September 8, 2014


SOKA lina historia ndefu sana, kwa hapa Tanzania ni nadra kukuta mtu anaingia hivihivi katika ngazi ya utawala pasipo kupitia uchezaji. Ni wachache sana, hususan kwa timu kubwa za Yanga na Simba. Viongozi waliopo wengi, wao wana historia kubwa katika klabu zao.


Na mmojawapo ni Ibrahim Akilimali, maarufu kama mzee Abramovich, ambaye anasema kama ingekuwa inawezekana hata kupitia maombi, basi angekesha akimuomba Mwenyezi Mungu damu yake aifanye iwe ya kijani. Ni shabiki, mwanachama na mnazi wa kutupwa wa Klabu ya Yanga.

Jina la Abramovich amepewa kupitia lile la bilionea wa Kirusi, Roman Abramovich anayeimiliki Chelsea. Akilimali si tajiri, lakini moyo wake ni wa utajiri kwa klabu yake ya Yanga na hasa mapenzi makubwa aliyonayo.


Abramovich, hakuwahi kucheza soka maishani mwake, pengine wengi wangejiuliza, aliingiaje kwenye himaya ya Yanga mpaka anakuwa mmoja wa viongozi wenye umaarufu klabuni hapo, akiwa kama Katibu Mkuu wa Baraza la Wazee wa Klabu ya Yanga?

Ana historia ndefu katika maisha ya soka hadi kufikia leo hii kutambulika kama Abramovich anayefahamika kwenye vyombo vya habari kutokana na umaarufu wake wa kuisifia Yanga. Katika mahojiano maalum na Championi Jumatatu, ameeleza mengi likiwemo suala la tambiko kwa timu kabla ya kucheza mechi.

Historia yake katika soka:
“Jina langu kamili, naitwa Ibrahim Omary Akilimali, mzaliwa wa Kigoma. Historia yangu katika suala zima la soka, mimi ni mmoja wa wapenzi na wanachama wa mwanzo kabisa wa Klabu ya Young African Sports Club, tangu mwaka 1956. Kuna sababu kuu mbili zilizonifanya niipende Yanga yapata miaka 58 sasa.

“Mosi, ni neno ‘Afrika’. Tangu zamani mimi nilipenda kudumisha na kuutukuza Uafrika wangu, kipindi hicho nilikuwa mfuasi na mwanachama wa Chama cha Tanu (Tanganyika African National Union), ambacho baadaye kiliipatia Tanganyika uhuru wake mwaka 1961.


“Niliingia katika chama cha Tanu mwaka 1955, mwaka mmoja baada ya kuundwa kwa chama hicho. Hivyo kukawa na thamani na kulikuza neno Afrika. Wakati nikiwa bado Kigoma, nilikuwa nikisikia kuna timu inaitwa Young African Sports Club, kwa hiyo nikawa nimependezewa sana na neno African, nikaona ilikuwa ni sehemu muhimu ya kuukuzia Uafrika wangu, ukawa ni mwanzo wa kuipenda Yanga.

“Sababu ya pili, baba yangu alikuwa ni mfuasi mkubwa wa neno Afrika pia akiwa ni mpenzi mkubwa wa Klabu ya Yanga, kwa hiyo na mimi nilirithi mapenzi. Hizo ndizo sababu za mimi kuwa Yanga damu mpaka sasa.

Aliingiaje Yanga?
“Mpaka mwaka 1962, nilikuwa mpenzi tu, hata kabla ya kuja Dar es Salaam. Nimekuja hapa Dar mwaka 1966 na kupata kazi bandarini mwaka 1967 kama Kuli. Zamani viongozi na wamiliki wa bandari walikuwa ni wanachama wa Yanga, hata wachezaji ambao hawakuwa na kazi basi waliunganishwa kufanya kazi bandarini. Mwaka 1972 nilipata kadi yangu ya uanachama wa Yanga hadi leo hii. Miaka 42.”

Milima na mabonde aliyopitia:
“Nimepitia mengi, migogoro ya hapa na pale ya klabu yangu. Kwanza kabisa zamani klabu hazikuendeshwa kwa sheria za TFF, ziliendeshwa na wazee (kwa Yanga kulikuwa na Baraza Tochi), kwa hiyo kulikuwa na changamoto kadha wa kadha…mara huyu kiongozi kung’ang’ania madarakani, ooh.. wanachama waukatae uongozi fulani, watu walipigana hovyo.

“Lakini mimi nilikuwa mfuasi wa kufuatilia chanzo cha mgogoro na kuhakikisha tunapata suluhu. Tumekwenda hivyo na migogoro kama hiyo ndiyo ilipelekea kuundwa kwa timu ya Pan Africa. Haikuundwa hivihivi, bali lilikuwa ni zao la migogoro ndani ya Yanga enzi za utawala wa mzee Tabu Mangara, hadi Mkuu wa Wilaya ya Ilala wakati huo, Kunambi akaingilia kati lakini mwisho wa siku tukamuangusha.

“Watu wake wa karibu wakamshauri kwamba hawezi kutoka hivihivi Yanga, ndipo wakajiunga na timu ya Jogoo huko Morogoro na baadaye kuunda timu iliyoitwa Pan African. Na wachezaji wote wa Yanga kama Sunday Manara, Kitwana Manara wote wakajiunga na timu hiyo.”

Historia ya Baraza la Wazee Yanga:
“Wakati naingia kama mwanachama wa Yanga 1972, kulikuwa na Baraza la Wazee lililoitwa Baraza la Tochi. Kazi yake kubwa ilikuwa ni kumulika na kuchunguza maadui wa Yanga. Wajumbe wa baraza hili walikuwa ni watu wazima, wazee na wasiri sana, ambao walihusika na kutoa taarifa sahihi kwa uongozi kuhusu wabaya na wahujumu wa klabu yao.

“Baadaye neno tochi likafifia, likabakia jina Baraza la Wazee. Wajumbe wa baraza hili ni lazima wawe wazee na hawa ndiyo wenye kuijua Yanga na miiko yake, ndiyo maana lipo mpaka sasa. Kutokana na kazi yake, kwani wazee ndiyo wanaijua Yanga kwa undani zaidi.”

Aigawa Yanga
Kutokana na migogoro, mwaka hadi mwaka, Abramovich ambaye kwa sasa ni katibu wa Baraza la Wazee, anasema alikuwa kiongozi katika kuikataa Yanga kufanywa mali ya kampuni, enzi za utawala wa Jabir Katundu.

“Alikuwa na siasa nzuri za kimaendeleo, lakini kutokana na upeo wetu mdogo sisi tulikataa timu yetu kuwa mali ya kampuni, mvutano ukatokea mpaka tukaamua kuunda Yanga Asili, nikishirikiana na Salum Mwaipande.

“Tuliushitaki uongozi uliokuwa madarakani (Jabir Katundu na katibu wake George Mpondela) kwa sababu hatuhitaji Yanga ifanywe kampuni. Migogoro ya namna hiyo imekwenda mpaka 2006, tulipompata Yusuf Manji aliyetupatanisha na kuitoa Yanga Asili mpaka Yanga tunayoiona leo hii.

“Hatukujua faida yake, baadaye nilikuwa wa kwanza kutia saini wakati Yanga inafanywa kampuni wakati wa utawala wa Abbas Tarimba na Francis Kifukwe.”

Hee..! kumbe Fat ni zao la Yanga!
“Anasema Yanga ilikuwa zao la kuundwa kwa Chama cha Soka Tanzania (Fat, sasa TFF) ingawa hakutaka kulizungumzia kwa kina. “Kwa kifupi, ni kwamba Yanga ndiyo ilikuwa timu ya kwanza kuileta Gor Mahia (ya Kenya) hapa nchini, ilikuwa na wanachama na wapenzi wa Yanga, hivyo walikuja hapa kucheza mchezo mmoja, katika mapenzi hayo, ndiko kukaanzishwa kwa vyama vya soka kama Fat.”

Halipwi hata senti Yanga:
Akieleza mafanikio yake ya kuwa mwanachama na mwanaharakati wa maendeleo ya Yanga, Abramovich, anasema halipwi chochote, bali mafanikio yake siku zote ni furaha ya ushindi, basi. “Mafanikio yangu kwa Yanga ni furaha tu basi, siyo kingine. Kwa mfano, tunapomfunga mtani wetu Simba, basi ninafurahi sana. Lakini siyo kusema kutokana na kuipenda kwa miaka yote hiyo na kuwa karibu nayo kiasi hicho, labda kuna mshahara napewa. Silipwi hata senti tano.”

Aomba Mungu ampe damu ya kijani
“Kiukweli kama ingekuwa inawezekana kwa Mwenyezi Mungu, ningemuomba anibadilishie damu yangu kutoka nyekundu, aifanye ya kijani au ya njano.”

“Hii inatokana na mapenzi yangu kwa Yanga ambayo inatumia rangi za kijani, njano na nyeusi. Rangi nyekundu ni Simba.”

Kutana na Kamati ya Miziziology

Ni kama jambo la kushtua lakini huo ndiyo ukweli, kwamba Yanga haiwezi kuanza ligi bila kufanyiwa tambiko. Mzee Abramovic amefunguka mkanda mzima.

“Yanga kuna kamati mbili. Kamati Kuu ya Utendaji na Kamati Kuu ya Utendaji ya Miziziology. Kamati hii huendeshwa na wazee na huteuliwa na mwenyekiti wa kamati ya utendaji ambaye anamteua mzee mmoja kuwa kiongozi wao.

“Kazi yake kuu ni kutunza tamaduni na miiko ya klabu, pamoja na kufanya tambiko kwa timu kabla ya kuingia kwenye ligi, kusoma dua kwa marehemu wazee wote walioanza kuiongoza Yanga pamoja na kufukiza ubani. Pia hujishughulisha katika kuimarisha urafiki kati ya Yanga na timu nyingine, maana wao ndiyo wana kumbukumbu, historia ya klabu yetu.”

Maana ya Miziziology:
“Wewe hujawasikia waganga? Hujawahi kuona timu inakwenda uwanjani na kuku au paka au pengine mnyama anapita katikati ya uwanja wakati mchezo unaendelea? Miziziology ni utamaduni wetu ambao tumeuzoea wa kufukiza ubani, hata Ulaya na Kombe la Dunia vitu hivi tuliviona. Kwa kifupi Miziziology ni utukuzaji na utoaji wa baraka za kimila kwa timu.”

Tukio ambalo hawezi kulisahau
“Sitasahau siku ambayo nilituhumiwa kuwa nilikuwa naisemea timu, mwenyekiti Manji alipowauliza wanachama wanichukulie hatua gani na wanachama wakamtaka anifukuze uanachama. Kiukweli niliumia kupita maelezo kusikia kauli ile. Yaani na miaka yangu yote tangu niipende Yanga na jinsi nilivyoipigania mpaka leo hii, nilihuzunishwa sana na kauli ya wanachama wenzangu. Lakini namshukuru Mungu yote yalikwisha, lakini mpaka nafukiwa chini, sitasahau kauli za watu wale.

“Nashukuru sana kwa kuwa Manji alilikataa ombi lile na kuonyesha kunidhamini, pamoja na kuumia, mimi ni mtu mzima, naendelea kuipenda Yanga na pia naweza kusamehe ingawa maumivu yaliumaliza moyo wangu.”
Ishu ya ‘logo’ nyekundu
“Ni kweli sisi baraza tulishinikiza kukataa logo nyekundu (ya wadhamini wa Ligi Kuu Bara, Vodacom). Tangu zamani tangu Yanga ianzishwe 1935, piga ua, rangi nyekundu haiwezi kukanyaga Yanga. Na Simba hivyohivyo, piga ua haiwezi kuvaa rangi ya kijani au njano.

Maamuzi yoyote ya kamati ya utendaji lazima yapite kwa wazee.
Anasema maamuzi yoyote yale ambayo kamati kuu ya utendaji itafikia kabla ya kutekelezeka, ni lazima yapite kwa baraza la wazee na kuomba ushauri. Kama baraza litaona jambo hilo ni baya, tunawashauri na kutoa tathmini ya ubaya wa kitu hicho au kuketi chini na kamati kuu na kufikia maridhiano pande zote.”

Akunwa na Manji, Katundu
Amefanya kazi na viongozi mbalimbali lakini anasema uongozi wa Jabir Mohammed Katundu na uliopo madarakani kwa sasa chini ya Yusuf Mehbub Manji hauna kifani.

“Siwezi kusahau kazi ya Katundu miaka ya 1970. Uongozi ambao ulijenga jengo la makao makuu ya klabu (Mtaa wa Twiga na Jangwani). Alikuwa jasiri na mpenda maendeleo ya Yanga, alijitosa mbele ya Rais Karume na kumuomba fedha kisha akaijengea Yanga makazi ambayo mpaka sasa wanatumia. Pili, ndiye aliyejenga Uwanja wa Kaunda, ambao mpaka sasa umeshindwa kuendelezwa na viongozi wanaoingia madarakani.

“Manji kila mtu anaona juhudi zake na pengine unaweza kuwa uongozi bora kuliko wote kutokana na juhudi zake ambazo amekuwa akionyesha, akitaka timu iwe ngazi za kimataifa.”  

Manji ampa jukumu jingine
Kutokana na harakati zake za kuiendeleza Yanga, Abramovich anasema jukumu kuu ambalo amekabidhiwa rasmi ni kutoa hamasa kwa wanachama kuelekea mchezo husika na kwa sasa kuna jukumu jingine amepatiwa lakini ni mapema sana kulitaja.

Duh…! Wajukuu 32

Mzee Akilimali ni babu wa wajukuu 32 katika watoto wake wanne aliobahatika kupata. Watatu wa kiume na mmoja wa kike aliowazaa na wake zake watatu lakini kwa sasa ana wake wawili.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic