December 29, 2014


HAMU yangu kubwa ilikuwa ni kuona kama kweli uwezo wa Amissi Tambwe kufunga mabao umekwisha kabisa.
Niliingia kwenye ubishi mkubwa na mmoja wa viongozi wa Simba wakati tukijadili taarifa za kutaka kuachwa kwa Tambwe.


Alinipa sababu nyingi ambazo kwa asilimia 90 niliona hazina msingi msingi na hasa aliponiambia Tambwe hakuwahi kuwatoka hata mabeki wawili.

Badala yake amekuwa akifunga mabao yake kwa kuvizia tu, nilimtolea mfano wa Ruud van Nisterlooy alivyoisaidia Man United kutwaa ubingwa akifunga mabao hayo ya ndani ya 18.

Lakini nilimkumbusha kwamba nina ushahidi wa picha za Tambwe akikimbizana mabeki wawili akiwa nje ya 18 na si kweli kwamba alikuwa hana uwezo wa kumtoka beki hata beki mmoja.

Wakati mwingine kunaweza kukawa na taarifa, mchezaji akazushiwa kitu na kila mmoja akakipokea na kuona ni kweli hata bila ya kujiuliza au kuchunguza naye akawa anasambaza, mfano hilo kwamba Tambwe anasubiri kufunga tu, yupi mwenye uhakika?

Yule kiongozi alipoona hoja zangu zina nguvu, akahamia na kunieleza ni mfumo wa Kocha Patrick Phiri ndiyo uliomkataa Tambwe na anaonekana ameshindwa  kuendana nao.

Lakini nilipozungumza na Phiri, akaniambia hakuwahi kuwa na mpango wa kumuacha Tambwe na si lahisi kuona kocha akitaka kumuacha mfungaji bora wa msimu uliopita, hata angekuwa majeruhi, labda aambiwe hawezi kucheza msimu mzima!

Ingawa sijui mpira, lakini nilikuwa nina maswali mengi sana kama kweli Tambwe hawezi tena kufunga na hasa juzi nikiishuhudia Simba ikicheza dakika 90 dhidi ya Kagera Sugar bila ya kufunga hata bao moja.

Lakini jana kwa mara ya kwanza Tambwe akiichezea Yanga katika mechi ya ligi, alifanikiwa kufunga bao lake la kwanza na la pili msimu huu.

Tambwe raia wa Burundi ameifungia Yanga bao ndani ya dakika 7 tu akiwa anaichezea. Siku moja nyuma kama nilivyoeleza, Simba hawakuweza kufunga hata bao moja.

Lengo langu si kulinganisha, au kuonyesha lazima 
Tambwe atafunga mechi zote zijazo, lakini hii inaonyesha kuna baadhi ya mambo huwa hayaendi kitaalamu.

Hasa mambo ya kuamini kuliko hali halisi. Kusema Tambwe hawezi kufunga kisa anasubiri au kuvizia tu, si sahihi hata kidogo. Na uwezo wa Tambwe kufunga, hauwezi ukamalizwa na mfumo.

Hata ukiliangalia bao la kichwa alilofunga dhidi ya Azam si lahisi kusema ni mfumo au mafunzo mazuri ya Kocha Hans van der Pluijm, badala yake ni uwezo binafsi.

Ulikuwa ni mpira wa krosi ulioingia ndani na Tambwe alichofanya ni kumzidi kasi beki wa Azam, akawahi na kuupiga kichwa. Bao lake ndiyo lilisaidia kuirudisha Yanga mchezoni baada ya kuwa imefungwa katika dakika ya tano tu baada ya uzembe wa Mbuyu Twite.

Simba ina haki ya kumuacha Tambwe, lakini ilipaswa kueleza sababu nyingine za msingi, si zile ilizozitoa. Nidyo maana bado ninaamini na huu ndiyo ukweli kuwa Simba ilikurupuka kumuacha Tambwe au hata lengo la kumuacha halikuwa madhubuti kulingana na sababu zilizotolewa.

Huenda ni matakwa ya wachache wenye sauti ya kusema ndani ya Simba au wanaoamini kweli amekuwa akivizia, hakuwahi kumpita beki, amekwisha, mzee na vinginevyo.

Inawezekana kabisa hata wao walipitisha uamuzi huo baada ya kuambiwa wakaamini. Hakuna aliyefanya tathmini. Hata angekuwa anavizia, lakini kama anafunga, basi ni jambo zuri. Kama havizii, anakimbia sana na mpira, halafu hafungi, faida yake ni nini?

Kwangu Tambwe amenipa somo, niliposikia ataachwa kwa mara ya kwanza. Nilijiuliza maswali mengi na moyo wangu ukakataa lakini nikataka kujiridhisha kwa kurudia kuangalia baadhi ya mechi zake za nyuma, bado sikukubaliana na nilichokiona.

Lakini baada ya bao lake la jana dhidi ya Azam FC, nimeamini kuna tatizo na nalichukua kama somo. 

Yoyote atakayetaka kuungana nami tujifunze awe huru, atakayeona kilichofanyika ni sahihi, pia sawa, kila mtu aamini kivyake.



0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic