December 8, 2014




Na Saleh Ally
NIANZE na kukumbusha baadhi ya mengi ambayo nimewahi kuzungumza, kwamba soka yetu Tanzania imetawaliwa na mizengwe zaidi kuliko hali halisi.


Soka ni burudani, lakini soka ni biashara kubwa inayoweza kulinganishwa na zile ghali kama za uuzaji mafuta au madini.

Hakuna anayeweza kukataa katika hilo, angalia katika mechi moja ya soka kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam, zimewahi kuingia hadi Sh milioni 700. Si mchezo, si kitu kidogo na si rahisi kutokea, biashara zenye uwezo huo kwa muda mchache kama huo, ziko ngapi? Zitaje!

Nauchukulia mchezo wa soka kama ajira kubwa kabisa ambayo ingeweza kuwakomboa Watanzania wengi na kuachana na kuamini kila mwenye maisha bora lazima awe amekwenda shule na kupata digrii au ‘mastaz’.


Hata Ulaya haiko hivyo, wachezaji wanalipwa mamilioni ya fedha kuliko hata maprofesa, huo ni mfumo mzuri wa mgawanyo wa ajira, waliosoma na wasiosoma lakini wenye vipaji vyao, nao wanaweza kuishi maisha bora.

Viongozi wengi wa soka nchini kuanzia kwenye Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), klabu kubwa kama Yanga, Simba na nyinginezo si wale wanaotaka maendeleo, wenye mawazo au mipango endelevu.

Viongozi hao ndiyo wamekuwa wakiua nguvu ya mchezo wa soka na kuugeuza kutoka ule unaoweza kutengeneza mamilioni kwa ajili ya wahusika na maendeleo ya taifa letu kwa jumla, hadi kuwa mchezo wa chuki, malumbano.

Lakini wachezaji nao, wanaamka, wanaliona hilo. Wanaweza kubadilika na kuachana na kuamini ushirikina? Wanaweza kupunguza hadi kuondoa chuki ya wao kwa wao?

Hebu angalia tukio hili lililotokea kule Ujerumani, mshambuliaji Mario Gotze wa Bayern Munich amekitoa kiatu chake kimoja tu cha mguu wa kushoto, kimeuzwa kwa euro milioni 2 (Sh bilioni 4.2).

Kiatu hicho aina ya Nike ndiyo kiliugusa mpira mara ya mwisho wakati Gotze alipopiga shuti na mpira kujaa wavuni, likawa ndiyo bao pekee wakati Ujerumani ilipoiangusha Argentina kwa bao 1-0 katika fainali ya Kombe la Dunia.

Gotze ambaye hakuwahi kukisafisha kiatu hicho tangu fainali, alikubali fedha ziwasaidie watoto kupitia mradi wa 'A Heart for Children', lakini hakuna aliyejua kitafikia bei hiyo.

Sasa kitasaidia watoto, hii ndiyo nguvu ya soka. Angalia, kiatu kinauzwa kwa fedha zaidi ya gari la kifahari, zaidi ya jumba la kifahari, zaidi ya thamani ya mishahara ya wachezaji wote wa Ligi Kuu Bara ikiwezekana kwa nusu au msimu mzima!

Fedha hizo kama zingeletwa hapa nyumbani, Yanga na Simba wangeweza kupata uwanja. TFF ingeweza kujenga uwanja mwingine na kupata fungu la kukuza watoto wenye vipaji, si kama vile ilivyotaka kuchukua asilimia 5 za fedha za wadhamini za klabu.

Mchezo wa soka uko hivi, unavyozidi kuuthamini na thamani yake inapanda. Ujerumani wamejiandaa vema, wana programu nzuri ya vijana. Matunda yao ilikuwa ni kuendelea kufikia kwenye Kombe la Dunia.

Gotze amefunga kwa kuwa wamefika Kombe la Dunia, kiatu chake kimeuzwa bei kubwa kwa kuwa wako kwenye mashindano makubwa kama hayo. Jiulize wamefikaje? Jiulize wangetanguliza majungu, ushirikina, ulafi wa fedha za mashirikisho au klabu, wangefika hapo?


2 COMMENTS:

TwitterFacebookGoogle PlusLinkedInRSS FeedEmail

GONGA HAPA KWENDA AZAM TV

B2.jpg
Image and video hosting by TinyPic