December 29, 2014


Na Saleh Ally
MECHI saba za mwanzo za Ligi Kuu Bara kwa Simba zilikuwa na msukosuko mkubwa sana kutokana na mambo kutokuwa mazuri.

Gumzo la kwanza zilikuwa ni mechi sita za mwanzo ambazo timu hiyo ilitoka sare zote, likazuka suala la Kundi la Ukawa ambalo zaidi lilitawaliwa na hisia za kishirikina.

Matokeo ya soka, hayapatikani kwa kuamini ushirikina, badala yake maandalizi ya kutosha, kumsikiliza mwalimu anayepaswa kuwa bora na ushirikiano wa kutosha uwanjani.

Baada ya mechi sita za sare ambazo zilizua mengi kama uongozi wa Simba kufanya mazungumzo na Kim Poulsen ikitaka kumleta kuchukua nafasi ya Patrick Phiri.
Usisahau, viungo watatu, Shabani Kisiga, Haruna Chanongo na mkongwe mwingine Amri Kiemba walisimamishwa. Mwisho waliondolewa, aliyebaki ni Kisiga ambaye ‘uhai’ wake Msimbazi unaonekana ni wa mashaka hadi sasa.

Mechi moja kabla ya ligi kusimama, Simba ilifanikiwa kushinda kwa bao 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting na kuamka morali huku Wanasimba wakiamini tabu imekwisha na maumivu sasa basi.

Kabla ya kurudi kwenye ligi, Simba imecheza mechi tatu kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar, zote za kirafiki.
Kwanza dhidi ya Express ya Uganda, ikawa ni sare ya bila mabao. Halafu dhidi ya Yanga ambayo ilishinda kwa mabao 2-0, furaha ikatawala na sasa ikaonekana Simba imeiva na sare sasa basi, kosa la kwanza lakini pia wakaichapa Mwadui ya Jumhuri Kihwelo 3-1.

Simba imeweka rekodi mpya ya kuwa timu ya kwanza nchini, kusajili wachezaji wake wageni wote kutoka nchini moja. Wachezaji wake watano, wote ni raia wa Uganda.

Kuna mabeki, Joseph Owino, Juuko Murishid, viungo washambuliaji, Danny Sserunkuma, Simon Sserunkuma na Emmanuel Okwi. 

Kwa wachambuzi wa mambo, hofu ilitawala kuona Simba ikisajili Waganda wote, lakini uongozi ulisisitiza ulichoangalia ni kiwango.
Inawezekana mengi yakasemwa, lakini hili litakuwa ni kosa la pili la Simba kuwa na timu ndogo ndani ya timu kubwa.

UGANDA:
Timu ndogo ya Waganda ambayo kama itaamua kutengeneza kiota chake ndani ya kikosi hicho, lazima kitazua mfarakano wa chinichini baina ya Waganda na Watanzania na kusababisha ‘matobo’ ya ndani.

Vigumu kwa sasa kukubali kwamba kunaweza kuwa na tatizo, uongozi hauwezi kuliona hili kwa sababu hautaki kuonekana umekosea. Lakini kiroho safi kabisa, hili litaisumbua Simba baadaye.

Litaisumbua kutokana na tabia za Waganda na hii imekuwa ni kawaida. Utaona Okwi na Owino walivyochelewa kurejea kambini mara ya kwanza.

Lakini utaona safari ya pili namna Waganda hao walivyochelewa kwa mara nyingi na athari ipo hivi; zamani alipochelewa Okwi na Owino, Warundi Amissi Tambwe na Pierre Kwizera ambao walionyesha nidhamu ya juu, walikuwa wakiwahi sana.

Lakini sasa kama Waganda wana tabia za kuambiana, basi wanapochelewa wote watano ni pengo kubwa kwa makocha ambao wanataka kwenda na prpgramu zao.

MFUMO:
Mfumo wa klabu zetu si mzuri, wachezaji wanaowaomba ruhusa viongozi badala ya makocha. Kocha hana la kusema ingawa kiutendaji ndiye anakuwa muathirika namba moja.

Taarifa za kwamba al manusura Simba ‘imwage’ Phiri mara tu baada ya kufungwa na Kagera zimezagaa. Lakini bado utaona kuna makosa mengine hahusiki, nitafafanua.
Wakati Waganda wanapoingia kambini wamechelewa, hakuna ubishi hawawezi kuwa fiti sahihi kama wale walioanza mazoezi mapema kwa kufuata kilichotakiwa, mfano kufika kambini mapema.

MORALI:
Kingine ni kuuwawa kwa morali ya baadhi ya wachezaji. Kwamba wanapotakiwa  kufika mazoezini, basi wale Wazalendo wanawahi kufika kama ilivyotakiwa.

Halafu wageni ambao ni Waganda wanafika wamechelewa huenda siku mbili kabla ya mechi. Halafu baada ya hapo siku ya mechi, kama si wote basi angalau watatu wanaanza na wengine wako benchi.
Wale baadhi Wazalendo, wanalazimika kukaa jukwaani kabisa. Inawezekana ikawa ni ishu ya uwezo kweli, lakini angalia kuhusiana na ukweli na suala la nidhamu.

Hii inajenga matabaka, inasambaza chuki taratibu na mwisho ‘matobo’ ndani ya Simba na inaweza kuwashangaza wengi kuona Simba inaanguka wakati ndiyo ina kikosi bora.

Angalia, Simba iliyoonekana haina kikosi bora, ililaumiwa kwa sare mfululizo lakini haikuwahi kupoteza mchezo.

Sasa ina kikosi bora chenye wachezaji wa Uganda walio na uzoefu, imepoteza mchezo. Hapa kuna mengi ya kujiuliza na uongozi wa Simba unapaswa kuyatilia maanani mambo ambayo yanaonekana ni kama madogo lakini sivyo.

Inawezekana kabisa viongozi wa Simba wakatumia nguvu nyingi kulazimisha ionekane si tatizo au haiwezi kuwa tatizo.

Ushauri, walione hili ni tatizo na kuanza kulishughulikia mapema kwa kuwa ligi ya sasa, si ya mwaka jana, timu nyingi zimejiandaa, angalau zina Sh milioni 100 za Azam TV na maandalizi yanaweza kuwa bora kuliko zamani.

 Kingine, lazima uongozi wa Simba usisitize usawa kwa maana ya nidhamu. Wale wachezaji Waganda wasitengenezewe daraja la juu utafikiri hawaishi Afrika Mashariki.

Ubora wa watu watano katika timu ya watu 28, hauwezi kukamilisha ubora wa kila kitu. Hivyo wanapaswa kuamini wao ni sehemu ya timu na wanaunganishwa na ushirikiano wao na wenyeji.

Hakuna ubishi wala hadithi, Waganda hao wanapaswa kuwaheshimu Watanzania, kuiheshimu Tanzania inayowapa maisha. Hakuna kikosi au timu inayoweza kufanikiwa kama miongoni mwa wahusika, hakuna heshima na upendo.





0 COMMENTS:

Post a Comment

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic