September 8, 2014




Na Saleh Ally
YANGA ni klabu iliyoshiriki kwa nguvu katika kutafuta Uhuru wa Tanganyika ambao baadaye ulipatikana mwaka 1961 na kujiondoa kwenye mikono ya Waingereza waliokuwa watawala.


Sehemu moja ya kuonyesha kuwa kweli Yanga ilishiriki ni nembo yake ambayo hadi leo imekuwa na alama ya Bara la Afrika ikiwa ni sehemu ya kusisitiza kuwa Waafrika wanapaswa kujitegemea bila ya kuongozwa na watu kutoka nje ya bara hilo.

Wakati wa utawala wa kikoloni, hakukuwa na nafasi ya kutosha kwa Waafrika kusimama na kujieleza kuhusiana na walichotaka kwa uwazi, badala yake mambo mengi yalilazimika kufanyika kwa siri kuhofia adhabu kutoka kwa wakoloni.

Jina la Young African ilikuwa ni sehemu ya dhana, kwamba linawabeba Waafrika vijana, hivyo ikawa rahisi kuihusisha klabu na wazalendo waliokuwa wakitaka kwa dhati uhuru wa nchi yao ambao ulikuwa lazima upiganiwe.

Kuanzia mwaka 1951, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, alikaribishwa na wazee waliokuwa Yanga na walikuwa tayari kushirikiana naye. Baadhi yao ni akina Dunstan Omar, Sheikh Suleiman Takadir, Idd Faiz Mafongo, Ally Sykes, Abdulwahid Sykes, Juma Sultan ‘Mabosti’, Said Chaurembo, Sheikh Jumbe Tambaza, Bibi Titi Mohammed, Tatu Binti Mzee na wengine wengi.


Wakati huo Nyerere alikuwa mwalimu katika Sekondari ya St Francis (sasa Pugu), mikutano ilianza kufanyika kwenye makao makuu ya Yanga ikiwa inahamasisha Watanganyika kuzungumzia unyonge wao ndani ya nchi yao na baada ya hapo kuanza kudai uhuru.

Mkutano hiyo haikuwafurahisha wakoloni hata kidogo, mara nyingi walituma mashushushu na kutaka kujua kilichokuwa kikiendelea ndani. Lakini Nyerere na wenzake wa Yanga waliamua kubuni mbinu tofauti kuwakwepa.

Kwa kuwa hakukuwa na ujanja wa kuhama katika eneo hilo na kufanya mikutano kwingine, mbinu mbadala moja wapo ilikuwa ni kukifanya kikundi cha taarabu cha Jipisheni kuendelea kutumbuiza kila walipoanza vikao.

Kikundi hicho ambacho baadaye kilipewa jina la Egyptian Musical Club, kiliendelea kutumbuiza huku watu wakishangilia kwa nguvu. Ingawa kelele zilikuwa juu, lakini Nyerere na wanachama wengine wa Yanga ambao pia walikuwa wanachama wa Tanu waliendelea na mikutano yao kuhakikisha wanafikia malengo.

Mwasisi wa kikundi hicho cha taarabu, Maalim Bom Hambaroni, yeye alijitolea ikiwa ni sehemu ya mchango wake na wanamuziki wa kikundi hicho wakakubaliana na hilo kila mmoja akiwa amepania kuona siku moja wanakuwa huru.

Baadhi ya wanamuziki wa kikundi hicho na wanachama wa Yanga walipokezana kuimba huku wengine wakipika chakula ambacho Nyerere, viongozi wa Yanga na wanachama wa Tanu walikula na baadaye kuendelea na vikao vyao hivyo vya ukombozi wa Tanganyika.

Mara kadhaa, katika baadhi ya mechi, klabu ya Yanga ilitoa kiasi cha fedha na kuhakikisha kinaisaidia Tanu katika mambo yake kadhaa ya kichama kwa lengo la kufanikisha upatikanaji wa uhuru.

 Kutokana na ushirikiano wa juu aliokuwa akiupata kutoka Tanu na Yanga, Nyerere aliamua kuacha kazi yake ya kufundisha ili apate nafasi ya kutosha kupambana kusaidia kupatikana kwa Uhuru wa Tanganyika.

Alianza kuzungumza kila sehemu Tanganyika, dereva akiwa ni Said Tanu, ambaye alikuwa shabiki wa ‘kulia’ wa Yanga na aliwahi kueleza kwamba nje ya siasa, mwalimu alizungumza sana kuhusu mpira na Yanga ndiyo iliyokuwa ikiukosha moyo wake.

Baadaye kwa ushirikiano wa Tanu, wananchi wengi, Nyerere alifanikiwa ku       ipatia Uhuru wa Tanganyika, rasmi Desemba 9, 1961.

Uhuru wa Zanzibar:

Uhuru wa Zanzibar pia Yanga ilishiriki kwa kuwa mwanamapinduzi namba moja, Abeid Amani Karume alikuwa anapenda sana mpira na ndiye mwanzilishi wa klabu ya African Sports ya Zanzibar.

Wakati fulani hata kabla ya uhuru wa Tanganyika, viongozi wa Yanga walialikwa Zanzibar na Karume. Wakiwa kule Yanga na African Sports, wakafanya mkutano wa kutaka kudumishwa undugu kwa watu wa Bara na wale wa visiwani.

Mikutano ilikuwa miwili, mmoja ulifanyika Zanzibar na mwingine ukafanyika Dar es Salaam, lengo lilikuwa ni hilo kusaidia kupatikana kwa Uhuru wa Tanganyika pia Zanzibar.

Mfano timu hizo ziliandaa mapambano mawili, moja likachezwa visiwani na fedha zikaichangia ASP kuendelea kupambana dhidi ya wakoloni, halikadhalika mechi nyingine ikapigwa Bara na fedha zikaisaidia Tanu kwa lengo lilelile.

Katika mechi iliyochezwa Kajengwa Makunduchi, Zanzibar na ile ya Ghymkhana (sasa Karume), watazamaji walikuwa wakiingia wanalipa kwa kuweka fedha kwenye vibubu moja kwa moja ili kudhibiti mapato.

Ndiyo maana hata baada ya Zanzibar kupata uhuru, Karume alikuwa akizialika ikulu klabu za Yanga, Simba, African Sports ya Tanga na ile ya Zanzibar kwenda kusherekea sikukuu mbalimbali kama pasaka au Idd.

Kwa hayo hii ni sehemu ya kuonyesha Yanga ilishiriki kwa kiasi kikubwa kupatikana kwa uhuru wa Tangayika, Zanzibar au Tanzania kwa ujumla na ndiyo maana ilipewa jina la timu ya wananchi.

Muungano:

Yanga inaelezwa kuwa sehemu iliyochangia kwa kiasi fulani kupatikana kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar ambao ulizaa Tanzania. Maana ndiyo zilichangia Nyerere na Karume kuwa karibu na suala la kuungana likaanza.

Kwa kuwa Nyerere na Karume, wote waliamini jambo moja kuwa kuungana ni kuongeza nguvu, hivyo waliweza kuzungumza kwa urahisi zaidi kwa kuwa waliona walikuwa na sera zinazofanana.

Hivyo suala la muungano halikuwa na ugumu na ikawa pia lahisi kwa Tanu na ASP kuungana na kutengeneza Chama cha Mapinduzi (CCM).

SOURCE: CHAMPIONI



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic