyika mkutano na makubaliano yakafikiwa kualika timu kutoka Kenya.
Ikaalikwa Abaluhya ambayo ilikuwa kali na inakubalika. Ikatua na kucheza na Yanga na mapato yote, hata wachezaji hawakupewa posho, yakatumika kununua kiwanja na baadaye kuanza ununzi wa nyumba ya Mtaa wa Mafia.
Nyumba ya Mafia ilikuwa ya Sunderland, ndiyo mashabiki wa Yanga walizoea kusema wakati huo, lakini ukweli ni kwamba nyumba ile ilikuwa inamilikiwa na shabiki na mwanachama wa Sunderland.
Shabani Feruzi ndiye alikuwa mmiliki wa nyumba hiyo kwa jumla ya Sh 17,000 tu. Mmiliki alichukua Sh 13,500 na zilizobaki zilitumika kuwalipa madalali pamoja na wengine waliohakikisha ununuzi unafanikiwa.
Katika mechi dhidi ya Baluhya, Yanga ilipata fedha nyingi sana, zilikuwa ni Sh 21,300. Hivyo fedha nyingine zikatumika katika mambo mengine ya maendeleo ikiwa ni pamoja na kupaka rangi za jengo na kuindoa nyeupe na nyekundu aliyokuwa amepaka mmiliki wa awali ambaye ni mnazi wa Sunderland.


Historia ya Yanga:

Young African ina historia ndefu lakini ukweli ndiyo klabu ya kwanza ya Waafrika ambayo ilijiimarisha na baadaye kuwa mfano kwa nyingine.
Ilianzishwa mwaka 1935 kwa jina la New Youngs, makao makuu yake yalikuwa pale Mwembe Togwa, kwa mara ya kwanza ikasajiliwa rasmi Februari 12, 1935.
Mwembe Togwa kwa sasa ni maarufu kama Fire, Kariakoo. Kutokana na kusaka maendeleo, New Youngs ilikwenda inahama taratibu hadi ilipobadilishwa jina na kuwa Young African, siku kadhaa baada ya wengine kujitenga na kuanzisha klabu ya Stanley ambayo baadaye ilikuja kuwa Sunderland halafu Simba.
Wakati inaanzishwa ilikuwa klabu pekee ya Waafrika hasa wazalendo wenye maisha ya kawaida, Waafrika wachache walijichanganya kwenye klabu za Wazungu na Waasia kama Aga Khan, Goans Club, European Club na Yatch Club na ilipozaliwa Sunderland ndiyo ikawa klabu ya pili ya weusi.
Wakati huo kiongozi mkuu wa klabu ambaye sasa ni mwenyekiti, aliitwa Patron na rekodi zinaonyesha mwenyekiti wa kwanza ni Athumani MWinyichande na katibu wake ni Mwichande Chonjo.
Maisha ya makao makuu ya klabu yalikuwa ni ya kutangatanga, baada ya kutoka Mwembe Togwa, klabu ilihamia Mtaa wa Udowe/Sikukuu, halafu ikahamia Sikukuu/Mafia na baadaye Mtaa wa Lumumba.
Juhudi zikafanyika kwa mchango wa mechi moja, uongozi ukafanikiwa kununua nyumba yake pale Mafia. Halafu ndipo zilipotolea fedha la Rais Karume mpango wa kujenga makao makuu na Uwanja wa Kaunda ukafanyika, sasa nyumbani kwa Yanga ni mtaa wa Twiga na Jangwani.







0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic