November 1, 2014


Na Saleh Ally
HAKUNA mwenye uhakika kama kweli Lionel Messi ndiyo anakwenda ukingoni au ni kipindi cha mpito na makali yake yatarejea tena.
Pia hakuna mwenye uhakika, Barcelona itaendelea kung’ara au taratibu inaendelea kutembea kwenye mteremko wa “bye bye” ufalme.


Kikosi cha Barcelona kimemtangaza Javier Mascherano kuwa mchezaji bora wa kikosi hicho kwa msimu uliopita. Tuzo ambayo aliichukua Messi mfululizo miaka mitatu!

Wakati Messi anakosa tuzo hiyo ya ndani ya Barcelona, kwenye Tuzo za La Liga, Barcelona na Messi wameonekana kupwaya kupita misimu mingine yote kwa kipindi cha zaidi ya miaka mitano.

Real Madrid ndiyo inaonekana kushika hatamu, inaonekana kuwa juu zaidi huku mpinzani mkubwa wa Messi, Mreno Cristiano Ronaldo, akipiga ‘hat trick’ ya tuzo.


Ronaldo amekuwa Mchezaji Bora, Mfungaji wa Bao Bora na Mshambuliaji Bora wa La Liga. Messi ameambulia patupu pia.

Madrid imeendelea kutamba kwa kutwaa zawadi nyingine tatu za Kiungo Bora (Luka Modric), Beki Bora (Sergio Ramos) na Kipa Bora (Keylor Navas) ambaye ameshinda kutokana na kazi yake nzuri msimu uliopita akiwa na Levante.



Barcelona ilichukua tuzo tatu, Andrés Iniesta alitangazwa kuwa kiungo bora mshambuliaji, huku Ivan Rakitic na Rafinha wakitwaa tuzo mbili za Fair Play na mchezaji aliyechipukia.

Utaona Barcelona imeondoka kwenye zile tuzo tatu kubwa za La Liga, yaani mchezaji bora, kiungo bora, beki bora au bao bora na imebaki kwenye Fair Play na mchezaji anayechipukia.

Barcelona ndiyo ilikuwa ikitawala tuzo hizo kwa kiasi kikubwa. Lakini kadiri siku zinavyosonga, imeanza kuonekana ya kawaida sana.

Si timu inayoogopeka tena na kila kitu kinaonyesha mabadiliko ya makocha tokea Pep Guardiola, hadi kufikia Luis Erinque, yanaweza kuwa chanzo na Barcelona inahitaji muda.

Kumalizika kwa kiwango cha Xavi Hernandez ambaye sasa anaingia au hamalizi dakika 90, tayari kumetibua ubora wa pembe tatu hatari zaidi duniani katika zote iliyokuwa ikiundwa na Xavi, Iniesta na Messi.

Kazi kubwa kwa kocha Enrique, lazima atengeneze kitu tofauti au kutengeneza pembe tatu nyingine ambayo itamchukua muda.

Lazima mashabiki wa Barcelona wakikubali kipindi hicho cha mpito. Wapo wanaoweza kuuliza kama wamezama, ukweli kwa kipindi hiki unaweza kusema wanakaribia kuzama.

Lakini kwa kikosi walichonacho, wakipata huo muda, wakaendelea taratibu na kuzoeana, wageni wakazoea utamaduni wa uchezaji, basi Barcelona inaweza ikaibuka na kurudi kwenye ubora uleule.

Angalia mechi ya El Classico pale Bernabeu, Messi alikuwa haonekani, utafikiri alikuwa ‘likizo’. Kuna jambo la kufanya kwake na kwa Enrique kwa kuwa Barcelona ya sasa, si ile yenye makali na msisimko iliyokuwa tishio kwa kila mpinzani.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic