October 22, 2014



Na Saleh Ally
MIAKA kumi iliyopita, msanii aliyekuwa anatamba sana, anayefanya shoo au kusafiri Marekani na barani Ulaya alikuwa ni Joseph Mbilinyi, wakati huo akijulikana kama 2 Proud kabla ya kuamua kubadili jina na kuwa Mr II.


Ukiachana na wale ‘watoto wa mama’ kutoka maeneo ya ‘uzunguni’, Mr II alikuwa kati ya vijana wa kwetu uswahilini waliokuwa wanavaa raba mtoni, cheni kali kama Public Enemy, miwani kama ya Jay Z, pozi utadhani Notorious BIG, kitambaa kama kile cha 2 Pac Shakur, lazima ungefurahi kukutana naye.

Hata iwe vipi, hakutakuwa na njia ya kukwepa mchango mkubwa wa Mr II katika muziki wa kizazi kipya hasa kutokea kipindi kigumu cha mapinduzi hadi ulipo sasa. Vipi alionekana hafai, kuna mambo mengi sana pamoja na hali halisi.

Hakuna anayeweza kubisha kwamba wako waliochukizwa na mafanikio ya Mr II ambaye sasa anajulikana kama Sugu. Pia hakuna ubishi, kuna ‘wakubwa’ ambao hawakutaka aendelee kutamba kutokana na kuwa na nguvu kubwa ambayo iliwasumbua na kusaidia kuwaamsha wengine.

Kwa jumla iko hivi, Sugu aliporomoka kutokana na vitu vitatu vikuu. Kwanza muda wenyewe, wakati wa wengine kuchukua nafasi uliwadia, pili; ‘wakubwa’ hawakutaka aendelee kutamba na kuwa na nguvu kubwa iliyowasumbua, tatu; roho mbaya, maana wapo ambao hawamkupenda tu, ukiwauliza kwa nini wanamchukua, jibu lao ni “basi tu!”

Msanii mwingine wa kizazi kipya ambaye ikifikia siku ameshuka kisanii, basi tutasema alikuwa na mchango na hatuwezi kuukwepa ni Nasib Abdul ‘Diamond’. Amefanya kazi nzuri, amepiga shoo nyingi Ulaya na Marekani, amekuwa gumzo barani Afrika.

Ajabu wikiendi iliyopita kwenye tamasha la Fiesta, alizomewa sana hadi kufikia kuahirisha shoo huku mwenyewe akilalama kuwa kuna jambo au mpango wa kummaliza.

Siwezi kuchangia kwenye hilo kwa kuwa si rahisi kung’amua, lakini haja ya yeye kujiuliza kwamba vipi watu wa Temeke, Ilala, Kinondoni na mikoa jirani wamzomee kwa pamoja!

Kabla ya kuingia ndani kwenye kuchangia unaweza kusema Diamond mchango wake hautakwisha pia kama ilivyo kwa Sugu kwa kuwa yako yale makubwa ameyafanya.

Utaendelea kukumbukwa ingawa kwa sasa tunapaswa kujiuliza, msanii huyo anaweza kukwepa sababu tatu zilizomporomosha Sugu ukijumlisha moja ambayo Sugu hakuwa nayo, lakini Diamond inamsumbua?

Muda:
Hakuna ujanja, ukifikia wakati Diamond atashuka tu kwa kuwa kwa tabia ya kila binadamu, hufikia wakati anahitaji kusikiliza vitu vipya na si vile vya zamani ambavyo huonekana ni ‘vya kila siku’.

Wakubwa:
Hawa ni tatizo kwa kila msanii, walimshusha Sugu kwa nguvu, wakampandisha Profesa Jay, naye wakamshusha na kumpandisha mwingine wakitumia nguvu yao lakini lengo hasa linakuwa ni maslahi yao na si ya sanaa au wasanii wenyewe.

Kitu kibaya wakati msanii mmoja anashushwa, anayepandishwa huchekelea kwa kipindi hicho akiwa amesahau msemo wa ‘mwenzako akinyolewa.’

Chuki:
Nani anakataa kuwa sisi binadamu tumeumbwa na husda, hatupendani na wachache wanaobaki kuwa watu wazuri hujizuia na kupambana na tabia hiyo. Wako wasiompenda Diamond kutokana na mafanikio yake, bila sababu za msingi.

Wanaomchukia hawajui kwa sababu gani na inawezekana katika wanaomchukia ni kwa kuwa msichana au mpenzi wake ameonyesha kuvutiwa sana na msanii huyo. Basi bifu upepo, linaanzia hapo na linakuwa kubwa utafikiri la watu waliowahi kupigana, kumbe hawajawahi kukutana hata siku moja.

Tandale:
Hii ndiyo hoja ya nne ambayo ninaamini inachangia kwa kiasi kikubwa kumtafuna Diamond. Kumfananisha na Sugu, haina maana wanafanana kwa kuwa hata muziki wanaopiga haulingani kwa asilimia mia.

Nimetengeneza mfano unaokumbusha zamani na sasa, pia wale waliotamba hadi nje ya Tanzania na kufikia kujulikana Ulaya na Marekani hata kama ni kwa Waafrika tu. Lakini utaona kwa Sugu, sikuzungumzia suala la Tandale ambako alikulia Diamond.

Sugu alikuwa akirudi Mbeya, aliimba na kuusifia mkoa huo, alionyesha mapenzi kwa watu wa eneo alilozaliwa na kukulia, aliisifia Mtwara aliyosoma shule hata kama alifeli, leo ni Mbunge wa Mbeya, huu ni mfano, aliwajali, nao wakamjali.

Tunajua ni mwenyeji wa Kigoma, lakini maisha yake wakati akifanya biashara ya kuuza mitumba, ndiyo sehemu ambayo ina watu wake, utaona hata alipoimba wimbo wa ‘Mbagala’, ilikuwa rahisi kwake kutoka na kupata sapoti kubwa.

Mafanikio yake yamemfanya abadilike, aishi Kimarekani, asahau watu wake hali inayojenga hisia za kudharau alikotoka au kutowajali watu wake ambao walikua naye. Siku zote mbwembwe sana hujengwa na msingi wa kiburi, kitu ambacho watu wengi hawapendi.

Kila mtu anapenda kuheshimiwa, kupendwa na kupewa kipaumbele. Diamond amejisahau kwa watu wake na huu ndiyo wakati wa kurudi Tandale na ikiwezekana Buzebazeba kule Kigoma na kuonyesha yeye kweli ni mtu wa watu.

Bila mashabiki hakuna Diamond, kuna kila sababu ya kuwaonyesha watu unawajali, unawathamini kwa kuwa ubora wa kazi zake umesukumwa kwenye mafanikio na watu hao na kufanya hivyo ni kuonyesha anawajali.

Huenda angeweza kutoa gari kwa Wema Sepetu au yeye kuzawadiwa kwenye siku yake ya kuzaliwa, lakini hakuna ambaye angeshangazwa au kutofurahia kama watu waliwahi kusikia alitoa gari la wagonjwa au alichangia kwa kununua gari la wagonjwa katika Hospitali ya Tandale, eneo moja la Mbagala, kokote jijini Dar es Salaam, kwao Kigoma au sehemu yoyote ile ya Tanzania.

Jamii ndiyo inayofanya uingize au kutengeneza, kuijali ni lazima na hili Diamond anaweza kujifunza kupitia gazeti hili la Championi ambalo kila wiki linaendelea kutoa zawadi za jezi, mipira, runinga, simu kwa wasomaji wake kuonyesha linawajali na kuthamini mchango wao, hakuna gazeti jingine linafanya hivyo, labda lianze wiki ijayo.

Kuishi Kimarekani sana si jambo baya, lakini kuishi Kitanzania ndiyo sahihi zaidi kwa kuwa hapa ni Tanzania. Inawezekana kwa Diamond linaweza kuwa jambo gumu lakini jamii iliyompa umaarufu, fedha na ukubwa alionao ni ya wa Tanzania, hivyo lazima awajali Watanzania na Tandale ingeweza kuwa ya kwanza, kwingine kukafuatia.


1 COMMENTS:

  1. Katika muda ambao Saleh umeutumia vizuri na mola wako atakulipa ni wakati wa kuandika waraka huu kwa Diamond na wasanii wengine kwa ujumla!

    ReplyDelete

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic